Simulizi za biba nina

Simulizi za biba nina Contact information, map and directions, contact form, opening hours, services, ratings, photos, videos and announcements from Simulizi za biba nina, Publisher, Ilemera.

RIWAYA: NGOME YA GIZA.MTUNZI: AHMED R. JIRIWA.SIMU: 0769 805251            0774 122007SEHEMU YA 03JIKUMBUSHE ILIPOISHIA....
19/08/2022

RIWAYA: NGOME YA GIZA.
MTUNZI: AHMED R. JIRIWA.
SIMU: 0769 805251
0774 122007

SEHEMU YA 03

JIKUMBUSHE ILIPOISHIA.

Huweza kukuua huku unakunywa nao sharubati au unavuta nao sigara, huweza kukuua huku unafanya nao ngono lakini pia unaweza kujikuta unakufa kwa maumivu makali hasa pale wanapoagizwa kutokuua kirafiki. Watu wote hao huishi k**a wafungwa ndani ya gereza hilo na watu hao ni watano tu wanajiita 'Gwala killers.' Serikali inawajua na inajua kuwa wanatumiwa na watu fulani."

"Wameshindwa kuwadhibiti?"

SONGA NAYO....

Alihoji Roi baada ya kuvutiwa na hiyo simulizi. Bwana Mohamed Aziz alimtazama Roi kisha akamwambia.
"Umeshindwa kuvumilia kutulia hadi nimalize?"
"Kwani hizi ni ngano za paukwa pakawa? K**a si hivyo ninayo haki ya kuhoji na ninapohoji natarajia jibu si swali tena k**a ulivyofanya sasa." Aliongea Roi. Bwana Mohamed Aziz akanyanyua chupa ya pombe akaigida kwa funda kadhaa kisha akairejesha mezani. Aliimeza kwanza kabla hata hajaokota kipande cha nyama na kutafuna.

"Unadhani yupo wa kuwazuia Gwala killers, sheria wako nayo wao na nahisi hata bunge la nchi hii linapotunga sheria huwenda ipo sheria hawaiweki wazi yenye lengo la kuwalinda hawa jamaa. Hawazuiliki. Kuna maslahi baina ya watu fulani serikalini na huyu mmiliki wa hili kundi la Gwala killers. Ni mtu mkubwa na maarufu asiyejulikana..."
"Mtu mkubwa na maarufu asiyejulikana?" Alihoji Roi akiikata kauli ya bwana Aziz bila kujali tena.

"Ndiyo, umaarufu wake unaonekana kwa vijana wengi wa hapa mjini. Kuna vijana wanaishi maisha ya kifahari kwa ajili ya mtu huyo, kuna vijana wanaishi kwa kumtegemea mtu huyo pia. Kivipi... Wapo vijana wengi na wafanyabiashara wakubwa hata wasanii mbalimbali, waliobobea kwenye utumivu wa dawa za kulevya wanamuona huyu k**a Mungu wao ingawa hawajawahi kuijua hata sura yake. Unadhani atashindwa kuwa maarufu. Ni maarufu asiyejulikana. Jina lake halijulikani hadi sasa lakini bado yupo, tunaishi nae na anafanya mambo ya kuogopesha. Hata serikali inamtumia mtu huyu." Alijibu bwana Mohammed Azizi.

"Serikali inamtumia kivipi?" Roi alihoji.

"Wanapotaka kuua mtu fulani labda kwa sababu za kisiasa ama vyovyote kwa lengo la kumfunga mdomo, humtumia huyu mtu kuwaagiza vijana wake kutekeleza hilo suala na hujulikana kwa jina la watu wasiojulikana."
"Nimekuelewa vizuri sasa. Nini lengo lako la kutaka niijue simulizi hii?" Roi aliuliza baada ya kuwa ameelewa vizuri.

"Kuna roho mbili hazina hatia nataka ziwe huru Roi."
"Mbona unataka kuniingiza kwenye jambo nisilolitaka na wewe unalijua hilo. Nikifanya hivyo nitakuwa kinyume na endapo nitak**atwa na kutiwa nguvuni jua fika nitahukumiwa k**a haini, mtu afanyae ujasusi kwenye taifa jingine. Adhabu yake ni kifo Aziz, wewe unajua. Unataka nife. Siwezi." Alisema Roi huku akipiga funda la mwisho kwenye chupa ambayo haikuwa na kinywaji kingi. Aliirejesha chupa mezani ikiwa tupu.

"Watu hawa watakufa Roi k**a hawatapata msaada. Nimejaribu kuwatumia watu wengi kwa kuwaambia hili lakini wamejificha mbali kabisa hawataki hata kuniona. Wengine ni wapelelezi mahiri" Alisema Aziz.

"Wamefanya hivyo kwa kuwa wanajua hicho ni kifo. Sasa mimi nitakuwa mpumbavu nikajiue mwenyewe? Siwezi na naomba tuondoke hapa k**a wewe ba..." Alitaka kumalizia kuongea Roi lakini domo lake lilijaa gundi ghafla mara baada ya msichana mrembo aliyepita mbele yao. Alikuwa mrembo haswa kiasi alijikuta akinyanyuka na kutaka kumfuata. Mtoto wa k**e mrefu kwenda juu, mwenye rangi yake nyeupe mwenye nywele alizozisuka rasta tatu na kuziunganisha pamoja nyuma akitengeneza mkia mnene k**a wa mamba au kenge. Alitembea kwa mwendo wa kilimbwende huku akizitikisa nyama zake laini za nyuma k**a hataki. Roi alipiga hatua ya kwanza pili na tatu huku macho yake yakitazamana na yule msichana aliyemuangalia kwa kitambo kifupi kabla ya kutazama mbele. Alijua kuwa amemkosha huyo kijana kwani hata tabasamu lake lilikuwa likimchokonoa Roi kwa makusudi kabisa. Bwana Mohamed Aziz alibakia akimtazama Roi aliyekatisha mazungumzo kwa ajili ya mrembo yule.

