02/04/2026
Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini imefanya hafla fupi kwa ajili ya kushukuru ushirikiano wa wataalamu wa REA kutoka makao makuu Dodoma, ambao leo wamehitimisha ziara maalum katika jimbo hilo ya kukagua maeneo yenye changamoto ya umeme.
Katika ziara hiyo, wataalamu wa REA walifanikiwa kupitia zaidi ya mitaa 39, wakifanya tathmini ya kina ili kubaini maeneo yenye uhitaji wa huduma ya umeme, kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo muhimu.
Ziara hii imekuja kufuatia swali lililoulizwa Bungeni na Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini, Ester Amos Bulaya, kuhusu mitaa inayokabiliwa na changamoto ya umeme.
Hafla hiyo, iliyofanyika katika eneo la Heriath mjini Bunda, iliambatana na chakula cha mchana na kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, chama, viongozi wa dini pamoja na wananchi.
Baadhi ya viongozi walipata nafasi ya kuzungumza.