
04/07/2025
Waziri Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed, ametangaza kukamilika kwa bwawa la umeme lenye utata linalojengwa kwenye Mto Nile, na kusema kuwa hatua hiyo ni mafanikio makubwa kwa taifa lake licha ya mvutano wa muda mrefu na mataifa jirani, hususan Misri na Sudan.
Akihutubia wabunge jijini Addis Ababa hapo jana, Abiy alisema serikali yake inaandaa uzinduzi rasmi wa mradi huo mkubwa wa umeme unaofahamika k**a Grand Ethiopian Renaissance Dam (GERD) mnamo mwezi Septemba. Bwawa hilo, ambalo ujenzi wake ulianza mwaka 2011, limeigharimu Ethiopia takribani dola bilioni nne na linatajwa kuwa mradi mkubwa zaidi wa nishati barani Afrika.
Licha ya mvutano wa muda mrefu kuhusu mgao wa maji ya Mto Nile, Abiy alisisitiza kuwa maendeleo ya Ethiopia hayataleta madhara kwa mataifa jirani. "Tunaamini kuwa maendeleo ya taifa moja hayapaswi kuwa mzigo kwa mwingine. Maendeleo ya Ethiopia ni kwa ajili ya ustawi wa wote," alieleza Abiy mbele ya Bunge.
Kwa miaka kadhaa, Ethiopia na Misri zimekuwa katika mvutano mkali kuhusu bwawa hilo, ambapo Misri imekuwa ikieleza hofu zake kuwa mradi huo unaweza kupunguza kiwango cha maji ya Mto Nile inayokitegemea kwa asilimia kubwa kwa matumizi ya nyumbani, kilimo na viwanda. Sudan pia imekuwa na mashaka kuhusu athari za kiusalama na kiikolojia zitakazotokana na mradi huo.
Tangazo la kukamilika kwa bwawa hilo linaashiria mwanzo mpya wa mwelekeo wa kisiasa, kiuchumi na kidiplomasia katika ukanda huo wa Afrika Mashariki na Kaskazini. Macho sasa yanaelekezwa kwenye uzinduzi rasmi wa mradi huo na mazungumzo ya kidiplomasia yatakayofuata kati ya Ethiopia, Misri na Sudan.
Waziri Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed, ametangaza kukamilika kwa bwawa la umeme lenye utata linalojengwa kwenye Mto Nile, na kusema kuwa hatua hiyo ni mafaniki...