"Bado kuna nguvu za ile mitambo iliyomfanya kuwa mashine ya ngono inaendelea kumtafuna huyu kijana, siyo kwa kupenda penda huku!" Alistaajabu bwana Aziz huku akiikumbuka historia ya Roi kule ilikotokea hadi kuwa jasusi maarufu na mahiri.
Roi hakufanikiwa kupiga hatua ya nne kwani alitokea kijana mmoja aliyekuwa akifanya malipo kaunta akamshika kiuno yule mrembo na kuondoka naye taratibu. Roi akabaki ameganda mithili ya mtu aliyeambiwa kuna mtu alikuwa akimchora kwa ajili ya kutengenezwa k**a sanamu la kumbukumbu hapo nchini Ungamo. Macho yakimtoka k**a mwanga wa kurunzi ya kichina. Yule mrembo kabla hajaufikia mlango aligeuka kisha akamfinyia jicho moja Roi akatoka. Bwana Mohamed Aziz alimshika mkono Roi na kumrejesha kitini. Hakujua k**a alisimama kwa lengo la kutaka kuondoka ama kwa lengo lipi, hilo hakulijua alijikuta tu akikaa tena kitini k**a mwehu tu. Tabia hii ya kupenda warembo wala haikumkatisha tamaa Mohamed Aziz kwani aliijua tabia ya mtu huyo na utendaji wake wa kazi ulivyo. Walitulia kwa kitambo kifupi kabla ya bwana Aziz kuyarejesha tena mazungumzo mezani.

"Kuna mzee mmoja anaitwa Mr. Wasika Jerome. Huyu ni mtu wa zamani ni mhandisi na msanifu mbobevu wa majengo ya kale aliyehusika kuchora ramani ya gereza la KIMKI pamoja na kulijenga akishirikiana na wajenzi wengine wabobevu wa nyakati zake. Yeye ndiye mwenye kila kitu kuhusiana na gereza lile. Sijui k**a unanielewa ninapozungumza hivi? Sikia, namaanisha kwamba huyu bwana analijua gereza la KIMKI k**a kahaba anavyozijua kona za vyumba kwenye nyumba za kulala wageni na mahoteli. Huyu mzee wamemk**ata yapata miaka mitano sasa yupo gerezani. Walimchukua kirafiki lengo lao likiwa ni kutaka kuwaonesha njia za siri za gereza lile ili iwe rahisi kwa hawa Gwala killers kutoka kwenda kufanya walichoagizwa kisha kurudi gerezani pasipo kugundulika k**a wanatokea ndani ya gereza hilo. Inaweza kukuchanganya hii. Ukajiuliza kwanini wawe na hofu wakati wamejivika mamlaka. Ingawa gereza la KIMKI halina ulinzi wa kuwazuia wasifanye wanachokitaka lakini wanataka kujilinda ili k**a litatokea jambo la kuwachunguza wasipatikane na hatia yoyote ile. Hivi ndivyo ilivyo. Aliwafanikishia lakini wamemzika huko huko ingawa anaishi vizuri na kula vizuri lakini gereza ni gereza Roi mtu huyu anahitaji uhuru. Hana kosa. Taaluma yake ndiyo inayomteketeza gerezani na serikali yake iliyoshindwa kujitengenezea ukuta mnene wa kushindwa kuingilika kipumbavu na kuchezewa na watu wachache k**a hawa wanaojiita wenye mamlaka. Yeye mwenyewe Wasika alidhani labda wangemwachia baada ya kumshinikiza sana na kuiathiri familia yake. Kumbe wao hawana nia hiyo mawazo yao huwatuma wakidhani huwenda siri zao zingejulikana au zitajulikana wakimwachia hivyo wameamua kumfanya mfugwa huru hadi pale hitimisho la maisha yake watakapoliamua wenyewe au Mungu." Alisema Aziz kwa maelezo marefu kabisa akiwa anamtazama Roi usoni ambaye hakuwa na muda hata wa kumsikiliza tena bwana huyo.

"Twende tuondoke hapa, siwezi kujiingiza huko mimi." Alisema Roi. Bwana Aziz akashusha pumzi nzito baada ya kuona kumbe yote aliyoongea ni bure kwa kijana huyo. Hata hivyo hakukata tamaa akasema.

