Kusini Yetu Online Tv

Kusini Yetu Online Tv Ukarasa maalum wa habari utakaokuweza kupata taarifa zote zinazotokea ndani na nje ya Tanzania.

14/12/2025

Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, amezindua rasmi miongozo ya uzalishaji endelevu wa mazao ya ufuta, mbaazi, maharage, dengu, choroko na soya, tukio lililowakutanisha zaidi ya wataalamu wa kilimo na ushirika 600 kutoka Mkoa wa Lindi.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Waziri Chongolo amesema hatua hiyo ni muhimu katika kuchochea uzalishaji wenye tija na kuwawezesha wakulima kufanya kilimo cha kisasa chenye manufaa ya kiuchumi.


11/12/2025

Katika kuhamasisha kampeni ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia, Shirika la TALIA Makazi kutoka Mtwara Mjini leo limetoa mafunzo kwa wananchi wa Kijiji cha Milidu, Kata ya Namikupa, Wilaya ya Tandahimba. Mafunzo hayo yalilenga kuwaelimisha wananchi kuhusu namna ya kutambua na kukabiliana na ukatili wa kijinsia kwa wanawake, wasichana na vijana.

Noel Kadaga, msimamizi wa miradi kutoka shirika hilo, amesema wako katika mwendelezo wa kampeni ya mwaka 2026 yenye kauli mbiu: “Ungana Kukomesha Unyanyasaji wa Kidigitali dhidi ya Wanawake na Wasichana.” Amesema lengo ni kukutana na jamii na kujadiliana njia bora za kutokomeza ukatili wa kijinsia, hasa katika maeneo ya vijijini.

Walengwa wa mafunzo ni akina mama, baba na vijana ambao wamepewa uelewa kuhusu aina mbalimbali za ukatili na namna ya kutoa taarifa pindi matukio yanapotokea.

Wananchi waliopata mafunzo hayo wamelishukuru shirika la TALIA kwa hatua hiyo, wakisema yamewasaidia kutambua dalili za ukatili na jinsi ya kuchukua hatua ndani ya jamii.

Afisa mtendaji wa Kata ya Namikupa pia amepongeza shirika hilo kwa kutoa mafunzo, akisema yamekuwa msaada mkubwa katika kuwafikia wananchi na kuwaelimisha juu ya kupambana na ukatili wa kijinsia.

MBUNGE WA NDANDA, MHE. FARAJI BURIANI NANDALA AWASHIKA MKONO WANANCHI WALIOKUMBWA NA MAAFAMbunge wa Jimbo la Ndanda, Mhe...
10/12/2025

MBUNGE WA NDANDA, MHE. FARAJI BURIANI NANDALA AWASHIKA MKONO WANANCHI WALIOKUMBWA NA MAAFA

Mbunge wa Jimbo la Ndanda, Mhe. Faraji Buriani Nandala, ameungana na wananchi wa kata za Ndanda, Mwena na Chikundi – hususan kijiji cha Mkalapa – kufuatia maafa yaliyosababishwa na mvua kubwa iliyoambatana na upepo mkali na kuleta uharibifu mkubwa.

Maafa hayo yametokea Desemba 06, 2025 mchana, ambapo zaidi ya nyumba 200 zimebomolewa, na familia nyingi kupoteza makazi, chakula na mahitaji muhimu ya kibinadamu.

Katika hatua za kushika mkono waathirika, Mhe. Nandala ametembelea maeneo hayo na kutoa tani 3 za unga, viroba 7 vya sukari, pamoja na sabuni za unga na sabuni za mche kwa ajili ya kusaidia familia zilizoathirika.

Aidha, Kamati ya Maafa ya Wilaya inaendelea na tathmini ya kina katika maeneo yote yaliyoathiriwa ili kufahamu ukubwa wa athari na mahitaji ya ziada yanayohitajika.

Mhe. Nandala ametoa pole kwa wananchi wote walioathirika na ameahidi kuendelea kushirikiana na Serikali na wadau wengine ili kuhakikisha waathirika wanapatiwa mahitaji ya msingi kwa wakati.

30/11/2025

Mradi wa Ulaghibishi unaotekelezwa na TWAWEZA EAST AFRICA kwa ushirikiano na LANGO umeendelea kuleta mabadiliko chanya kwa wananchi wa Halmashauri ya Mtama, mkoani Lindi, kwa kuwajengea uwezo wa kubaini changamoto na kuibua miradi ya maendeleo kupitia vipaumbele vyao.

