13/06/2026
Rais wa Nigeria, Bola Tinubu, ametoa onyo kali kwa magaidi, watekaji nyara na wafadhili wa ugaidi nchini humo, akiwataka kujisalimisha mara moja au wakabiliane na operesheni kali za kijeshi zinazoungwa mkono na bajeti kubwa zaidi kuwahi kutengwa kwa sekta ya usalama.
Akihutubia taifa katika maadhimisho ya Siku ya Demokrasia Juni 12, 2026, Tinubu alisema serikali yake imepiga hatua kubwa katika mapambano dhidi ya makundi ya wanamgambo, licha ya matukio ya hivi karibuni ya utekaji wa wanafunzi katika majimbo ya Oyo na Borno.
Rais huyo alibainisha kuwa bajeti ya mwaka 2026 imetenga zaidi ya trilioni 5.41 za naira kwa shughuli za ulinzi na usalama, kiwango kikubwa zaidi kuwahi kutolewa nchini Nigeria. Aidha, serikali imeidhinisha kuajiri zaidi ya maafisa 50,000 wa polisi pamoja na maelfu ya wanajeshi wapya ili kuimarisha usalama katika maeneo yenye migogoro.
Kwa mujibu wa takwimu za serikali, zaidi ya magaidi 13,000 wameuawa katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, huku zaidi ya wapiganaji 124,000 pamoja na familia zao wakijisalimisha kupitia mpango wa marekebisho unaojulikana k**a Operation Safe Corridor tangu mwaka 2023.
Tinubu alisema vikosi vya usalama sasa vinatumia zaidi mashambulizi ya kijasusi na operesheni za usahihi mkubwa kwa ushirikiano na washirika wa kimataifa, hatua ambayo imewezesha kushambuliwa kwa ngome za kundi la ISWAP katika jimbo la Borno.
Hata hivyo, wachambuzi wa masuala ya usalama wanaonya kuwa licha ya mafanikio hayo, visa vya utekaji nyara kwa ajili ya fidia, mashambulizi ya majambazi na uvamizi wa jamii bado vinaendelea katika maeneo mbalimbali ya Nigeria, huku wananchi wakikabiliwa pia na changamoto za mfumuko wa bei na kupanda kwa gharama za maisha.
“Kwa majambazi, watekaji nyara na wafadhili wa ugaidi: Jisalimisheni au mkabiliane na nguvu kamili ya dola ya Nigeria. Fursa hii haitabaki wazi milele,” alisema Rais Tinubu.