13/12/2025
Ziara ya Mbunge wa Jimbo Jipya la Katoro Yaweka Msingi wa Utekelezaji wa Ahadi za Barabara na Afya
Baada ya kugawanywa kwa Jimbo la Busanda na kuundwa kwa majimbo mawili ya Katoro na Busanda, Mbunge wa Jimbo jipya la Katoro, Mhandisi Kija Limbu Ntemi, ameanza rasmi utekelezaji wa ahadi alizotoa kwa wananchi wakati wa kampeni, kwa kuweka kipaumbele katika uboreshaji wa miundombinu ya barabara na huduma za afya, maeneo yaliyokuwa changamoto kwa muda mrefu katika wilaya hiyo.
Alhamisi, Mbunge Ntemi alifanya ziara ya kukagua ujenzi wa mitaro ya kupitisha maji katika maeneo mbalimbali ya Katoro, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kulinda barabara dhidi ya athari za mvua na maporomoko. Mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya Jonta Investment Limited ya Mkoa wa Shinyanga, unafadhiliwa na Benki ya Dunia kwa zaidi ya shilingi bilioni 1.299 na unahusisha ujenzi wa mitaro yenye urefu wa kilomita 5.25.
Akiwa katika ziara hiyo, Mbunge wa Katoro aliipongeza Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia katika kutekeleza miradi ya maendeleo, akieleza kuwa ujenzi wa mitaro hiyo utaongeza uimara wa barabara na kuboresha usafiri kwa wananchi. Aidha, aliwataka wakandarasi kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi na kuhakikisha ubora unazingatiwa ili kazi ikamilike kwa wakati uliopangwa.
Wahandisi kutoka TARURA Wilaya ya Geita walieleza kuwa utekelezaji wa mradi unaendelea vizuri, huku wakisisitiza umuhimu wa mkandarasi kuzingatia maelekezo yote ya kitaalamu ili kupata matokeo bora yanayokusudiwa. Wakazi wa Katoro nao walipongeza hatua hiyo, wakisema ni mwanzo wa suluhisho la changamoto ya barabara iliyokuwa ikiwasumbua kwa muda mrefu, hasa wakati wa mvua.
Siku iliyofuata, Ijumaa, Mbunge Mhandisi Kija Limbu Ntemi aliendelea na ziara yake kwa kutembelea Hospitali ya Wilaya ya Katoro, ambapo alipokea changamoto mbalimbali zinazohusu utoaji wa huduma za afya. Miongoni mwa changamoto hizo ni ukosefu wa njia ya watembea kwa miguu (walkway) ndani ya hospitali, hali inayosababisha usumbufu kwa wagonjwa, watumishi na wananchi wanaofika kupata huduma. Mbunge aliahidi kuwasilisha suala hilo kwa viongozi husika ili kupatikane ufumbuzi wa kudumu.