Dawati La Michezo

Dawati La Michezo Hii ni Tovuti ya Michezo na Burudani.

25/07/2025

Vinara wa Ligi ya Taifa Daraja la Pili Kanda ya Kaskazini ya Kundi A ya Shirikisho la Kandanda nchini Kenya (FKF) vijana wa Teita Estate FC ya kutoka Kaunti ya Taita Taveta, wikendi hii, wanacheza mechi mbili za ugenini katika Kaunti ya Kwale.
Kwanza Teita Estate FC wataanza kuwakabili wenyeji wao RWAFA FC kwenye Uwanja wa Nyumba Sita ulioko eneobunge la Msambweni Jumamosi hii ya Julai 26 kabla ya kumalizia kwa kuwavaa Denmark FC katika mechi ya mkondo wa pili itakayogaragazwa kwenye Uwanja wa Kombani ulioko eneobunge la Matuga siku ya Jumapili hii ya Julai 27, 2025.

Teita Estate FC, ambao waliwacharaza Denmark FC mabao 3-0 katika mechi ya mkondo wa kwanza, wamejenga kibanda kileleni mwa jedwali ya ligi hiyo wakiwa na alama 67 baada ya kushuka dimbani mara 26 na kushinda mechi 21 wakitoa sare mechi nne na kupoteza mchezo mmoja.
Walifikisha alama hizo baada ya kupata ushindi wa nyumbani wa mabao 3-0 dhidi ya Mbungoni FC ya kutoka Kaunti ya Kilifi katika mechi iliyofanyika Uwanjani Alexander Complex Jumamosi ya Julai 20, 2025. Nao Denmark FC wanakamata nafasi ya tano kwa alama 52 wakati RWAFA FC ni ya nane ikiwa na alama 39.

Denmark FC waliwazaba Ziwani Youth FC ya Kaunti ya Mombasa mabao 2-0 katika mechi ya ugenini iliyochezwa kwenye Uwanja wa shule ya msingi ya Ronald Ngala (RG Ngala) Jumatano ya Julai 23, 2025.

25/07/2025

Azam FC ya kutoka Vanga huko Shimoni Kaunti ya Kwale, wikendi hii, itacheza mechi mbili za Ligi ya Jimbo la Pwani(CRL) ya Kanda A ya Shirikisho la Soka nchini Kenya(FKF). Jumamosi hii ya Julai 26 Azam FC itaanza kushuka dimbani ugenini katika Kaunti ya Mombasa dhidi ya Mikindani FC kwenye Uwanja wa shule ya msingi ya Kwa Shee huko Mikindani eneobunge la Jomvu.
Siku ya Jumapili hii ya Julai 27 vijana hao wa Azam FC, wanaopata hamasa kutoka Kocha Mkuu Musa Abdallah, watamalizia nyumbani kwa kuwakaribisha wageni Okoa Speciality FC ya kutoka Mombasa katika Uwanja wake wa Azam Complex.

Azam FC inashikilia nafasi ya tano ikiwa na alama 20 katika msimamo wa ligi hiyo ya Kundi A. Mikindani FC ni ya saba kwa alama 18 huku Okoa Speciality FC inakamata nafasi ya 10 baada ya kuambulia alama 16. Mechi hizo zitaanza alasiri saa tisa, kwa Majira ya Afrika Mashariki.
Mwishoni mwa juma lililopita, Azam FC iliondoka na alama moja baada ya kulazimisha kutoa sare ya bao 1-1 ugenini dhidi ya wenyeji wao timu ya Kenya Coast National Polytechnic(KCN Poly FC) kwenye mchezo uliopepetwa Jumamosi ya Julai 20, 2025 katika Uwanja wa MTTI Bomani.

20/07/2025

ORODHA KAMILI YA MAREFA WATAKAOCHEZESHA MICHUANO YA KOMBE LA CHAN 2024

Marefa wa Kati
• Adissa Abdoul Raphiou Ligali (Benin)
• Messie Jessie Oved Nvoulou (Congo)
• Kpan Clement Franklin (Côte d'Ivoire)
• Malala Kabanga Yannick (DR Congo)
• Ahmed Nagy Mosa Mahmoud (Misri)
• Tsegay Teklu Mogos (Eritrea)
• Jammeh Lamin N. (Gambia)
• Nyagrowa Dickens Mimisa (Kenya)
• Ahmed Abdulrazg (Libya)
• Diakhate Ousmane (Mali)
• Milazare Patrice (Mauritius)
• Loutfi Bekouassa (Algeria)
• Diouf Adalbert (Senegal)
• Jelly Chavani (Afrika Kusini)
• Ahmed Arajiga (Tanzania)
• Aklesso Gnama (Togo)
• Melki Mehrez (Tunisia)
• Lucky Razake Kasalirwe (Uganda)
• Vincent Kabore (Burkina Faso)
• Brahamou Sadou Ali (Niger)
• Brighton Chimene (Zimbabwe)
• Mefire Abdou Abdel (Cameroon)
• Bouchra Karboubi (Morocco)
• Shamirah Nabadda (Uganda)
• Kech Chaf Mustapha (Morocco)
• Houssam Benyahya (Algeria)