"Kuna mpelelezi mahiri na mweledi. Yeye alikuwa akikipeleza kifo cha mfanyabiashara mkubwa ambaye alitekwa na kupotea zaidi ya wiki mbili kabla ya maiti yake kukutwa kwenye jaa kubwa la jiji hili ukiwa ndani ya kiroba cha salfeti, ndipo idara yake ikamtuma akipeleleze kifo hicho ili ajulikane aliyetenda unyama huo. Ni siku tatu tu zilitosha kumpoteza kijana huyo na asionekane machoni mwa watu. Sasa ni miaka mitatu kijana huyo hajaonekana. Hakuna mpelelezi aliyekubali kujiingiza kwenye kasumba hiyo. Hata idara yake ya usalama imekuwa kimya sana haizungumzii chochote kuhusiana na jambo hilo. Kijana huyo anajulikana kwa majina Frank Matiale."
"Nani?" Roi aliuliza akiwa na mshangao mkubwa. Ni k**a masikio yake hayakuwa yamesikia vizuri. Bwana Aziz akarejea kulitaja jina hilo na kumueleza kinaganaga kuwa alizipata taarifa za kupotea kijana huyo lakini pia alipata taarifa kuwa kijana huyo anateseka sana ndani ya gereza la KIMKI. Lengo kuu la mateso hayo ni kumfanya akubali kuisaliti serikali, aungane nao ili awe miongoni mwa wauaji wa Gwala killers. Inaaminika Frank hayupo tayari kujiunga na hilo kundi na yupo tayari kufa kuliko kuwa kinyume na kazi yake. Nao wanamfanyia kusudi hawamwachii na wanamwonesha kwamba wana nguvu kuliko hiyo serikali anayoiaminia. Ni aibu kusema maneno haya Roi mbele yako lakini hakuna njia. Hakuna watu wanaweza kujiingiza kwa makusudi gerezani na kusema tunamtaka kijana wetu au tunawataka watu wetu. Wanajitapa kwa kila hali. Anateseka sana Frank kiasi kwamba huwezi kumtazama mara mbili. Wanasema hivyo wakiwa kwenye majumba ya starehe. Inasemekana wamepanga kumtesa hadi kifo chake k**a ataendelea kusimamia msimamo wake. Hakuna jeshi, polisi wala nini wote kimya hadi hata mimi naogopa kuzungumza." Roi alijikuta mwili ukimsisimka, damu zilikuwa zikimchemka si haba baada ya kumkumbuka rafiki yake aliyemsaidia kwenye ile misheni ya kuikomboa Ungamo kwa watu madhalimu waliotaka kuiangamiza Ungamo na Tanzania. Alimkumbuka maana kwenye misheni hiyo Frank alijiita Frank kichaa na kweli alikuwa kichaa.

Kweli Roi alifika nchini hapo kwa ajili ya kuifaidi likizo yake aliyopewa na kitengo chake baada ya kuimaliza shughuli ngumu iliyotaka kuondoka na maisha yake huko nchini Uganda. Lakini si kwa Frank lazima ajiingize mzimamzima tena anajiingiza bila hata kitengo chake kujua. Hakujua k**a alikuwa akitaka kujipeleka mwenyewe kwenye shimo la mauti.
Hakujua.

Baada ya kuwa amejipa utayari wa kuingia kwenye hiyo kazi na ni kwa lengo moja tu la kumkomboa rafiki yake, alianza kumuuliza maswali bwana Aziz kuwa yeye habari zote hizo alikuwa akiambiwa na nani maana amekuwa akizijua siri nyingi za hao Gwala killers. Bwana Aziz akasema kuwa mbali na wao wenyewe G Killers kujitapa ovyo wakiwa kwenye majumba yao ya starehe, pia kuna askari jela mmoja ambaye anafanya kazi kwenye gereza hilo ndiye anayemfikishia hizo habari.

"Kabla sijaachana na masuala ya jeshi na kupewa kazi ya siri na mkuu wa nchi, nilijenga ukaribu mkubwa sana na askari jela huyo kwa kuwa nilifahamu anafanya kazi wapi na nilifanya hivyo ili kupata habari za gereza lile kabla hata huu uvundo haujaanza kunuka na kuchafua hali ya hewa ya taifa. Nilimfahamu kwa roho yake mbaya maana yeye na wenzake ndiwo tuliokuwa tukiwatumia kutesa watu wetu watukutu walioshindikana katika sehemu mbalimbali za shughuli zetu wakati huo gereza lile likitumika kisheria baada ya kupinduliwa sheria chafu zilizowahi kuwekwa na Rais wa awamu ya pili wa nchi hii aliyekuwa ametunga sheria za kujilinda yeye mwenyewe ili aishi miaka mingi madarakani. Hivyo akalitumia lile gereza kuwaangamiza wanasiasa wote waliokuwa wakimpinga. Watuhumiwa tunapowafikisha kwenye gereza hilo maarufu kwa kunyoosha watuhumiwa sugu basi huyo askari ndiye anayeongoza jopo la watesaji. Tulijenga ukaribu mkubwa sana hata nilipokuja kustaafu bado nilikuwa karibu na huyu ingawa nilijua kwa kipindi hiki anatumiwa vibaya na wale watu washenzi ila yeye hajui k**a mimi najua. Umri wake ni mkubwa lakini bado analitumikia lile gereza kwa kuwa ni mtesaji mmoja hatari sana aliyeishi akitesa kwa miaka mingi na hakuna siri inayofichwa k**a umesogezwa mbele ya mtu huyo." Ndivyo ambavyo alijibu Bwana Mohamed Aziz pindi alipoulizwa.

"Anaitwa nani huyo mtu na anaishi wapi hapa mjini?" Aliuliza Roi.

