Dizzim Fm

Dizzim Fm Official page for Dizzim fm | Instagram & Twitter | Frequency 93.1 Morogoro |

13/05/2026

Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam limethibitisha kupatikana kwa sehemu ya kichwa cha marehemu James Rogers Temba, mwanafunzi wa mwaka wa pili wa Chuo cha IFM, kilichokuwa kikitafutwa baada ya mauaji yaliyotokea mwishoni mwa mwezi Aprili mwaka huu.

Kwa mujibu wa taarifa ya polisi, sehemu hiyo ya mwili ilipatikana eneo la Kitunda Kibeberu, Ilala jijini Dar es Salaam ikiwa imefukiwa ardhini, kufuatia uchunguzi wa kina ulioendelea tangu tukio hilo liripotiwe rasmi Aprili 30, 2026.

Polisi wamesema jumla ya watuhumiwa watano wanashikiliwa kuhusiana na tukio hilo, akiwemo mganga wa kienyeji anayetambulika kwa jina la Said Ally maarufu “Side”, huku taratibu za kisheria zikiendelea ili hatua zaidi zichukuliwe dhidi ya watuhumiwa hao.

13/05/2026

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Adam Kighoma Malima, amenunua tiketi 1000 kwa ajili ya mashabiki 1000 wa kwanza watakaoingia Uwanja wa Jamhuri kuangalia mchezo wa Ligi Kuu kati ya Mtibwa Sugar na KMC utakaochezwa kesho mjini Morogoro.

Malima, ambaye pia ni mlezi wa Mtibwa Sugar, amesema hatua hiyo inalenga kuhamasisha wakazi wa Morogoro kuendelea kuipenda na kuiunga mkono timu yao licha ya changamoto za matokeo kwenye msimamo wa ligi. Ameeleza kuwa ana imani kubwa na kikosi hicho kuelekea mchezo huo muhimu.

Aidha, amesema serikali ya mkoa inaendelea kuboresha Uwanja wa Jamhuri kwa kuweka taa, viti, kuongeza vyoo pamoja na kuboresha vyumba vya kubadilishia nguo ili kuendana na maandalizi ya AFCON 2027 na kuvutia timu zitakazokuja kufanya mazoezi mkoani Morogoro.

13/05/2026

Wakulima wa ufuta Wilaya ya Momba mkoani Songwe wamesema mfumo wa minada ya kidijitali umeongeza uwazi, ushindani wa bei pamoja na kuondoa changamoto za unyonyaji zilizokuwa zikijitokeza katika biashara holela ya mazao yao.

Wakizungumza baada ya kushiriki mnada wa kwanza wa kidijitali wa ufuta kwa msimu wa 2025/2026, wakulima hao walikubaliana kuuza ufuta wao kwa bei ya shilingi 2,714.90 kwa kilogramu, wakieleza kuwa mfumo huo umeongeza uhakika wa soko na kuwasaidia kupata bei zenye tija zaidi.

Aidha, wameipongeza serikali kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) kwa kuendelea kutoa elimu kuhusu uzalishaji bora, ubora wa mazao pamoja na biashara ya mazao katika soko la dunia, hali inayowasaidia wakulima kuongeza ushindani wa mazao yao.

13/05/2026

Serikali imeahidi kuendelea kusimamia ustawi na maendeleo ya vijana ili kuhakikisha wanapata mazingira bora ya kujifunza, kujiajiri, kuajiriwa pamoja na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya taifa.

Akizungumza katika tamasha la Nje ya Box Youth Talk lililoandaliwa na Ufaulu Project, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Vijana kutoka Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Godfrey Massawe, amesema serikali itaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali zinazowawezesha vijana kutumia vipaji, ubunifu na elimu yao kujiletea maendeleo.

Kwa upande wake, Mwanzilishi wa Ufaulu Project, Simon Chamy, amesema majukwaa ya vijana yana mchango mkubwa katika kuwajengea uwezo, kuwapa hamasa pamoja na kuwaunganisha na wadau mbalimbali wa maendeleo. Zaidi ya vijana 1,600 walihudhuria tamasha hilo lililolenga kujadili fursa na changamoto zinazowakabili vijana nchini.

13/05/2026

Timu ya Mtibwa Sugar leo Mei 12, 2026 imefanya mazoezi katika Uwanja wa Jamhuri Morogoro kujiandaa na mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya KMC utakaochezwa Mei 14 mwaka huu.

Kocha wa timu hiyo, Yussuph Chipo, amesema kikosi hicho kinaendelea kupambana kuhakikisha kinabaki katika Ligi Kuu, huku akieleza kuwa maandalizi yanaendelea vizuri kuelekea mchezo huo muhimu.

