14/06/2026
Jeahi la Polisi Mkoa wa Arusha limekanusha vikali taarifa zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii zikituhumu uwepo wa askari polisi aliyepigwa mkoani humo, likitaja maudhui hayo kuwa ni ya uongo na yenye lengo la kuchochea taharuki katika jamii.
Ufafanuzi huo umetolewa leo, kupitia taarifa rasmi kwa umma iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, kufuatia kusambaa kwa picha mjongeo (video) iliyochapishwa na mwanaharakati Maria Sarungi ikidai kuwa tukio hilo limetokea mkoani humo.
Jeshi hilo limebainisha kuwa hakuna tukio lolote la namna hiyo lililotokea ndani ya Mkoa wa Arusha na uchunguzi wa awali unaonyesha wazi kuwa video hiyo ilichukuliwa maeneo mengine nje ya nchi, kisha kuwekewa maneno ya uongo ili kuaminisha umma vibaya.
"Tunawaomba wananchi kupuuza taarifa hiyo, kwa kuwa mtu huyo amekuwa akiandaa na kusambaza maudhui ya uongo, uchonganishi na kutaka kuleta taharuki kwa jamii jambo ambalo ni kinyume na makuzi, mila, desturi na mifumo ya kisheria," amesema Kamanda wa Polisi mkoani humo kupitia taarifa hiyo.
Mbali na kukanusha, jeshi hilo limetoa onyo kali kwa watu wote wenye tabia ya kuandaa, kusambaza taarifa za uongo, na kupandikiza chuki ili kuchonganisha jamii, likisisitiza kuwa vitendo hivyo ni kinyume cha sheria za nchi na hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayebainika kukiuka taratibu hizo.