"Anaitwa Matole Gimba ila kwa jina lake maarufu la utani kutokana na matendo yake wanamuita Jeki simba. Anaishi huko mjini Sami ado kwenye mji uliojitenga unaotwa Majito, ndiko liliko jumba lake la kifahari. Liko juu ya mwamba mmoja mkubwa sana. Amepata pesa nyingi kwa kazi yake ya utesaji ukiachilia mbali mshahara wake anaoupokea kwa kila mwisho wa mwezi. Ukimtazama humdhanii k**a ni mtu mwenye roho mbaya ya kuogopwa. Ni rahisi kukukutanisha naye ni mtu wangu wa karibu sana." Alijibu bwana Aziz.

"Umesema anaishi kitajiri na anapata pesa nyingi kwa shughuli zake za utesaji?"
"Ndiyo,"
"Sitaki unikutanishe naye najua hawezi kuwa rafiki mwema kwangu huku akijua anakwenda kukitia dosari kibarua chake. Inatosha kwa kunielekeza anapokaa. Najua nitampata nikimtaka. Unakutana naye vipi hapa mjini?"
"Pamoja na utu uzima alionao lakini hajabahatika kuoa. Amebahatika tu kuzaa na kahaba hivyo ana mtoto mmoja wa kiume ambaye yupo nchini Afrika ya kusini. Anaishi huko. Anapenda sana anasa hasa mabinti wadogo waliyokosa maadili na kwenda kuiuza miili yao kwenye makasino na kumbi kubwa za starehe. Bwana Matole anapenda sana kumaliza haja zake za kimwili na watoto wazuri kwenye kasino moja kubwa la kimataifa liitwalo. Merinde Cassino lililopo katikati ya jiji hili la Sami ado, ukimkosa hapo utamkuta kwenye kasino la New Angel au kwenye Hoteli kubwa maafuru hapa nchini."
"Merinde Casino, naijua hata hizo nyingine hivyo naweza kukutana naye tukazungumza mawili matatu."
"Naam." Alijibu Bwana Aziz kisha akapiga tarumbeta chupa yake kisha akairejesha mezani tena.

"Huyo Mr. Wasika Jerome upotevu wake haukuwahi kuchunguzwa?" Aliuliza Roi huku akijifuta mikono yake kwa tishu alitoshelezwa tayari kwa kilaji na nyama choma. Hakutaka tena kuendelea kunywa kwani kinywaji kilikuwa hakipandi kabisa hasa alipoambiwa habari za rafiki yake Frank Matiale. Mtu anayetoa msaada mkubwa sana hasa anapojua ndani yake anafanya kazi na majasusi tokea Tanzania.

TUKUTANE TENA JUMA TATU KWA SEHEMU YA NNE.

RIWAYA: MUUAJI KATIKATI YA MJI.MTUNZI/MWANDISHI: AHMED R. JIRIWA.SIMU: 0769 805251SEHEMU YA 01Gari chache zilikuwa zikik...
17/08/2022

RIWAYA: MUUAJI KATIKATI YA MJI.
MTUNZI/MWANDISHI: AHMED R. JIRIWA.
SIMU: 0769 805251

SEHEMU YA 01

Gari chache zilikuwa zikikatiza juu ya barabara tulivu iliyopo pembezoni mwa bahari ya hindi. Zilikuwa ni gari za kuhesabika kiasi kwamba mtu yeyote ambaye angejishughulisha na hizo gari, asingeshindwa kujua idadi ya gari zilizopita kwa kila muda wa saa moja. Hakukuwa na watembea kwa miguu juu ya barabara hii kwa majira hayo ya saa sita za mchana, baiskeli zilikosekana kabisa licha ya kuwa jiji hili la Tanga ni miongoni mwa miji inayoongoza kwa wingi wa baiskeli. Pikpiki hazikupishana idadi na gari kwa upitaji wake. Hali hii iliifanya hiyo barabara kuwa pweke iliyopooza. Si k**a ilizongwa na vichaka kwa kila pande la hasha! Ni upande mmoja tu ndio kulikuwa na vichaka vya hapa na pale huku kwa umbali wa meta kumi toka barabara ilipo, kukiwa kunaonekana jumba moja kubwa lililozongwa na miti ya mikoko.

