23/07/2026
Wadau kutoka Taasisi mbalimbali Mkoani Mtwara wameaswa kuimarisha ushirikiano katika kupambana na usafirishaji Haramu wa Binadamu, kupitia kutoa elimu kwa wananchi na utaratibu wa pamoja wa hatua za kisheria na utendaji.
Wito huo umetolewa Leo Julai 23, 2026 Mkoani Mtwara na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Dkt Benedicto Ngaiza wakati akifungua semina ya kuhusu Usafirishaji haramu wa Binadamu na Uhamiaji salama.
Dkt Ngaiza amesema, Usafirishaji haramu wa Binadamu ni uharifu mkubwa unaokiuka haki za Binadamu na kuvunja utu wa Mwanadamu.
Ameongeza kuwa uhalifu huu unathiri sana Wanawake, Watoto, vijana pamoja na makundi mengine yaliyo katika mazingira hatarishi.
Nao baadhi ya washiriki wa semina hiyo wamesema, imekuja kwa wakati muafaka na ni muhimu sana na ni mambo ambayo yamekuwa yakitokea kwenye Jamii zetu na Kuna wakati wananchi wanafanya kwa kujua na kutokujua.
"Kuna vijana waliletwa na kushawishiwa kutoka Dar es Salaam na walihaidiwa kuja kufanya kazi hapa Mkoani Mtwara, lakini walivyofika ile kazi waliyohaidiwa hawakupata, ndipo kijana mmojawapo, alimtumia ujumbe baba yake kuwa tangu wamefika hapa hakuna kazi yeyote inayoendelea naomba nitumie hela ya chakula, sababu aliyewashawaishi aliwaambia waje na hela zao na wakifika watarudishiwa, lakini baada ya kufika, aliwazungusha na bila kuwarudishia hela zaidi ya mwezi, ndipo baba wa kijana huyo alipiga simu na akatueleza sehemu alipo huyo kijana na tukampata huyo mtu aliyewaleta na tukamwambia awarudishe vijana wote 30 na kurudishwa Dar es Salaam" amesema Bahati Sendela Naibu Mkuu wa upelelezi Mkoa wa Mtwara.
Semina hiyo imeandaliwa na shirika la CVM kwa ufadhili wa serikali ya Italia kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Sekretarieti ya kupambana na Usafirishaji Haramu wa Watu (ATS) ambao imewashirikisha wadau kutoka vyombo vya ulinzi na Usalama, Mahakama, Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Uhamiaji, Maafisa Ustawi wa Jamii, Viongozi wa Dini, Viongozi wa Serikali Wawakililishi wa Asasi za kiraia.