Kusini Yetu Online Tv

Kusini Yetu Online Tv Ukarasa maalum wa habari utakaokuweza kupata taarifa zote zinazotokea ndani na nje ya Tanzania.

28/10/2025

Mgombea Ubunge wa Jimbo la Nachingwea kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Fadhiri Liwaka, amefunga kampeni zake kwa kishindo leo Oktoba 28, 2025 katika viwanja vya Maulidi, saa chache kabla ya Uchaguzi Mkuu wa kesho.

Akihutubia maelfu ya wananchi, Liwaka ameahidi kushirikiana na wenyeji wa jimbo hilo katika kuharakisha maendeleo, ikiwemo ujenzi wa barabara ya Nachingwea–Masasi kwa kiwango cha lami, kuboresha huduma za maji, afya, elimu na miundombinu ya barabara.

Liwaka ndiye mgombea pekee wa ubunge katika Jimbo la Nachingwea, na ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kupiga kura ili kuhakikisha utekelezaji wa ahadi hizo unafanyika kwa vitendo.

Wapiga kura zaidi 1,000 wanatarajiwa kupiga kura kesho katika jimbo la Mtama Mkoani Lindi.Akizungumza wakati wa kufunga ...
28/10/2025

Wapiga kura zaidi 1,000 wanatarajiwa kupiga kura kesho katika jimbo la Mtama Mkoani Lindi.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo kwa wasimamizi wa vituo na wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi wapatao 632 wa jimbo la Mtama, Msimamizi wa uchaguzi wa jimbo hilo Bwn. Boniface Fungo amewataka wasimamizi hao kwenda kuviishi viapo vyao vya kutunza siri.

"Mmeajiriwa na Tume huru ya Taifa ya uchaguzi mwende mkatunze siri na kufuata katiba na miongozo iliyowekwa na Tume."amesema Fungo.

27/10/2025

Mtwara imezindua mtambo mpya wa kufua umeme wenye uwezo wa megawati 20, unaolenga kuongeza upatikanaji wa nishati na kumaliza tatizo la kukatika kwa umeme katika mikoa ya Lindi na Mtwara.

Uzinduzi umefanyika leo, Oktoba 27, 2025, na Kanali Patrick Sawala, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara.

Kanali Sawala amesema uzalishaji wa umeme sasa umefikia megawati 70, huku mahitaji ya mikoa hiyo yakiwa megawati 38.5, hali inayowapa Lindi na Mtwara ziada ya umeme.

“Ukosefu wa umeme unakuwa historia. Tunamshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuongeza uzalishaji na kutuunganisha na gridi ya taifa,” amesema.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Antony Mbushi, ameeleza kuwa mtambo mpya utapunguza changamoto wakati mitambo mingine inapofanyiwa matengenezo.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Lindi pia amepongeza juhudi za serikali na TANESCO katika kuboresha huduma za umeme na kutatua changamoto za muda mrefu kwa wananchi.

27/10/2025

Mgombea Ubunge wa CCM Jimbo la Mchinga, Mama Salma Kikwete, amehitimisha kampeni zake leo katika mkutano uliofanyika Kata ya Nangaru, Manispaa ya Lindi, akiwataka wananchi kujitokeza kwa wingi Oktoba 29, kupiga kura kwa CCM akisisitiza kuwa chama hicho kina Ilani inayotekelezeka.

Amesema endapo atachaguliwa, atashirikiana na wananchi kuharakisha maendeleo, ikiwemo ujenzi wa Kituo cha Afya katika Tarafa ya Nangaru.

Mgombea Udiwani wa kata hiyo, Salum Ng’ondo, ametoa wito kwa wapiga kura kujitokeza mapema siku ya uchaguzi.

Kampeni hizo zimepata mwitikio mkubwa katika maeneo mbalimbali ya Mchinga.