Wakati utulivu ukiendelea kuwapo juu ya barabara hii, mtikisiko wa miti midogomidogo ya mikoko karibia na barabara hasa upande lililoko lile jumba, ulionekana dhahiri. Kwa namna miti ile ilivyokuwa ikitikisika, ungeweza kudhani labda ni upepo mwanana upatikanao pembezoni mwa fukwe hizo za Chongoleani. Kadiri muda ulivyosonga ndivyo wazo la kuwa kitikisacho ni upepo kingefutika fikirani mwa mtu yeyote yule ambaye angejishughulisha na kiendeleacho eneo lile. Haukuwa upepo, alikuwa ni mtu tena pandikizi la mtu kwa lugha rahisi ungeweza kuliita jitu la miraba minne. Mtu huyu hakutoka kabisa barabarani alijituliza kimya pembezoni mwa barabara huku akitazama saa yake ya mkononi mara kwa mara. Hakukaa kwa muda mrefu hilo eneo kwa makadirio ni k**a dakika tano tu pekee ndizo ziliweza kumsimamisha hapo hadi pale alipoona gari aina ya Toyota Raum ya rangi nyekundu ikitokea upande wa kusini mwa barabara hiyo. Haraka pandikizi lile la baba lilijitoa pale kichakani na kusimama pembezoni mwa barabara kisha akalipungia mkono gari lile. Dereva wa ile gari ni k**a alitaka kumpita lakini hakufanya hivyo akapunguza mwendo na hatimaye kusimama mbele ya yule bwana. Yule bwana alitembea kwa hatua chache akafika usawa wa dirisha la dereva akainama wakati huo dereva akiwa anakishusha kioo taratibu. Dereva alimtazama bwana yule usoni hakuonekana kumfahamu.
“Habari yako bwana unaelekea wapi?” Aliuliza yule dereva. Alikuwa ni mtu wa makamo yule dereva aliyeonekana kuikimbiza miaka arobaini na tano hivi huku yule pandikizi la mtu akionekana kuwa ni mwenye miaka isiyozidi thelathini na sita. Yule bwana aliinama akamuuliza. “Unafika Tanga mjini?”
“Ndiyo, naelekea huko,”
“Samahani bwana msaada wako nina haraka sana,” aliomba yule mtu mkubwa.
“Ingia, ingia nikusogeze,” alisema yule bwana huku akimfungulia mlango yule mtu mkubwa. Yule mtu mkubwa aliingia akajiketisha kitini lakini kabla hata gari halijaondoka, kulitokea tukio la ghafula lililomtikisa matumbo yule mtu mkubwa. Ni wakati yule bwana akiwa anataka kuliruhusu lile gari kuweza kuondoka, sauti mbaya ya mpasuko wa kioo cha dirisha cha upande wa dereva ilisikika. Yule mtu mkubwa alishuhudia kichwa cha yule dereva kikivunjwa mithili ya n**i kavu wakati huohuo naye akikoswa na pigo hilo na kujikuta akichanwa vibaya kwenye paji lake la uso. Alishtuka mno! Hakuamini kile anachokiona.
“Ni nini hiki kinatokea?” Alihamanika.

Damu zilianza kumtoka kwa wingi kutokana na risasi iliyomkwagua kuchimba pakubwa. Haraka mtu yule mkubwa aliuk**ata mlango kwa nguvu na kutaka kuufungua ili atoweke lile eneo, alichelewa. Mdomo wa bastola kubwa ukamtazama tena ukiwa karibu kabisa na midomo yake. “Shiiit!” aling’aka yule mtu mkubwa. Hajakaa sawa alishuhudia mlango wa upande wa dereva ukifunguliwa kisha dereva yule kutolewa nje kibabe akiwa ni mfu tayari. Watu hawa wawili walionekana kuwa ni watu wanaoijua kazi yao vizuri na wenye kasi mno. Yule mtu mkubwa alipewa ishara ya kusogea kwenye kiti cha dereva kwa kuchezeshewa ile bastoala mara baada ya ule mwili wa dereva kutolewa nje.
“Sijui chochote jama…mimi si…sijui kit…” alilalama yule mtu mkubwa hata hivyo wavamizi wale wawili hawakujisumbua kumjibu zaidi walimtaka akikalie kile kiti cha dereva. Hakuwa na ujanja ilimbidi kufanya hivyo. Haraka yule mvamizi wa upande ule akatoa sold tape akaifunga mikono ya yule mtu mnene, mtu mnene kuona vile akajua k**a akizembea kuna jambo baya lingeweza kumkuta, njia rahisi kwake ikawa ni kujitetea. Hivyo alijikurupusha mikono ikamponyoka mfungaji. Alivurumisha ngumi moja nzito ambayo lengo kuu lilikuwa ni kumpata mvamizi yule usoni. Mtu yule aliyumba na ngumi ya mtu mnene ikapiga kwenye kona ya mlango na kumsababishia maumivu makali, alipigwa ngumi mbili za tumbo bonge la mtu zilizomsababishia kichefuchefu kiasi akatulia. Mikono yake ikak**atwa tena kibabe na kufungwa pamoja kwenye usukani wa gari. Alifungwa mdomoni halafu akapigwa pigo jingine zito shavuni na kuachwa akitweta.

Yule jamaa mwingine alipomwona mwenzake amemaliza, alilik**ata dumu la lita tano walilokuja nalo na kuanza kulimwagia mafuta ya petroli lile gari. Yule mtu mkubwa alikuwa akinung’unika bila juhudi yoyote ya kuweza kujitetea. Yule jamaa alipomaliza alilitupia lile dumu ndani ya gari kisha akawasha kiberiti cha gesi na kukitupia kwenye lile gari na kuondoka zao wakiliacha gari lile likiwa linateketea na yule mtu ndani yake. Bonge la mtu alikuwa anakufa anajiona.
Hatari hii.
___________

