29/08/2026
30-August-2026
DOMINIKA YA 22 YA MWAKA
TAFAKARI KATEKESI
Na Padri Emmanuel Gembuya
Jimbo Katoliki Bariadi
0764545247
Somo 1
Yer 20:7-9
Ee Bwana, umenihadaa, nami nimehadaika; wewe una nguvu kuliko mimi, ukashinda; nimekuwa kitu cha kuchekesha, mchana kutwa; kila mtu hunidhihaki. Maana kila ninenapo napiga kelele; nalia, Dhuluma na uharibifu! Kwa kuwa neno la Bwana limefanywa shutumu kwangu, na dhihaka, mchana kutwa. Nami nikisema, Sitamtaja wala sitasema tena kwa jina lake; ndipo moyoni mwangu kumekuwamo k**a moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu, nami nimechoka kwa kustahimili, wala siwezi kujizuia.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 63:1-5, 7-8 (K) 1a
Ee Mungu, Mungu wangu, nitakutafuta mapema,
Nafsi yangu inakuonea kiu.
Mwili wangu wakuonea shauku,
Katika nchi kame na chovu, isiyo na maji.(K)
(K) Ee Bwana, Mungu wangu, nafsi yangu inakuonea kiu.
Ndivyo nilivyokutazama katika patakatifu,
Nizione nguvu zako na utukufu wako.
Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai,
Midomo yangu itakusifu.(K)
Ndivyo nitakavyokubariki maadamu ni hai,
Kwa jina lako nitaiinua mikono yangu.
Nafsi yangu itakinai k**a kushiba mafuta na vinono,
Kinywa changu kitakusifu kwa midomo ya furaha.(K)
Maana Wewe umekuwa msaada wangu,
Na uvulini mwa mbawa zako nitashangilia.
Nafsi yangu imekuandama sana,
Mkono wako wa kuume unanitegemeza.(K)
Somo 2
Rum 12:1-2
Basi ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.
Shangilio
Lk 21:36
Aleluya, aleluya,
Kesheni kila wakati, ili mpate kuokoka,
na kusimama mbele ya Mwana wa Adamu.
Aleluya!
Injili
Mt 16:21-27
Tangu wakati huo Yesu alianza kuwaonya wanafunzi wake ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka. Petro akamchukua, akaanza kumkemea, akisema. Hasha, Bwana, hayo hayatakupata. Akageuka, akamwambia Petro, nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu. Wakati huo Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayeipoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona. Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake? Kwa sababu Mwana wa Adamu atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika zake; ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake.
MSALABA K**A ALAMA YA USHINDI
Somo la kwanza (Yer 20:7-9) ni kutoka kitabu cha nabii Yeremia. Katika somo hili, Yeremia anamtolea Mwenyezi Mungu manung’uniko na uchungu ambao kazi yake ya unabii imemletea. Anamwambia Mwenyezi Mungu “umenihadaa nami nikahadaika” yaani umenidanganya nami nikadanganyika. Yeremia anaona amedanganyika kwa sababu ahadi ambazo Mungu alimpa alipomwita kuwa nabii zimegeuka kuwa kinyume.
Sasa kila anayemwona anamcheka, neno analotangaza haoni k**a linapenya katika maisha ya watu. Na hata yeye badala ya kupokelewa k**a mjumbe wa Mungu anaonekana kituko machoni mwao. Pamoja na manung’uniko hayo yote, pamoja na kukata tamaa, Yeremia bado anashangazwa na kitu kimoja. Anapoamua kuiacha kazi ya unabii na kupanga kutokuhubiri tena Neno la Mungu, anashindwa.
Hawezi kujinasua kutoka katika utume wa unabii aliokwisha upokea na aliokwisha uanza. Kimwili amekata tamaa lakini bado kwa ndani Neno la Mungu linawaka na linamsukuma aendelee kulitangaza.
Nabii Yeremia, katika somo la kwanza, analetwa kwetu leo k**a mfano wa namna ya kujikana mwenyewe. Manung’uniko yake, kukata kwake tamaa na hata kufikia hatua ya kutaka kuuacha utume wa unabii ni matokeo ya kutokujitambua k**a mfuasi na mtumishi anayepaswa kujikana. Mtumishi hapaswi kujiweka katika ngazi moja na utume ambao Mungu amemwitia.
Utume ambao Mungu anamwita mtu na kumpatia unazo njia zake na unayo malengo yake ambayo si mara zote yataendana na malengo ya yule aliyeitwa kuufanya. Na tena ni mtumishi anayebeba gharama za utume aliopewa. Gharama hizo anazibeba kwa kujikana, yaani kujisadaka na kwa kukubali atumike ili utume usonge mbele. Yeremia anatuonesha kuwa hata pale sadaka inapokuwa kubwa, mtumishi hapaswi kuukimbia utume alioupokea.
K**a usemavyo msemo maarufu “bora punda afe lakini mzigo ufike”, ni muhimu kutambua kuwa ni utume ulio na kipaumbele kupita maslahi binafsi ya mtumishi.
Somo la pili (Rum 12: 1-2) ni kutoka katika waraka wa Mtume Paulo kwa Warumi. Katika mpangilio wa waraka kwa Warumi, sura hii ya 12 ambayo tunaisoma leo inafungua sehemu ya pili ya waraka, sehemu ambayo Paulo anajielekeza kutoa maonyo na maelekezo mbalimbali kuhusu maisha ya kila siku ya wakristo wa Rumi.