27/10/2025

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Patrick Sawala, amewatoa hofu wananchi na kuwataka wajitokeze kwa wingi kushiriki uchaguzi mkuu utakaofanyika Jumatano, Oktoba 29, 2025.

Amesema hali ya usalama mkoani humo ni shwari, na vyombo vya ulinzi na usalama vimejipanga kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa amani na utulivu.

“Jitokezeni kwa wingi kutumia haki yenu ya kikatiba. Mkoa wetu uko salama na tumejipanga vizuri kuhakikisha utaratibu wote wa uchaguzi unaenda vizuri,” amesema Kanali Sawala.

Aidha, amewataka wananchi kufuata taratibu za uchaguzi, ikiwemo kutofanya kampeni siku ya kupiga kura na kuondoka vituoni mara baada ya kupiga kura, pamoja na kuepuka lugha za matusi au vitisho kwa watendaji wa uchaguzi.

27/10/2025

Mratibu wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Richard Kasesela, ameendesha elimu kwa watu wenye ulemavu wa macho ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Kasesela alisema hatua hiyo inalenga kuhakikisha kundi hilo haliachwi nyuma katika kutumia haki yao ya kikatiba ya kupiga kura.

Amesema elimu hiyo imejikita katika kuwafahamisha namna ya kutambua karatasi ya kura, taratibu za kupiga kura na umuhimu wa kura yao katika kuchagua viongozi wanaowataka.

Kasesela ameitaka jamii kuendelea kuwasaidia watu wenye ulemavu na kuhakikisha wanapata huduma zinazostahili ili waweze kushiriki kikamilifu katika masuala ya kijamii na kidemokrasia.

26/10/2025

Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Zainab Telack, amekabidhi vifaa vya kisasa kwa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ili kuongeza ufanisi katika kukabiliana na majanga mkoani humo.

Hafla hiyo imefanyika viwanja vya Ilulu, ikihusisha pia zoezi la utayari wa vyombo vya Ulinzi na Usalama.

Vifaa hivyo ni pamoja na gari la wagonjwa la kisasa, Command Car, gari dogo la ukaguzi, na mtambo wenye uwezo wa kubeba lita 5,000 za maji na povu la kemikali lita 400.

Telack amesema serikali inaendelea kuimarisha uwezo wa vyombo vya ulinzi na usalama ili viendelee kutoa huduma bora kwa wananchi, hasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.

Mrakibu wa Zimamoto Mkoa wa Lindi, Joseph Mwasabeja, ameishukuru serikali akisema vifaa hivyo vitapunguza changamoto za uokozi na kuimarisha utayari wa jeshi hilo.

Makarani waongozaji wapiga kura 377 wa Jimbo la Mtama, mkoani Lindi, wametakiwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo ya...
25/10/2025

Makarani waongozaji wapiga kura 377 wa Jimbo la Mtama, mkoani Lindi, wametakiwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo ya uchaguzi ili kuhakikisha zoezi la kupiga kura linafanyika kwa amani na bila malalamiko.

Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo hilo, Boniface Fungo, akifungua mafunzo kwa makarani hao leo Oktoba 25, 2025, amesisitiza umuhimu wa kutekeleza majukumu kwa uadilifu na haki, kwa kuzingatia viapo vyao vya utii.

“Mkafanye kazi kwa kuzingatia viapo mlivyokula. Msiwadharau wananchi watakaofika kupiga kura; wahudumuni kwa heshima na usawa,” amesema Fungo.

25/10/2025

Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Ruangwa, Mwalimu George Mbesigwe, amewataka makarani wa uchaguzi kuhakikisha hawawi chanzo cha malalamiko kutoka kwa vyama vya siasa wakati wa Uchaguzi Mkuu.

Akifungua mafunzo kwa watendaji hao, amesema baadhi yao hapo awali walikuwa wafuasi wa vyama vya siasa, lakini baada ya kula kiapo wanapaswa kufanya kazi kwa uadilifu na kufuata sheria bila upendeleo.

