03/06/2026
Taharuki kubwa imeikumba jamii ya Kijiji cha Imarabupina wilayani Chato mkoani Geita kufuatia madai ya mwanafunzi wa shule ya sekondari kutekwa na kufanyiwa ukatili wa kijinsia na mtu aliyedaiwa kumtaka mama mzazi wa mtoto huyo kumpatia kiasi cha fedha. Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa, mwanafunzi huyo alikuwa amerejea nyumbani kuchukua madaftari
aliyoyasahau shuleni ndipo alipokumbana na mtuhumiwa ambaye anadaiwa kumchukua kwa nguvu na kumpeleka katika eneo la pori la Burigi-Chato ambapo tukio hilo la kusikitisha lilitokea.
Akizungumza kuhusu tukio hilo, mama mzazi wa mwanafunzi huyo amesema alipigiwa simu na mtuhumiwa akitaka apewe fedha ili amwachie mtoto wake, jambo ambalo lilimshangaza kutokana na kutokuwa na uwezo wa kutoa kiasi hicho. Baada ya kupokea taarifa hizo, alitoa taarifa kwa viongozi wa eneo husika na mamlaka zinazohusika, ambapo hatua za haraka zilianza kuchukuliwa kwa lengo la kumtafuta mtoto na kuhakikisha haki inapatikana
Kufuatia tukio hilo, viongozi mbalimbali wakiwemo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Geita wametembelea familia ya mwanafunzi huyo kutoa pole na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano katika kutoa ushahidi utakaosaidia uchunguzi na hatua za kisheria. Wakati huo huo, Jeshi la Polisi limethibitisha kumkamata mtuhumiwa na linaendelea na uchunguzi wa kina ili kubaini ukweli wa tukio hilo kabla ya hatua stahiki za kisheria kuchukuliwa.