Gari ndogo nyeusi ilisimama nje ya jumba moja tulivu huko Mikanjuni, jumba kubwa kwelikweli na lenye thamani ya kutupa. Punde mlango wa upande wa dereva wa gari hiyo ulifunguliwa. Kiatu cha ngozi chenye soli ngumu kilichokozwa rangi kiliikanyaga ardhi ya mbele ya hilo jumba kabla hata ya mtu mwenye kukivaa kiatu hicho hajakitoa kiwiliwili chake garini. Aliteremka mtu huyo, alikuwa mrefu kiasi aliyevaa suti nyeusi zilizomkaa vizuri. Kabla hata hajaziruhusu hatua zake zimpeleke anakokukusudia, kijana mmoja alifika na kumsabahi, kijana huyo alivaa suruwali ya jeans rangi ya kibuluu, fulana nyeusi na raba nyepesi nyeupe.
“Wanakusubiri wewe tu,” yule kijana mlinzi wa getini alimwambia mtu yule mwenye kuvaa suti. Mtu yule mwenye kuvaa suti alimtazama yule kijana bila kusema neno kisha akayazungusha macho yake kuwatazma wengine watatu walioik**atia mitutu yao ya bunduki, alizirusha hatua zake na kuelekea ndani ya jengo hilo. Ndani mule yule bwana aliwakuta watu watatu ambao walionekana kuendelea na soga za hapa na pale. Walipomwona walinyamaza wakamtazama.
“Smart boy, ni wewe tu ndiye uliyekuwa umesalia hapa kikaoni,” alisema kijana mmoja aliyekuwa akilingana umbo na huyo aliyeingia muda huo.
“Peter, ilikuwa lazima niweke mambo sawa kabla sijaondoka kuja huku. Sikutaka wale jamaa warudi na kukuta hakuna mtu,” alisema mtu huyo aliyeingia muda huo huku akiwatazama watu wale usoni.
“Umefanya amuzi sahihi Paul, ni mrejesho gani wameuleta kwako sasa?” Mzee mmoja mwenye ndevu nyingi nyeupe aliuliza, alimtazama Paul usoni moja kwa moja. Paul alikuwa ni yule kijana ‘smart’ aliyeingia hivyo punde.
“Nadhani hiki ndicho kilichotukutanisha hapa,” alisema Paul.
“K**a ndicho, basi inabidi twende taratibu ili kuelezana kila kitu kwa marefu na mapana. Lazima tujue ni wapi tumekosea na wapi tumepatia ili kwenye makosa marekebisho ya haraka yaweze kufanyika,”
“Umenena. Haya twendeni kwenye kiini cha kikao hiki bila kupoteza wakati,” huyo alikuwa ni msichana mrembo aliyekuwa amekaa pembeni ya yule mzee mwenye ndevu nyingi nyeupe.

Paul alivuta chupa ya pombe akajimiminia kwenye gilasi kisha akavuta pumzi kuwatazama wenzake huku ile gilasi ya pombe ikiwa mkononi mwake. Idadi yao sasa ilifikia kuwa ni yenye watu wanne. Paul mwenyewe, yule mzee mwenye ndevu nyingi nyeupe afahamikaye kwa jina la mzee Mikidadi p.a.k Babu Miki, Peter na yule binti aitwaye Naomi.
“Kwanza tujipongeze kwa kuweza kufikia hapa tulipofika,” alisema mzee Mikidadi huku akiinyanyua juu gilasi yake ya kinywaji, kwa pamoja wakagonga gilasi zao na kila mmoja akapata funda moja la nguvu kabla ya kuzirejesha mezani.
“Kwa kweli lazima tujipongeze kwa hili,” aliendelea kuzungumza mzee Mikidadi.
“Ingawa bado safari ni ndefu hata hivyo hatua tuliyoipiga ni kubwa,” aliwatazama wenzake ili kuona k**a yupo wa kukataa kile alichokizungumza, aliuona utulivu.
“Kabla hatujakwenda kusikiliza matokeo ya kazi tuliyompa Paul,” alisema mzee Mikidadi.
“Ni vema tukakumbushana jambo moja la msingi sana,” mambwana wale wakatega masikio kwa umakini ili kuupata usikivu mzuri. Mzee Mikidadi akaendelea kuzungumza.
“Mabwana, hadi sasa tunazo asilimia sabiini na tano kibindoni mwetu. Wazi kabisa hii inatuonesha sisi ni washindi. Mbinu walizozifanya wajinga wale ili kutudhoofisha, ni mbinu za kitoto sana na bahati nzuri kwetu ikiwa ni mbaya kwao ni kwamba mbinu hizo tumeshazijua. Unajua sikutegemea k**a jeshi la polisi lingeweza kutumia mbinu za kitoto hivi? Jeshi la polisi? Aaah!”
“Babu Miki, unataka kuniambia jeshi la polisi nd’o limehusika kwenye vifo vya watu wetu?” Alidakia Peter akionekana kushangazwa na jambo hilo.
“Kwa asilimia mia moja, ni wao bwana, ni wao. Kamote hawezi kuwa na ujuzi wa kuua namna ile. Vijana wangu wanauawa na fundi Peter,” aliongea kwa mhemko mkubwa Babu Miki. Macho yake aliyazunguusha akiwatazama vijana wale k**a atakaye kuwashuku jambo. Kimya kizito kikatwaa nafasi, watu wale ni k**a wakawa hawana la kuongea kwa muda ule. Kila mmoja sasa akaruhusu mkono wake ufanye kazi ya kuokota gilasi mezani na kuipeleka kinywani, kinywa cha kila mmoja mahala pale kikaburudika na ladha ya kipekee ya ile pombe.
“Basi Kamote atakuwa anashirikiana na jeshi la polisi ili kutuangusha,” aliufukuza ule ukimya Naomi.
“Mh!” Babu Miki aliguna. Alimtazama Naomi kisha akaokota gilasi ya kinywaji ila kabla hata hajaipeleka kinywani, akasema.
“Kwenye hilo sina hakika, ninachokiamini…” aliiacha kauli yake ielee hewani, alikunywa kile kinywaji kisha ak**alizia.
“Kamote ameamua kuanika kila kitu chetu hapa mjini na yote ni kwa sababu ya lile pigo tulilompiga. Anaonekana kuwa na hasira na sisi sana,”
“Asije kutufelisha huyu mpuuzi?” Alionesha wasiwsi wake Peter.
“Yeye na aliowapa siri wamefeli na naapa kuanzia sasa, endapo ataendelea kuwa bado tu kila siku anatufuatilia, haki ya Mungu namuua kwa mikono yangu,”
“Mi nadhani tungemuua sasa hivi, ni hatari sana Kamote kwenye mikakati yetu,” alikazia Paul. Jambo hili lilionekana kumkera sana kijana huyo hata akaonekana akiongea kwa jazba. Babu Miki alimtazama akiwa mtulivu akamwambia.
“Kamote ni mtoto mdogo sana kwangu hivyo sioni sababu ya kulipaparikia hili. Nikitaka afe mbona ni muda mfupi sana,” walitazamana tena mithili ya wanaotegeana kuzungumza. Kimya hicho kilidumu kwa muda wa dakika moja nzima kabla ya Naomi kukifukuza kwa mara nyingine.
“Babu Miki, hii chelewa chelewa itakuja kututokea puani mi…”
“Naomi, najua unachokihisi. Sitaki kuziona hizo hisia zako mbele yangu, unahisi labda mimi siko imara kwenye maamuzi yangu? Mimi najua mengi binti na ndio maana niko kwenye hii nafasi, mimi si kiongozi mzembe,” aliweka tuo macho yake yakawa yamebadilika, hakutaka kucheka tena. Alihema kwa nguvu kisha akapiga funda kubwa la kinywaji akaiacha ile gilasi ikiwa tupu.
“Nisikilizeni,” alisema Babu Miki. Akawatazama wale vijana kwa haraka haraka halafu akaendelea.
“Yamipasa mfahamu kuwa mimi ni nani kwenu, ninapozungumza jambo huwa nina hakika nalo sifanyi mambo yangu kipumbavu. Mimi nina watu wengi wanaonifanyia kazi hivyo katu sitaki kuona mdudu yeyote kati yenu akijaribu kunipanda kichwani na kujiona yeye ni mjuaji kuliko mimi au anao uwezo wa kufikiri na kufanya maamuzi kuniliko,” akahema tena kwa nguvu akikifanya kifua chake kupanda na kushuka kwa kasi. Wale vijana watatu wakamtazama Naomi kwa macho ya kupepesa. Walijua mwenzao amemkanyaga nyoka mkiani.

