25/04/2026
Ferdinand Omanyala alirejea kileleni kwa kishindo baada ya kutwaa ubingwa wa mita 100 katika Kip Keino Classic 2026, akitumia sekunde 9.96 katika uwanja wa Nyayo, Nairobi Ijumaa.
Gift Leotlela alifungiwa nje ya mashindano baada ya kutimua mbio kabla ya ishara rasmi ya kuanza.
Hata hivyo, Omanyala hakutikiswa na presha hiyo, akiongeza kasi hatua za mwisho na kujihakikishia ushindi wake wa tatu katika mkutano huo wa kimataifa.
Rivaldo Roberts alishika nafasi ya pili kwa sekunde 10.12, akifuatiwa na Aaron Brown aliyemaliza wa tatu kwa sekunde 10.15.
Ushindi huo unaendeleza makali ya Omanyala, akiwa tayari ametimka chini ya sekunde 10 mara mbili ndani ya kipindi cha chini ya wiki mbili, baada ya ushindi wa sekunde 9.98 nchini Ethiopia.
Umati mkubwa wa mashabiki ulioingia bure ulilipuka kwa nderemo, ukishuhudia shujaa wao akizunguka uwanja akiwa amejivika bendera ya Kenya.
Malenga Wa Spoti Tony Mballa