02/03/2025
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Mhe. Dkt. Doroth Gwajima, amesema atatembelea ofisi za Benki ya Stanbic ili kupata ufafanuzi wa takwimu zao kuhusu namna walivyowezesha wanawake kiuchumi kupitia mikopo nafuu. Lengo lake ni kuhakikisha Watanzania wengi wanapata taarifa hizo na kutumia fursa hiyo kuinuka kiuchumi.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Kanda ya Ziwa katika Wilaya ya Bukombe Mkoani Geita, Dkt. Gwajima alisema amesikia Stanbic wakieleza kuwa wametoa mikopo yenye thamani ya shilingi milioni 10 kwa wanawake.
Hata hivyo, alibainisha kuwa baadhi ya takwimu alizozisikia kutoka kwa benki hiyo ni mpya kwake, na huenda pia kwa wananchi wengine.
"K**a mimi sijawahi kusikia, basi kuna wananchi wengi pia hawajawahi kupata taarifa hizi. Nitatembelea ofisi za Stanbic ili nipate ufafanuzi wa kina na niweze kuwafikishia wananchi taarifa hizi kwa sababu Rais Samia ameweka mazingira mazuri yanayowawezesha wananchi kunufaika na fursa mbalimbali," alisema Dkt. Gwajima.
Katika maadhimisho hayo, Waziri Gwajima pia alisifu mchango wa Benki ya Stanbic kwa maendeleo ya taifa, akisema kuwa kwa kipindi cha miaka 30 ya uwepo wake nchini, benki hiyo imefanya kazi nzuri.
Kwa upande wake, Afisa Mkuu wa Biashara wa Benki ya Stanbic, Bw. Fredrick Max, alisema benki hiyo inaendelea kukua kwa kasi na imeendelea kuwahudumia Watanzania kupitia matawi yake 11, huku matawi mengine sita yakiwa mbioni kufunguliwa mwaka huu, ikiwemo tawi moja mkoani Geita.
"Tuna zaidi ya mawakala 1,500 nchini kote na tunatoa huduma bora za kibenki kidijitali. Ukuaji wetu umeambatana na ongezeko la wafanyakazi, ambapo sasa tuna zaidi ya 600 nchini nzima," alisema Bw. Max.
Aidha, alibainisha kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, Benki ya Stanbic kwa kushirikiana na benki mama ya Standard Bank Group, imetoa mikopo nafuu kwa Serikali ya Tanzania inayofikia zaidi ya dola bilioni 1 za Kimarekani. Kati ya hizo, dola milioni 600 zimetolewa na Stanbic Tanzania na Standard Bank Group, huku kiasi kingine kikitolewa na washirika wao mbalimbali.
Fedha hizo zimetumika katika miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo sekta za nishati, miundombinu, elimu, maji, na afya.
Pia, Bw. Max alieleza kuwa Benki ya Stanbic imekuwa ikiwezesha biashara za wanawake nchini kwa kutoa mikopo kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati. Katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, benki hiyo imesaidia zaidi ya biashara 1,000 zinazomilikiwa na wanawake kwa mikopo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 10.
Maadhimisho haya ya Siku ya Wanawake Duniani Kanda ya Ziwa yamekuwa jukwaa muhimu la kujadili masuala ya uwezeshaji wa wanawake kiuchumi na fursa zinazopatikana kupitia taasisi mbalimbali za kifedha k**a Benki ya Stanbic.
Imeandikwa na Gharos Riwa