Mzee Mikidadi huwa hahitaji kosa kubwa kuweza kuchukia, kosa dogo tu kwake linaweza kumtoa mtu roho hii iliwafanya vijana wake wote kuwa makini sana na vinywa vyao hata utendi wao wa kazi. Babu Miki ni mwepesi wa kufanya maamuzi ambayo kwa kawaida unaweza kudhani baadaye anaweza kujutia kwa alichokifanya lakini wala! Anapofanya huwa amefanya na hana kawaida ya kurudi nyuma anapoamua kufanya maamuzi yake. Ni miaka thelathini sasa anafanya kazi hiyo akiwa chini ya tajiri mmoja mkubwa wa kiarabu hapo jijini Tanga na tajiri huyo ndiye ambaye anamiliki hilo jumba la kifahari na la ajabu. Jumba ambalo ukikaa hapo sebuleni huwezi kujua mengi yanayofanyika ndani yake hadi ulipekue au mengine uoneshwe na wahusika. Sasa Miki analijua nje ndani jumba hilo kwa sababu ya mamlaka makubwa aliyopewa na kazi yake kubwa mzee huyo tangu hapo kabla na sasa ni kuliongoza genge kubwa la siri linalohusika na usambazaji wa dawa za kulevya mjini hapo. Alianza kazi hii akiwa ni mwenye umri wa miaka ipatayo ishirini na mitani na alianza k**a msambazaji wa kawaida. Juhudi yake ya kazi na roho mbaya aliyojaaliwa nayo ndiyo ikawa chachu kubwa kwa Miki kupanda cheo kwa kasi hadi kuwa hapo alipo. Maisha ya mzee huyu kwa ujumla wake yalitawaliwa na ukatili mkubwa. Wakati akiwa msambazaji wa kawaida wa dawa za kulevya, alihakikisha hakuna makosa madogo madogo yanayofanyika, aliamini kosa lolote liwe dogo au kubwa linaweza kumharibia mtu kazi yake. Kwa mikono yake alishuhudiwa na kiongozi wake wa muda wote aliyemwajiri akifanya mauaji magumu kuyatazama sababu ikiwa ni kosa dogo tu lililofanywa naye eidha la kupoteza hesabu au kuwaonesha njia polisi hata wakazigundua maskani zao ndogondogo za mafichoni.

