09/12/2025
Jeshi la Polisi Tanzania limesema hali ya usalama nchini imeendelea kuwa shwari hadi kufikia mchana wa Desemba 9, 2025, siku ambayo baadhi ya watu wamepanga kufanya maandamano yanayodaiwa kuwa ya amani, huku Serikali na vyombo vya ulinzi na usalama vikisema maandamano hayo si halali.
Kwa mujibu wa taarifa ya Msemaji wa Jeshi la Polisi Tanzania, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) David Misime, vyombo vya ulinzi na usalama vinaendelea kuimarisha hali ya usalama na kulinda maisha na mali za wananchi kote nchini.
Polisi imewataka wananchi kupuuza picha mnato na picha mjongeo zinazoenezwa mitandaoni zikidai kuwa maandamano yameanza sehemu mbalimbali za nchi, ikibainisha kuwa picha hizo ni za matukio ya zamani zikiwemo zile za Oktoba 29, 30 na 31, 2025.