24/05/2026
Ukiukaji usalama Ganze
Jeshi la polisi nchini kupitia ofisi ya Inspekta jenerali limethibitisha kutokea kwa ukiukaji wa usalama leo tarehe 24 Mei 2026 katika eneo la Ganze, Kaunti ya Kilifi, wakati rais William Ruto alikuwa akihutubia wananchi katika hafla ya shukrani ya katibu mkuu Fikirini Jacob .
Kupitia taarifa rasmi kwa vyombo vya habari, polisi walisema vikosi vya usalama vilichukua hatua za haraka kudhibiti hali hiyo na kurejesha utulivu, huku tukio hilo likitajwa kuwa la kuhatarisha usalama wa rais na taifa kwa ujumla.
Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja amesema tayari ameunda kikosi maalum cha uchunguzi kuchunguza kwa kina namna tukio hilo lilivyotokea. Aidha, mabadiliko ya haraka yamefanywa kwa maafisa waliokuwa wakisimamia usalama wa rais ili kuimarisha taratibu za kiusalama.
“Tukio lolote linalohatarisha usalama wa mkuu wa nchi halitavumiliwa na litashughulikiwa kwa uzito mkubwa,” sehemu ya taarifa hiyo ilisema.
Polisi pia wamewataka wananchi wanaohudhuria hafla za viongozi wa kitaifa kufuata kikamilifu taratibu za usalama zilizowekwa, wakionya kuwa yeyote atakayekiuka sheria atachukuliwa hatua kali za kisheria.
Jeshi la Polisi limehakikisha wananchi kuwa linaendelea kuchukua hatua zote muhimu kuhakikisha matukio k**a hayo hayajirudii tena nchini.