04/02/2026
🛑ARUSHA, TANZANIA
RC MAKALLA ATANGAZA KAMATI 7 ZA MAANDALIZI YA AFCON 2027, ARUSHA
Asema Kuundwa kwa Kamati hizo ni kuonesha utayari wa Arusha kwa AFCON
Wananchi, wenye Mahoteli, Makampuni ya utalii na usafirishaji wahimizwa kuchangamkia fursa
Aagiza Jiji Arusha kuhimiza usafi na kupendezesha Jiji la Arusha
Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla leo Jumanne Februari 04, 2026 ametangazwa kuundwa kwa Kamati Saba Maalumu kwaajili ya maandalizi ya Michuano ya Mpira wa Miguu kwa Mataifa ya Afrika, AFCON 2027.
Mbele ya Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi na Wenyeviti wa Halmashauri, Makatibu Tawala, Waganga wakuu na Maafisa Tarafa wa Mkoa wa Arusha, Mhe. Makalla amesema kuundwa kwa Kamati hizo ni kuonesha utayari wa Mkoa kuwa Mwenyeji wa michuano hiyo mikubwa zaidi barani Afrika.
Amemuelekeza Kaimu Katibu Tawala mkoa kuunda kamati hizo 7 ikiwemo Kamati ya Usalama, Kamati ya Itifaki na Mapokezi, Kamati ya Habari, Mawasiliano na Hamasa, Kamati ya Afya, Kamati ya Malazi, ya Miundombinu pamoja na kamati ya utalii na ukarimu.
Katika hotuba yake, Mhe. Makalla amewataka wananchi, wamiliki wa Mahoteli, Makampuni ya Utalii na usafirishaji kuchangamkia fursa za kiuchumi za Ujio wa michuano hiyo, akiagiza Jiji la Arusha pia kuhimiza usafi na kuongeza jitihada za kupendezesha maeneo ya Jiji hilo.
Aidha, Mhe. Makalla amemshukuru Mhe. Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuichagua Arusha na kujenga uwanja wa kisasa wa 'category 4' wenye sifa za CAF na kuahidi kushirikiana na watalamu wa ngazi zote kusimamia kikamilifu maandalizi yote ili kuhakikisha Taifa linapata sifa pamoja na ushiriki wa wananchi waweze kujipatia kipato.