Kwa upande wake, nahodha wa timu Oscar Masai amesema kurejea kucheza katika Uwanja wa Jamhuri Morogoro kutawaongezea morali na hamasa wachezaji, ikiwa ni mara ya kwanza kwa Mtibwa Sugar kutumia uwanja huo tangu kuanza kwa msimu wa Ligi Kuu 2025/2026.

12/05/2026

Gari aina ya Toyota Hiace limeteketea kwa moto katika eneo la Mwenge Mataa jijini Dar es Salaam baada ya kile kilichoelezwa kuwa ni hitilafu ya kiufundi kwenye mfumo wa gari hilo.

Moto huo ulizuka wakati gari likiwa linaendelea na safari barabarani, hali iliyosababisha taharuki kwa wananchi pamoja na watumiaji wengine wa barabara waliokuwa eneo hilo kwa kuhofia moto kusambaa zaidi.

Hata hivyo, hakuna taarifa za majeruhi wala vifo zilizoripotiwa kufuatia tukio hilo, huku chanzo kikitajwa kuwa ni hitilafu ya mfumo wa umeme wa gari hiyo.

12/05/2026

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapo, amesema serikali imejipanga kuongeza kasi ya upimaji wa mipango ya matumizi ya ardhi vijijini ili kupunguza migogoro ya ardhi na kuhakikisha matumizi bora ya maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa jukwaa la matumizi ya ardhi mkoani Morogoro, Akwilapo amesema hadi sasa vijiji 4,925 vimepimwa sawa na asilimia 40, huku vijiji zaidi ya 7,400 vikiwa bado havijapimwa, jambo linalohitaji juhudi zaidi kutoka serikalini na wadau wa maendeleo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Joseph Mafuru, amesema jukwaa hilo litasaidia kuweka mikakati ya utekelezaji wa mipango ya matumizi ya ardhi kwa vitendo, huku Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Adam Malima akieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza migogoro ya ardhi nchini.

12/05/2026

Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, Hamis Shabani Taletale maarufu (), amependekeza kuwepo kwa huduma ya ambulance ndani ya treni ya SGR ili kusaidia usafirishaji wa wagonjwa kutoka Morogoro kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa haraka na usalama zaidi.

Akizungumza kuhusu changamoto za matibabu kwa wananchi wa Morogoro, Babu Tale amesema wengi hawawezi kumudu gharama za kukodi ndege au ambulance binafsi kwenda Dar es Salaam, hivyo huduma hiyo ndani ya SGR ingeweza kuwa msaada mkubwa kwa wagonjwa wanaohitaji rufaa.

Aidha, amesema anaamini Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, atalifanyia kazi wazo hilo kwa kuwa ni kiongozi msikivu anayejali ustawi wa wananchi.

12/05/2026

Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, Hamis Shabani Taletale maarufu (), amesema aliwahi kumuomba Rais kuboresha Hospitali ya Mkoa wa Morogoro kutokana na changamoto ya msongamano mkubwa pamoja na uchakavu wa majengo ya hospitali hiyo.

Akizungumza kuhusu hali ya hospitali hiyo, Babu Tale amesema licha ya wananchi kuendelea kupata huduma za matibabu, mazingira na majengo yaliyopo ni ya muda mrefu na yanahitaji maboresho makubwa ili kuendana na ongezeko la wagonjwa.

11/05/2026

Bodi ya Nishati Vijijini (REB) imewataka wananchi kuwa walinzi wa kwanza wa miundombinu ya umeme inayotekelezwa na serikali kupitia miradi ya REA, huku ikionyesha wasiwasi juu ya matukio ya wizi wa vifaa vya umeme katika baadhi ya maeneo nchini.

Akizungumza Mei 11, 2026 mkoani Manyara, Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Balozi Meja Jenerali Mstaafu Jacob Kingu, amesema serikali imetumia fedha nyingi kuhakikisha huduma ya umeme inawafikia wananchi wa vijijini, hivyo ni muhimu wananchi kushiriki kulinda miundombinu hiyo dhidi ya hujuma na vitendo vya wizi.

Aidha, REA imeeleza kuwa zaidi ya shilingi bilioni 45.8 zimetengwa kwa ajili ya miradi ya kusambaza umeme katika vitongoji 267 vya mkoa wa Manyara, huku vijana wa maeneo yanayotekelezwa miradi hiyo wakipewa kipaumbele katika fursa za ajira zinazotokana na utekelezaji wa miradi hiyo.

Address

Mtawala
Morogoro

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Dizzim Fm posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Share

Category