14/10/2025                                                                            
                                    
                                                                            
                                            Mtoto Josiah Mwambene, aliyemaliza darasa la saba katika Kijiji cha Majengo, wilayani Mbozi, mkoani Songwe, amefariki dunia katika mazingira ya kushangaza baada ya kudonolewa na kuku tetea kwenye paji la uso.
Tukio hilo limezua simanzi na taharuki kubwa miongoni mwa wakazi wa eneo hilo, huku baadhi wakihusisha kifo hicho na imani za kishirikina kutokana na mazingira ya tukio hilo.
Kwa mujibu wa ndugu wa marehemu, Raphael Mtafya, marehemu Josiah alikuwa mwanafunzi mwenye uwezo mkubwa kitaaluma na katika mahafali ya shule yao alitambuliwa rasmi kwa kupokea zawadi maalum kutokana na ufaulu wake.
“Usiku wa siku hiyo, akiwa amelala, ghafla aliamka akipiga kelele akidai kuvamiwa na kuku tetea aliyemdonoa usoni. Tuliona jeraha dogo tu, tukadhani si tatizo kubwa,” alisema Mtafya.
Hata hivyo, siku chache baadaye Josiah alianza kulalamika maumivu ya kichwa, jicho kuvimba, na baadaye akaanza kuharisha. Alipofikishwa hospitalini, madaktari walieleza kuwa hakukuwa na ugonjwa ulioonekana wazi, jambo lililowafanya wazazi wake kumpeleka kanisani kwa maombi. Licha ya jitihada hizo, hali yake iliendelea kuwa mbaya hadi alipofariki dunia.
Wakati baadhi ya wananchi wakihusisha tukio hilo na imani za kishirikina, wataalam wa afya wamesema huenda kifo hicho kimetokana na maambukizi ya bakteria hatari yaliyosababishwa na jeraha alilopata baada ya kudonolewa na kuku huyo.