29/09/2025
MATOKEO mabovu katika mechi mbili mfululizo yamemtibulia Kocha wa Chelsea, Enzo Maresca kwa mashabiki wengi wakitaka aondoke, lakini mabosi wa mabingwa hao wa Dunia wamesema bado wanamwamini na watamjadili mwisho wa msimu.
Chelsea ilikumbana na kichapo cha pili mfululizo Ligi Kuu England kutoka kwa Brighton wikiendi iliyopita cha mabao 3-1 nyumbani, baada ya kutoka kuchapwa na Manchester United mabao 2-1 ugenini.
Hata hivyo, licha ya kelele hizo za mashabiki, mabosi wa wababe hao wa darajani, wanaamini kocha huyo bado anaweza akatimiza malengo ambayo wamemwekea na anahitaji kuendelea kupewa muda ili kujenga timu na walishawishika sana kutokana na kiwango ilichoonyesha Chelsea katika michuano ya Kombe la Dunia la Klabu.
Mashabiki walikataa utetezi wa Maresca aliyedai timu imepoteza mechi hizo mbili kwa sababu ya kadi nyekundu, wakidai kadi haikuwa sababu bali kocha huyo ameshindwa na hana kiwango cha kuipa mafanikio timu yao.
Hata hivyo, kadi hizo nyekundu za Robert Sanchez na Trevoh Chalobah zinachukuliwa kwa uzito mkubwa na viongozi wa juu wa klabu ambao wanaamini zimechangia sana timu kufanya vibaya.
Akiwa na Chelsea, Maresca amepoteza mechi tano tu katika miezi sita iliyopita na katika mechi hizo, nne kati ya hizo timu hiyo ilimaliza ikiwa pungufu.