08/09/2025
Watimka mbio Peter Mwangi na Fridah Ndida waling’ara katika mbio za maandalizi za Kilomita 21 za Standard Chartered Nairobi Marathon zilizofanyika Parklands Sports Club Jijini Nairobi nchini Kenya.
Katika mbio hizo, zilizowavutia zaidi ya wanariadha 1500, Fridah alitumia muda wa dakika 77 na kuibuka bingwa katika kitengo cha wanawake huku Mwangi akitwaa ushindi kwa upande wa wanaume baada ya kutimka mbio hizo kwa muda wa dakika 65.
Baada ya kushinda mbio hizo, Mwangi alisema ushindi wake ni ishara tosha kuwa yuko tayari kwa mashindano makubwa yajayo ya marathon.
“Kushinda kwangu leo kumenipa faraja kubwa na kunifanya nijiamini licha ya ushindani uliokuwepo huku nikijianda kushiriki kwenye mashindano yajayo makubwa yatakayofanyika mwezi Oktoba. Nina matumaini nitafanya vizuri,” Mwangi aliiambia Radio Mabingwa.
Wanariadha hao walitumia mbio hizo kwa minajili ya maandalizi ya mapema kabla ya kushiriki kwenye mbio za mashindano makubwa ya makala ya 22 ya Standard Chartered Nairobi Marathon ya mwaka huu, yatakayoandaliwa Jumapili ya Oktoba 26, 2025 kwenye eneo la Uhuru Gardens, Jijini Nairobi.
Mbio nyingine za maandalizi ya mapema yatakayofuata, yatakayofanyika kabla ya mashindano makubwa ya makala ya 22 ya Standard Chartered Nairobi Marathon 2025, yataandaliwa Karura Forest, ndani ya kambi ya matibabu ya Kibera Nairobi kisha ifuatiwe na mbio za satellite run ya Mombasa.
Mbio za mwaka huu zinatarajiwa kuwavutia zaidi ya wakimbiaji 30,000 ambao watashiriki katika vitengo mbalimbali, vya Wanawake na Wanaume, k**a vile mbio za marathon za kilomita 42, mbio za half marathon za kilomita 21, mbio za kutembea za kilomita 10 na mbio za kilomita 10 za wanariadha wanaoishi na ulemavu watakaotumia viti vya magurudumu.
Madhumuni ya mbio za mwaka huu za Standard Chartered Nairobi Marathon ni kukusanya zaidi ya kima cha Ksh.70 milioni kusaidia mradi wa Kimataifa wa Standard Chartered’s Futuremakers ulioanzishwa kwa lengo la kuwawezesha vijana, hususan wanawake na watu wanaoishi na ulemavu, kupitia elimu, ajira na ujasiriamali.
Mradi huo ulioanzishwa na benki hiyo ya Standard Chartered, pia unasaidia kizazi kijacho kupata ujuzi, kuimarisha uwezo wao wa kupata ajira na kuanzisha biashara.
Katika mbio za makala ya 21 za Standard Chartered Nairobi Marathon zilizofanyika mwaka jana 2024, Ksh.48 milioni zilikusanywa na kuwekezwa moja kwa moja kwenye mradi wa Futuremakers programmes.
Benki ya Standard Chartered ndio udhamini mbio hizo za Standard Chartered Nairobi Marathon kila mwaka.
, , , , , , , ,