Waamuzi Wasaidizi
• Ngila Guilain Bongele (DR Congo)
• Lucky Kegalogetswe (Botswana)
• Sanou Habib Judicael Oumar (Burkina Faso)
• Emery Niyongabo (Burundi)
• Rodrigue Menye Mpele (Cameroon)
• Amaldine Soulaimane (Comoros)
• Alao Salim (Benin)
• Fasika Biru Yehualashet (Ethiopia)
• Jawo Abdul Aziz (Gambia)
• Addy Roland Nii Dodoo (Ghana)
• Mwangi Samuel Kuria (Kenya)
• Joel Wonka Doe (Liberia)
• Nassiri Hamza (Morocco)
• Yacouba Abdoul Aziz (Niger)
• Dieudonne Mutuyimana (Rwanda)
• Omer Hamid Mohammed Ahmed (Sudan)
• Wael Hanachi (Tunisia)
• Ronald Katenya (Uganda)
• Eleyeh Robleh (Djibouti)
• Ettien Eba Medard (Côte d'Ivoire)
• Abeigne Ndong Amos (Gabon)
• Sirak Samuel (Eritrea)
• Ally Hamdani Said (Tanzania)
• Malondi Chany (Congo)
• Adel Abane (Algeria)
• Diana Chikotesha (Zambia)

Wasimamizi wa teknolojia ya video ya usaidizi (VMOs)
• Mahmoud Ashour (Misri)
• Dahane Beida (Mauritania)
• Lahlou Benbraham (Algeria)
• Bamlak Tessema Weyesa (Ethiopia)
• Samir Guezzaz (Morocco)
• Hamza El Fariq (Morocco)
• Issa Sy (Senegal)
• Atcho Prierre Ghislain (Gabon)
• Daniel Lareya (Ghana)
• Abongile Tom (Afrika Kusini)
• Yasir Abdalaziz (Sudan)
• Viana Letticia (Eswatini)
• Maria Rivet (Mauritius)
• Akhona Makalima (Afrika Kusini)
• Stephen Yiembe (Kenya)
• Atezambong Fomo Carine (Cameroon)
• Jermoumi Fatiha (Morocco)
• Ghorbal Mustapha (Algeria)

20/07/2025

Algeria, Morocco na Uganda ndizo nchi pekee ambazo zitakuwa na marefa wawili wa kati kila mmoja watakaopuliza kipenga wakati wa michuano ya makala ya nane ya Ubingwa wa mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa Ligi za Nyumbani, yaani Kombe la CHAN 2024. Mashindano hayo yataandaliwa kwa pamoja nchini Kenya, Tanzania na Uganda kuanzia Jumamosi ya Agosti 2 hadi Jumamosi ya Agosti 30, mwaka huu 2025.

Kwa mujibu wa orodha ya majina ya marefa hao wanawake na wanaume iliyotolewa na Shirikisho la Soka Afrika CAF, jumla ya marefa 70 kutoka nchi 36 wanachama wa CAF, ndio watakaochezesha mechi za Kombe la CHAN 2024 wakiwemo waamuzi wa kati 26 na waamuzi wengine 26 wasaidizi pamoja na maafisa 18 watakaokuwa wakisimamia teknolojia ya video ya usaidizi (VMOs) kwa marefa yaani VAR.
Wenyeji wa michuano hiyo Kenya, Uganda na Tanzania, wametoa refa mmoja wa kati kila mmoja huku refa wa Kenya ni Dickens Nyagrowa Mimisa wakati Ahmed Arajiga ni wa Tanzania.

Mataifa hayo pamoja na Uganda pia yatakuwa na waamuzi wasaidizi ambapo Samuel Kuria Mwangi anatoka Kenya wakati Ronald Katenya anatoka Uganda huku Ally Hamdani Said akitoka Tanzania. Mkenya mwengine Stephen Yiembe atakuwa mmoja wa maafisa 18 watakaosimamia teknolojia ya video ya usaidizi (VMOs) kwa marefa yaani VAR.
Marefa Bouchra Karboubi wa Morocco na Shamirah Nabadda wa Uganda ndio wanaongoza kikosi cha marefa wa kati wanawake ilhali Diana Chikotesha wa Zambia na Atezambong Fomo Carine wa Cameroon ni waamuzi wasaidizi wenye uzoefu.