Akizungumza katika kikao kazi cha walaghbishi kutoka vijiji 10 vinavyotekeleza mradi huo, mwakilishi wa Twaweza, Richard Temu, amesema mradi umewawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika kupanga na kutekeleza miradi, hatua iliyoleta matokeo ya kudumu katika jamii.

Kwa upande wake, mwakilishi wa LANGO, Bi. Aina Pero, amesema mradi huo ulioanza mwaka 2022 unatekelezwa katika vijiji vya Nahukahuka, Chiuta, Mmumbu, Sudi, Mandawa, Mtua Longa, Mtakuja, Mwangu, Rondo na Namangale.

Wananchi wamesema mradi umeongeza uelewa wao juu ya umuhimu wa kutengeneza miradi ya maendeleo bila kusubiri serikali. Wameeleza kuwa miradi waliyoiibua imepata msaada wa serikali katika hatua za mwisho za utekelezaji, hali iliyoongeza hamasa ya ushiriki wao kwenye shughuli za kijamii.

24/11/2025

Wazazi mkoani Lindi wametakiwa kuwapeleka watoto wao waliokosa kuchaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza, kidato cha sita au vyuo vingine, ili kupata mafunzo ya ufundi katika fani mbalimbali.

Wito huu umetolewa na Afisa Elimu Sekondari wa Manispaa ya Lindi, Mwalimu Rehema Nahale, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Manispaa, wakati wa mahafali ya 39 ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Chilala, kilichopo Kata ya Rutamba.

Mwalimu Nahale alisema kuwa badala ya watoto kukaa mitaani na kulaumu serikali kwa ukosefu wa ajira, kushiriki mafunzo katika chuo hicho kutawasaidia kujiajiri na kujikwamua kiuchumi.

Mhandisi Mohamed Chuo, Mkuu wa chuo hicho, aliongeza kuwa mafunzo waliyopewa vijana hayo yanawapa fursa ya kujiajiri au kupata ajira katika fani zao.

Wanafunzi waliohitimu mafunzo hayo walieleza matarajio yao na kuwasihi wazazi kuwapeleka watoto wao vyuoni ili kujiandaa kwa maisha ya baadaye yenye mafanikio.


Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara linafanya uchunguzi kuhusu mauaji ya Sumaya Hassan Mataka (12), mwanafunzi wa darasa la t...
23/11/2025

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara linafanya uchunguzi kuhusu mauaji ya Sumaya Hassan Mataka (12), mwanafunzi wa darasa la tano Shule ya Msingi Ufukoni, aliyepatikana amefariki katika ufukwe wa bahari ya Hindi eneo la Mangoela.

Sumaya alitoweka tarehe 21 Novemba 2025 baada ya kuondoka nyumbani asubuhi akiwa na watoto wenzake. Mwili wake uligundulika siku iliyofuata ukiwa na majeraha na mchanga mdomoni na puani.

Uchunguzi wa awali unaonyesha alikosa hewa baada ya kuwekwa mchanga usoni na pia alifanyiwa vitendo vya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia.

Mwili wa marehemu umekabidhiwa kwa familia kwa taratibu za mazishi.

Polisi wamewaomba wananchi kutoa taarifa zozote zitakazosaidia kuwabaini waliohusika na mauaji hayo.

Diwani mteule wa Kata ya Mtanda kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Mheshimiwa Idd Lulida, ametia nia ya kugombea nafasi ...
20/11/2025

Diwani mteule wa Kata ya Mtanda kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Mheshimiwa Idd Lulida, ametia nia ya kugombea nafasi ya Umeya wa Manispaa ya Lindi baada ya kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya chama hicho.

Lulida alichukua fomu hiyo leo, Novemba 20, 2025, katika Ofisi za CCM Mkoa zilizopo Wailes, Manispaa ya Lindi, ambapo alikabidhiwa na Katibu wa CCM Wilaya ya Lindi, Bw. Mohammed Lawa.

Akizungumza mara baada ya kuchukua fomu, Mhe. Lulida alisema dhamira yake ni kuboresha huduma muhimu za jamii ikiwemo elimu, barabara na afya, pamoja na kuandaa mazingira rafiki kwa uwekezaji.