Leo anawaambia “itoleeni miili yenu k**a sadaka hai na takatifu impendezayo Mungu”. Na tena anawaonya wasishawishike kuiga mitindo ya watu wa ulimwengu bali wao k**a wakristo wazigeuze fikra zao, wamuelekee Mungu ili walitambue na kulitenda lililo jema, lililo kamilifu na lile linalofaa.
Paulo anawaandikia maonyo haya akiyatambua fika mazingira ya Roma ya wakati huo. Huu ulikuwa ni mji mkubwa yalipokuwa makao makuu ya dola ya kirumi. Ni mji ulikusanya kila aina ya watu hivi kwamba pamoja na maendeleo uliokuwa nayo, ulijikuta kuwa pia na mmomonyoko mkubwa wa maadili na uchaji.
Mausia ya Paulo yalilenga basi kuwatahadharisa wakristo walioishi katika mji huu ili wasipoteze utambulisho wao wa kuwa wakristo na wasimezwe na mitindo ya wakazi wa mji huo. Somo hili linazungumza nasi pia ambao mazingira ya ulimwengu tunaoishi hayatofautiani sana na ya Roma ya wakati wa Paulo. Mwaliko ni uleule wa kutunza utambulisho wetu ili tusimezwe na mitindo ya sasa ya ulimwengu.
Waraka wa Mtume Paulo kwa Warumi na mafundisho yake juu ya maisha ya kila siku yampasayo mkristo ndiyo ufuasi wenyewe. Kisha kujikana na kisha kujitwika msalaba, mfuasi anaalikwa kuyaweka katika maisha yake ya kawaida ya siku kwa siku yale anayoyaamini na kuyachuchumalia kwa sadaka na matumaini makubwa.
Injili ya Dominika hii ni kutoka kwa mwinjili Mathayo (Mt 16:21-27). Petro ambaye ni kitambo kidogo tu amekiri Yesu kuwa ndiye Kristo na ambaye Kristo mwenyewe amemwita mwamba ambao juu yake atalijenga kanisa lake, sasa anageuka kuitwa shetani.
Tunasikia katika injili ya leo Yesu anamwambia “rudi nyuma yangu shetani maana wewe huyawazi yaliyo ya Mungu bali yaliyo ya wanadamu”. Karibu katika Israeli yote kulikuwa na mambo makubwa mawili yaliyowatatiza watu kumhusu Yesu.
La kwanza lilikuwa ni kukubali kuwa Yesu ndiye Kristo, yaani Yesu ndiye masiha yule aliyetabiriwa na ndiye masiha aliyekuwa akingojewa kwa miaka mingi. La pili lilikuwa ni kukubali kuwa huyu Yesu ni Masiha atakayeteswa, yaani ataudhihirisha umasiha wake na kuwaokoa watu kwa njia ya mateso. Kwa myahudi ilikuwa haiingii akilini kuchora picha ya masiha mteswa. Ilikuwa ni fedheha na kashfa kubwa.
Petro alipomkiri Yesu kuwa ndiye Kristo alivuka kizingiti cha kwanza. Lakini alishindwa kuvuka kizingiti cha pili cha kukubali kuwa itampasa Yesu kuigia katika mateso hadi kuuwawa na siku ya tatu kufufuka.
Yesu anamkaripia na kutumia maneno makali hadi kumuita shetani ili kurekebisha kasoro hiyo waliyokuwa nayo watu kumhusu. Ni hapa tunaona kuwa karipio hili la Yesu kumuita Petro shetani sio lake peke yake. Ni karipio la wote ambao wanamwamini Yesu kuwa ndiye Kristo lakini bado hawataki au hawako tayari kumfuata katika njia ya mateso Kristo huyo wanayemuamini.
Mtume Petro katika Injili analetwa kwetu k**a mfano mintarafu kigezo cha kujitwika msalaba.
Petro kwa kumzuia Yesu asiingie katika mateso na kifo msalabani ni kushindwa kukipokea kigezo cha pili cha ufuasi, yaani kujitwika msalaba. Njia ya msalaba ni njia ngumu na tena yenye mateso na uchungu mwingi. Hakuna ambaye katika hali ya kawaida angaliichagua k**a kungalikuwa na njia nyingine ya kupita.
Yesu anatudhihirishia kwa mara nyingine tena leo kuwa mfuasi hawezi kuikwepa njia ya msalaba bila kugeuka yeye mwenyewe kuwa kikwazo kwa wokovu. Ni katika njia ya msalaba ndipo unapolala wokovu.
Yesu anatualika tuibebe misalaba yetu tumfuate akijua fika kwamba ni misalaba hiyo hiyo ambayo kwa uhalisia ndiyo inayotubeba sisi kutufikisha katika wokovu anaotuitia.
Mwenyezi Mungu na atujalie neema katika juma hili na siku zote za maisha yetu ili tuweze kujikana na kujitwika misalaba yetu ili tumfuate mwanae Yesu Kristo kila siku ya maisha yetu bila kusitasita na bila kizuio.
Ombi;Tuombe neema ya Mungu itusaidie kuibeba misaba yetu kikamilifu tukiifungamanisha na Kristo ili iwe misalaba ya ushindi.
TUMSIFU YESU KRISTO
TAFAKARI KATEKESI