Katika mafunzo hayo yaliyohusisha kiapo cha utii, Msimamizi Msaidizi wa Jimbo hilo, Frank Komba, amesisitiza umuhimu wa kutunza siri na kuzingatia maelekezo ya Tume ya Uchaguzi.

Makarani hao wametoa ahadi ya kusimamia haki, usawa na kanuni katika vituo vya kupigia kura.


19/10/2025

Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Wilaya ya Lindi limewakutanisha mashekh na maimamu wa misikiti kutoka kata 35 za Manispaa ya Lindi kuwakumbusha umuhimu wa kushiriki katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29 mwaka huu.

Shekhe Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mohammed Mshangani, amewataka waumini kujitokeza kupiga kura kwa amani, akisisitiza kuwa hiyo ndiyo njia ya kupata viongozi bora watakaoipeleka nchi mbele.

Amesisitiza pia umuhimu wa kutii sheria za uchaguzi na kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima katika vituo vya kupigia kura.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa BAKWATA Wilaya ya Lindi, Abdalah Madebe, amesema mafunzo hayo yamelenga kuwakumbusha viongozi wa dini haki na wajibu wao wakati wa uchaguzi.

Baadhi ya washiriki wameahidi kuwa mabalozi wa kuhamasisha waumini wengine kushiriki kwa amani.

19/10/2025

Bodi ya Korosho Tanzania (CBT) imezindua mkakati maalum wa kuimarisha usimamizi wa ubora wa korosho, ili kuongeza ushindani wa kimataifa na kuinua bei sokoni.

Mkurugenzi wa CBT, Francis Alfred, amesema bodi imeanza kudhibiti ubora kuanzia ngazi ya vyama vya msingi na imefanya usaili wa waendeshaji maghala kwa kushirikiana na TCDC na WRRB.

Amesema mwaka huu CBT inalenga uzalishaji wa tani 70,000 za korosho, huku vijana 500 wa programu ya Jenga Kesho wakisambazwa kusimamia ukusanyaji na ubora wa zao hilo.

CBT imesisitiza kuwa itaendelea kuongeza tija kwa wakulima na uwazi katika mauzo ya korosho.

18/10/2025

Mwenyekiti wa Bodi ya Korosho Tanzania (CBT), Brigedia Jenerali Aloyce Mwanjile, amesema kuwa minada ya korosho kwa msimu wa 2025/2026 inatarajiwa kuanza rasmi tarehe 31 Oktoba 2025.

Akizungumza na waandishi wa habari leo hii 18 October, Brigedia Jenerali aloyce Mwanjile amesema kuwa minada ya korosho itaendelea kuendeshwa kwa mfumo wa minada ya mtandaoni chini ya usimamizi wa Soko la Bidhaa Tanzania (TMX), lengo likiwa ni kuongeza uwazi na ufanisi katika biashara ya zao hilo.

Ameeleza kuwa, kihistoria, minada ya korosho imekuwa ikianza wiki ya mwisho ya Oktoba kutokana na wingi wa korosho ghafi zinazokusanywa ghalani katika kipindi hicho.

Aidha, amevitaka vyama vya msingi (AMCOS) kuanza kupokea korosho za wakulima kuanzia Oktoba 22, 2025, kwa sharti la kuwa na unyevu usiozidi asilimia 10. Amesema pia kuwa kuanzia Oktoba 25, 2025, ghala kuu zitaanza kupokea korosho ghafi zenye ubora uliokubalika, tayari kwa maandalizi ya minada.

Mwanjile ameongeza kuwa Bodi ya Korosho itaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa taratibu zote ili kuhakikisha wakulima wananufaika ipasavyo na mazao yao katika msimu huu mpya wa mauzo.

Address

1050, Mtwara
Mikindani

Telephone

+255682907172

Website

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Kusini Yetu Online Tv posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Business

Send a message to Kusini Yetu Online Tv:

Share