Ameeleza kuwa mipango hiyo inaenda sambamba na maandalizi ya kupokea miradi mikubwa ya kimkakati k**a ilivyoainishwa kwenye Ilani ya CCM ya 2025–2030, akisisitiza kuwa yupo tayari kushirikiana na wananchi kuleta maendeleo katika Manispaa ya Lindi.

19/11/2025

Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) imekabidhi jumla ya tani 12 za mbegu bora za ufuta, choroko na mbaazi kwa wakulima wa Mkoa wa Mtwara, katika hafla iliyofanyika Novemba 18 katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mtwara.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanal Patrick Sawala ameipongeza Wizara ya Kilimo kupitia COPRA kwa hatua ya kuhakikisha wakulima wanapata mbegu bora bila gharama, akibainisha kuwa mkoa umekabidhiwa tani 6 za ufuta, tani 3 za choroko na tani 3 za mbaazi.

Amesema hatua ya kugawa mbegu bure itapunguza gharama za uzalishaji na kuongeza tija kwa wakulima wanaojihusisha na mazao mchanganyiko katika mkoa huo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa COPRA, Bi. Irene Mlola, amesema mamlaka hiyo imeamua kusogea karibu zaidi na mkulima kwa kuhakikisha anapata mbegu bora kuanzia shambani, sambamba na kutoa mafunzo kwa maafisa ugani watakaosimamia uzalishaji wa mazao hayo.

"Tumeona siyo tu tukutane na mkulima sokoni, bali tusimame naye bega kwa bega shambani ili kuhakikisha ubora unaanzia kwenye uzalishaji,” amesema Bi. Mlola.

Wakulima pamoja na maafisa ugani waliohudhuria hafla hiyo wameishukuru COPRA kwa hatua hiyo, wakisema itawasaidia kuongeza uzalishaji na kuboresha kipato chao.

18/11/2025

Wakulima wa Ufuta mkoani Lindi wameipongeza Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) kwa kukabidhi tani saba za Mbegu Bora za Ufuta kwa Uongozi wa Mkoa huo ili zigawiwe bure kwa wakulima hao.

Wakulima hao wamesema hatua ya utoaji wa mbegu hizo utawapa hamasa zaidi kuendelea kulima ufuta kwa tija na hatimaye kupata matokeo chanya kwenye msimu huu.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Victoria Mwanziva, amesema mbegu hizo zitaenda katika halmashauri zote sita za mkoa huo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha uzalishaji wa ufuta. Aidha, amewataka maafisa ugani kusimamia kikamilifu sekta ya kilimo ili kuongeza tija na ubora wa mazao.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa COPRA , Bi Irene Mlola, amesema mamlaka hiyo ina jukumu la kusimamia mazao ya nafaka na mazao mchanganyiko, yakiiwemo ufuta, mbaazi na choroko.

Ameongeza kuwa lengo la serikali ni kuunga mkono juhudi za wakulima wa ufuta mikoa waliouza mazao yao kupitia mifumo rasmi ya biashara ya zao hilo.

Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) leo Novemba 18 imekabidhi tani 7 za mbegu bora za ufuta—sawa na kilo 7,000—kwa wakulima wa Mkoa wa Lindi, katika hafla iliyofanyika kwenye viwanja vya maonesho ya Nane Nane, Ngongo mjini Lindi.
mwanziva

16/11/2025

Shirika la Mafuta na Gesi Tanzania (TPDC) limefanya Bonanza la Michezo katika Kata ya Nanguruwe, Wilaya ya Mtwara, likiwa na lengo la kuimarisha ushirikiano na jamii inayozunguka miradi ya gesi.

Bonanza hilo limefanyika Novemba 15, 2025 katika viwanja vya Shule ya Msingi Nanguruwe, likijumuisha michezo wa mpira wa miguu.

Mgeni rasmi, Mkuu wa Wilaya Abdallah Mwaipaya, amepongeza TPDC kwa kuandaa tukio hilo na kusema kuwa michezo ni njia muhimu ya kujenga umoja na kuimarisha mahusiano na wananchi. Ameitaka jamii ya Nanguruwe kuendelea kushirikiana na TPDC katika utekelezaji wa miradi ya gesi.

Kwa upande wake, Afisa wa TPDC, Ali Mluge, amesema Nanguruwe ni eneo muhimu katika uzalishaji wa gesi nchini, ambapo kiasi cha futi za ujazo trilioni 1.6 kimegunduliwa, na kukifanya kuwa miongoni mwa maeneo yenye mchango mkubwa k**a Msimbati na Songosongo.