Kabla ya michuano hiyo ya Kombe la CHAN 2024 kuanza marefa hao wanatarajiwa kufanyiwa warsha ya mafunzo kuhusu kanuni zinazozingatiwa na CAF katika uchezeshaji wa soka pamoja na mafunzo zaidi kuhusiana na teknolojia ya video ya usaidizi kwa marefa yaani VAR.

20/07/2025

Gabriel ‘GM’ Mghendi amempongeza mwamuzi wa kati wa Kimataifa kutoka nchini Kenya Dickens Nyagrowa Mimisa kwa kuteuliwa kuwa mmoja wa waamuzi kutoka Kenya watakaopuliza kipenga wakati wa Michuano ya Afrika za Ubingwa wa Mataifa ya Afrika kwa Wachezaji wa Ligi za Nyumbani, yaani Kombe la CHAN 2024.
Mashindano hayo ya CHAN 2024 yanaandaliwa kwa pamoja na Kenya, Tanzania na Uganda na yataanza rasmi Jumamosi ya Agosti 2 hadi Jumapili ya Agosti 30, mwaka huu 2025 ikishirikisha mataifa 19.

Mghendi ambaye ni mwakilishi wa Jimbo la Pwani katika Kamati Kuu ya Kitaifa ya Utendaji (NEC) ya Shirikisho la Soka nchini Kenya FKF amemwagia sifa refa huyo wa Kimataifa kutoka eneo la pwani ya Kenya mwenye beji ya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).

‘’Kwa niaba ya wadau wa soka kutoka Pwani ya taifa letu la Kenya tunakupongeza (Mimisa) kwa kuchaguliwa kuwa mmoja wa marefa watakaopuliza kipenga wakati wa michuano ya kombe la CHAN 2024 na tunakutakia kila la kheri. Na fahamu kuwa hautatubwaga na sina shaka yoyote kwako na huu ni wakati wako muafaka wa kujenga tasnia yako ya kupuliza kipenga katika siku za usoni. ’’ Mghendi aliiambia Dawati La Michezo.

Kiongozi huyo mkongwe wa soka nchini Kenya hakuishia hapo aliongezea kwa kusema kuwa Kombe la CHAN 2024 ni tukio kubwa kwa marefa walioteuliwa kuonyesha uweledi wao wa kupuliza kipenga na shirikisho la soka FKF linafanya kila jitihada kuimarisha na kuinua viwango vya marefa kuwa bora zaidi kwasababu hilo ni mojawapo wa jukumu la FKF.

“Juhudi zetu za kuwajenga marefa zimeshazaa matunda na kuleta matokeo chanya, na kusababisha idadi ya marefa kutoka eneo la pwani ya Kenya, wanaopuliza kipenga kwenye mechi za ligi za hadhi za juu, kuongezeka. ’’ Mghendi alikariri.

Miongoni mwa waamuzi wengine kutoka Kenya waliopata fursa hiyo ya kuchezesha kwenye michuano ya Kombe la CHAN 2024 ni mwamuzi msaidizi Stephen Yiembe kutoka Kaunti ya Nakuru na msimamizi wa teknolojia ya video ya usaidizi kwa marefa yaani VAR Samwel Mwangi Kuria kutoka Kaunti ya Nairobi.
Licha ya refa huyo kupata mafunzo mengi ya hali ya juu ya uchezeshaji wa soka, ana uzoefu katika kuchezesha mechi zenye haiba kubwa za Kimataifa.

Mimisa ameshawahi kuchezesha kwenye michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa vijana wenye umri wa chini ya miaka 20 AFCON U20 iliyoandaliwa mwezi Mei 2025 Jijini Cairo, nchini Misri. Mpuliza kipenga huyo pia alihusika katika mechi ya kufuzu katika michuano ya Kombe la AFCON 2025 kati ya Msumbiji na Mali iliyopigwa mwezi Januari 2025 pamoja na mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya klabu ya Djoliba AC de Bamako ya Mali na ASKO de Kara ya Togo.


18/07/2025
18/07/2025

Hapa ni mapigano ya timu za wasichana wakati wa mashindano ya mchezo wa Taekwondo yaliyofanyika katika Ukumbi wa Marycliff Tudor Kaunti ya Mombasa nchini Kenya siku ya Jumamosi ya Agosti 12, 2025.
Mashindano hayo yalitumika kutafuta kikosi cha timu ya wasichana ya Kaunti ya Mombasa kitakachochuana kwenye mashindano ya Jimbo la Pwani yatakayofanyika Mtwapa Kaunti ya Kilifi siku ya Jumamosi ya Agosti 19, 2025.

Address

Mombasa

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Dawati La Michezo posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Share