Tabia hii ilimvutia sana Guliam hata akamvusha na kumpa nafasi za juu za uongozi hata akawa chini yake hivi sasa. Hata alipotunukiwa hiyo nafasi na bosi wake bado aliendelea kuwa moto wa kuotea mbali kiasi kundi lao la uzaaji na usambazaji wa dawa za kulevya kukua kwa kasi kubwa hadi nje ya mipaka ya jiji la Tanga. Biashara yao ikatanua wigo na kuwa biashara kubwa iliyoajiri vijana wengi jijini hapo. Kadiri siku zilivyokwenda, kundi hili likawa si tu kuuza na kusambaza dawa za kulevya nchini bali lilijihusisha na ukodishaji wa silaha kwa ajili ya kufanyia matukio ya kihalifu. Katika hali ya kushangaza ni kwamba ilikuwa ni vigumu sana kuweza kulidhibiti kundi hilo liitwalo Young Seekers (YS) kabla hawajafikiria kulibadili jina k**a walivyofanya. lililokuwa limebeba maana ya vijana watafutaji au vijana wachakalikaji. Kwa nini iwe ni vigumu kuweza kulidhibiti kundi hilo? Lilikuwa ni kundi linaloongozwa na watu wenye kujua wanafanya nini, weledi na makini katika utendaji wao. Walikuwa na njia nyingi za ufikishaji bidhaa zao kwa wateja wao. Kutokana na utajiri mkubwa wa Guliam, kwa namna moja ama nyingine iliweza kulifanya kundi hili kuwa ni lenye utendaji wa siri sana hapo mjini na miji ya jirani. Licha ya Guliam kumiliki vituo vingi vya mafuta nchini, maduka ya kisasa ya vyakula, pamoja na gereji kubwa hapo jijini. Hata hivyo alikuwa na watu wengi aliowaajiri k**a haramu. Vijana hawa walikuwa wanazunguuka kwenye kila kona ya mtaa wakiwa na bidhaa mbalimbali k**a geresha tu huku wakiwa kwenye misheni zao nyingine; Hawa jamaa walikuwa ni hatari kwelikweli na shughuli zao zilikuwa zikipenya sehemu zote hata zile ambazo kwa mtazamo wa kawaida ungedhani isingewezekana. Pia walikuwa wakishirikiana na baadhi ya maafisa wa jeshi la polisi wasio waaminifu. Hizi zilikuwa ni baadhi tu ya mbinu ambazo kundi hili ilizitumia kwa kiasi kikubwa lakini walikuwa na mbinu nyingine hatari zaidi na zenye usiri mkubwa ambazo hata polisi waliokuwa wakishirikiana nao hawakuwa wakizifahamu.

Hivyo historia hii ya ukatili wa Babu Miki, ilitosha kuwafanya vijana wake wote wahofie mara tu wanapomwona amekasirika.
Walimwogopa mno kuliko hata bosi wao mkuu ambaye hawajawahi kumwona.
“Paul tuambie nini kilichojiri huko ulikokuwa umewatuma vijana wako,” alisema Babu Miki akiwa ameukata ukimya ule mkubwa. Vijana wale wakayahamisha macho yao sasa na masikio kusikia kile ambacho Paul angesema. Paul alijikohoza akaliweka koo lake sawa kisha akamtazama kiongozi wake sasa akiwa ni mwenye mashaka kuliko alivyokuwa hapo awali.
“Vijana wameitenda kazi Babu Miki, wameitenda kazi hiyo kikamilifu kabisa,”
“Wamefanikiwa kumuua Erasto?” Alidakia kwa swali Babu Miki.
“Yaa,”
“Hebu nieleze mazingira ya kifo cha huyo mshenzi,”
“Vijana waliniambia kwamba walipofika kwenye lile jumba lao la mafichoni huko Chongoleani, walimwona akiwa anatoka. Inamaana k**a wangechelewa kwa dakika mbili mbele wangekuwa wamemkosa. Walimwona akisimamisha gari kisha kuingia ila kabla hata dereva wa gari ile hajaliondoa, walifanikiwa kumpiga risasi nzito iliyomuua palepale kisha kuizingira ile gari kabla Erasto hajajitetea. Haikuwa kazi ngumu kuweza kumdhibiti kwani lilikuwa ni tukio la ghafula sana kwake lililomnyima nafasi ya kujiandaa. Walimshughulikia papo hapo kwa vipigo kisha wakamfunga mule garini wakaichoma moto ile gari yeye akiwamo ndani yake,”
“Safi kabisa,” Naomi alisema kwa sauti kubwa. Wale vijana wengine wakaonekana kufurahishwa na taarifa hiyo ispokuwa Babu Miki, yeye alikaa kimya akiichuja ile taarifa hadi alipoona imechujika ndipo alimtazama Paul na kumuuliza.
“Waliishuhudia gari ikiteketea kabisa?” Paul alifikiri kwa muda kisha akatikisa kichwa huku akijibu.
“Hapana, hapana, walisema walipoiona gari inawaka wao wakaondoka,”
“Unaona sasa,” alisema huku akiwa anamtazama Paul.
“Ndivyo nilivyoagiza kazi iende kwa namna hiyo? Halafu na ninyi mnaufurahia upumbavu alioufanya mwenzenu. Mimi nilitaka Erasto afe kabisa, yaani afe wakiwa au ukiwa umeshuhudia kwa macho yako aaah!” Alighadhibika mno Babu Miki. Na ili kuzidhihirisha hasira zake, aliik**ata bastola yake na kuisogeza risasi chemba.

NINI KITAJIRI?

TUKUTANE HAPA SIKU YA JUMA TANO KWA SEHEMU YA PILI.

Address

Ilemera

Website

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Simulizi za biba nina posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Share

Category