19/08/2026
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, ametoa agizo kali kwa madereva wa mabasi kuwa lazima wapakie na kushusha abiria katika kituo cha mabasi cha Magufuli pekee, akisema atakayekaidi atakamatwa na kufikishwa mahakamani. Ameeleza kuwa alishatoa muda wa wiki moja kwa utekelezaji na sasa muda huo umekwisha.
Alitoa msisitizo huu katika mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na wafanyabiashara wadogo wadogo, wakiwemo mama lishe, machinga, madereva wa bodaboda na bajaji, pamoja na mawakala wa mabasi ya safari za mikoani na nchi jirani.
Wabunge na viongozi wengine wa eneo hilo wameunga mkono agizo hilo. Anjela Kairuki, Mbunge wa Kibamba na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, amesema hatua hiyo inaenzi uwekezaji wa serikali na inatoa fursa kwa wafanyabiashara wadogo. Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Wakili Albert Msando, amesisitiza kuendelea kusimamia utekelezaji wake, huku Meya wa Manispaa ya Ubungo, Laurance Mlaki, akithibitisha kuwa halmashauri na baraza la madiwani wanaunga mkono mpango huo, akisema eneo hilo lina nafasi ya kutosha kwa ofisi na maegesho.