05/06/2026
HALMASHAURI ya wilaya ya Nyang’hwale mkoani Geita imeweka mpango maalum wa kushirikisha wadau wa maendeleo ili kumaliza uhaba wa madawati kwa shule za sekondari.
Mpango huo umeazimia kufikia mahitaji la madawati 3,000 kwa mwaka wa masomo 2026 katika shule za sekondari za serikali 20 ambazo zimepokea wanafunzi wa kidato cha kwanza 3,056.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Husna Toni amesema hayo katika taarifa yake kwa mkuu wa mkoa alipokagua na kupokea madawati 1,200 yaliyopatikana hadi kufikia Mei 2026.
Husna amesema madawati hayo ni mafanikio ya awamu ya kwanza ya mpango huo unaolenga kupata madawati 1,500 ambapo juhudi zinaendelea ili kufikia nusu ya mahitaji yaliyopo.
Amesema upungufu wa madawati umetokana mwitikio mkubwa wa wazazi kupeleka watoto shule baada ya sera ya elimu bila bure inayotekelezwa na serikali ya awamu ya sita.
“Ninaamini utoaji wa madawati haya utaboresha utoaji wa huduma ya elimu kwa wanafunzi wetu, na hatimaye kuongeza ufaulu shuleni”, amesema Husna.
Mkuu wa wilaya ya Nyang’hwale, Grace Kingalame amesema wadau wakubwa walioshirikishwa kuunga mkono mpango huu ni wawekezaji katika sekta ya madini na wameonyesha mwitikio.
Amesema mpango huo ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za serikali kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto na kuendana na kasi ya ujenzi wa madarasa inayotekelezwa na serikali.
Mkuu wa mkoa wa Geita, Martine Shigela amepongeza mpango huo huku akizitaka halmashauri zingine kuiga mfano wa Nyang’wale kuunga mkono juhudi za serikali katika sekta ya elimu.
“Huu ni ujumbe kwa wengine hususani kwa viongozi na watendaji kuhakikisha kwamba wanaiga mfano wa Nyang’hwale katika kuhakikisha kwamba wanafunzi wanapata madawati.
“Shule ambazo zitapokea Samani hizi, ni vyema wakapokea na kuthamini mchango huu, na kubwa zaidi kutunza na kuhakikisha pale panapotokea uharibifu, marekebisho yafanyike”, ameelekeza.
Habari Na .yohana.jr