Wananchi wameishukuru TPDC kwa bonanza hilo na kueleza kuwa miradi ya gesi inaleta matumaini ya ajira, biashara na maendeleo ya kijamii.

14/11/2025

Tukio la Korosho Marathon msimu wa nne, linalotarajiwa kufanyika Novemba 29, 2025 mkoani Mtwara, limeelezwa kuwa litafungua fursa nyingi za kiuchumi kwa wajasiriamali kutoka ndani na nje ya mkoa huo.

Akizungumza na vyombo vya habari leo tarehe 14 Novemba 2025, Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Abdallah Mwaipaya, amesema maandalizi yanaendelea vizuri na kwamba tukio hilo litatoa nafasi kubwa kwa wafanyabiashara kuonyesha na kuuza bidhaa zao, hasa zinazotokana na zao la korosho.

DC Mwaipaya amesema kuwa zaidi ya watu 3,000 wanatarajiwa kuwasili Mtwara kushiriki na kufuatilia Korosho Marathon 2025, jambo litakaloongeza mzunguko wa fedha na kuchochea uchumi wa wananchi.

“Hili ni tukio kubwa, si la kimkoa tu bali kitaifa na kimataifa. Ujio wa Korosho Marathon utaleta fursa kubwa kwa wajasiriamali na wananchi kupitia huduma mbalimbali watakazotoa kwa washiriki,” amesema.

Aidha, ametoa wito kwa wananchi na wadau wa maendeleo kujitokeza kwa wingi, akieleza kuwa tarehe 29 Novemba sekta ya michezo nchini itakuwa Mtwara, ambapo wanariadha kutoka ndani na nje ya mkoa watafanya mashindano hayo makubwa.

Amesisitiza kuwa Korosho Marathon 2025 si tukio la michezo pekee bali ni jukwaa la kukuza biashara, ubunifu na kutangaza bidhaa za Mtwara kimataifa.

Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) imeendesha mafunzo kwa makundi mbalimbali mkoani Mtwara, ikiwemo walemavu,...
12/11/2025

Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) imeendesha mafunzo kwa makundi mbalimbali mkoani Mtwara, ikiwemo walemavu, wanawake na wajasiriamali, kuwajengea uwezo wa kuchangamkia fursa za tenda zinazotangazwa na serikali kupitia idara za ununuzi.

Akifungua mafunzo hayo katika Manispaa ya Mtwara-Mikindani, Katibu Tawala wa Mkoa huo, Bahati Geuzye, amesema mafunzo hayo ni muhimu kwani yanawawezesha wadau hao kuelewa vyema sheria, kanuni na taratibu za ununuzi wa umma.

Geuzye amesema zaidi ya asilimia 70 ya bajeti ya serikali hutumika kwenye ununuzi wa umma, hivyo ni muhimu kwa wananchi wote wenye sifa kushiriki na kunufaika na miradi ya maendeleo kupitia mifumo rasmi ya serikali.

“Tunaishukuru PPRA kwa fursa hii, kwani mafunzo haya yataleta uelewa na kutoa nafasi sawa kwa makundi yote kushiriki katika tenda za serikali,” alisema Geuzye.

Kwa upande wake, mwakilishi wa PPRA, Magnus Steven, ameeleza mafunzo hayo yalianza Novemba 10, 2025 katika Manispaa ya Mtwara-Mikindani na yataendelea katika halmashauri zote tisa za mkoa huo.

Amesema yanalenga kutoa elimu juu ya sheria na kanuni za ununuzi wa umma pamoja na namna ya kutumia mfumo wa kielektroniki wa manunuzi (NeST) ili kurahisisha ushiriki wa wananchi.

Baadhi ya washiriki, akiwemo Fatuma Mpondomoka, wameishukuru serikali kwa kuwajengea uwezo huo, wakisema elimu hiyo itawawezesha kushiriki ipasavyo katika zabuni za serikali.

Mwingine, Mustafa Yasini, amesema kupitia mfumo wa NeST sasa wataweza kufuatilia na kushiriki kikamilifu katika fursa mbalimbali za ununuzi wa umma.

Address

1050, Mtwara
Mikindani

Telephone

+255682907172

Website

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Kusini Yetu Online Tv posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Business

Send a message to Kusini Yetu Online Tv:

Share