06/07/2026
BALOZI LAZARO NYALANDU AIPONGEZA SNADAREAL TV KWA KUIBUKA MSHINDI MDAU SHUPAVU AWARD BEST DIGITAL MEDIA PLATFORM.
Balozi na Mshauri wa Rais Masuala ya Diplomasia, Balozi Lazaro Nyalandu, ameipongeza Snadareal TV kwa kuibuka mshindi wa Tuzo za Mdau Shupavu Awards 2026 katika kipengele cha Best Digital Media Platform, akieleza kuwa ushindi huo ni uthibitisho wa mchango mkubwa wa chombo hicho katika kuhabarisha jamii na kuhamasisha maendeleo ya Mkoa wa Singida na Taifa kwa ujumla.
Tuzo hizo zilitolewa Mei 25, 2026 katika Ukumbi wa Aqua Vitae Resort, mkoani Singida, chini ya uratibu wa Mkurugenzi Mkuu wa Holly Smile, Arnold Bweichum. Kwa mujibu wa Balozi Nyalandu, mafanikio hayo yametokana na juhudi, ubunifu na weledi wa Snadareal TV katika kuwasilisha habari zenye maslahi kwa wananchi.
Akizungumza mapema mwezi Julai 2026 alipokutana na Mkurugenzi wa Snadareal TV, John Hassan, Balozi Nyalandu alisema amekuwa akifuatilia kwa karibu kazi zinazofanywa na chombo hicho, ambazo zimeendelea kuhabarisha wananchi kuhusu masuala mbalimbali ya kijamii, kiuchumi na maendeleo, hususan ndani ya Mkoa wa Singida.
“Nimekuwa nikishuhudia kwa karibu kazi kubwa inayofanywa na Snadareal TV katika kuhabarisha wananchi kuhusu masuala mbalimbali ya kijamii, kiuchumi na maendeleo mkoani Singida na nchini. Ushindi huu ni motisha wa kuendelea kufanya kazi kwa weledi na ubunifu zaidi,” alisema Balozi Lazaro Nyalandu.
Aidha, Balozi Nyalandu alimtakia kila la heri Mkurugenzi wa Snadareal TV pamoja na timu nzima ya chombo hicho, akiwahimiza kuendelea kusimamia maadili ya taaluma ya uandishi wa habari na kutumia jukwaa lao kuhabarisha umma kwa usahihi, uwajibikaji na uzalendo huku wakichochea maendeleo ya jamii.
https://www.instagram.com/p/DabgdV1DOg0/?igsh=amE3Zzk4YXFyenBz