14/05/2026
Wanafunzi na Waalimu wa shule ya sekondari ya Wasichana Geita wamemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uwekezaji wake mkubwa wa zaidi ya Shilingi Bilioni 4.6 katika shule hiyo, suala ambalo limerahisisha mazingira ya upataji na utoaji wa elimu ikiwa ni pamoja na ujenzi wa maabara, maktaba na Mabweni ya kisasa pamoja na nyumba za waalimu.
Ujenzi wa shule hiyo ni utekelezaji wa mpango mkubwa wa Rais Samia wa kuimarisha elimu ya sayansi kwa wasichana Nchini, lengo likiwa ni kuongeza idadi ya wasichana wanaosoma masomo ya sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati pamoja na kuwapa mazingira salama na bora ya kujifunzia ili waweze kushindana katika taaluma mbalimbali.
"Shule hii imejengwa kwa fedha za Watanzania kwa awamu mbili ambazo zilitumika kujenga madarasa 12, mabweni 8, nyumba mbili za waalimu, lakini pia ikajenga matundu 19 ya vyoo na vyote hivi vimekamilika kwa asilimia 100." Amesema Mwalimu Mwamini George, Mkuu wa Shule ya Sekondari Geita.
Mwalimu Mwamini kadhalika amemshukuru Rais Samia kwa ujenzi wa nyumba za waalimu katika shule hiyo suala ambalo limewaweka waalimu katika mazingira salama, rafiki na ya karibu, akiungana pia na Mwalimu Japhet Thobias ambaye amesema ujenzi wa shule hizo Nchi nzima zimesaidia pia katika kutoa fursa ya ajira kwa waalimu wengi.
Aidha kwa upande wao wanafunzi wa shule hiyo Lydia Hezema, Rahel Marwa na Penina Mshegoli, wamemshukuru Rais Samia kwa kuwawekea mazingira rafiki ya kusoma, wakimuahidi kusoma kwa bidii pamoja na kumtumia k**a kilelezo sahihi cha kuamini kuwa wanaweza kutimiza ndoto zao mbalimbali ikiwemo za kutamani kuwa Viongozi wakubwa wa baadae.