08/02/2024
Na Ismail Jussa
MZEE KARUME ALISEMA AKIMNUKUU SITTI BINT SAAD, "MSIJITIE KIWEWE, ZANZIBAR INA WENYEWE."
Leo tuwadokeze kidogo kuhusu kisiwa kiitwacho Latham island (kwa Kiswahili wenyeji wa Zanzibar wanakiita Fungu Mbaraka) ambacho ni katika milki ya Zanzibar.
Kisiwa hicho kiliitwa Latham kutokana na meli ya kiingereza Latham ambayo ilitia nanga hapo mwaka 1878. Hadi mwaka 1898 kikiitwa Fungu Kizimkazi na hatimaye kiliitwa Fungu Mbaraka kwa jina la Ahmed Mbarak aliyepewa ruhusa na Sultan kuzamua mali katika meli iliyozama hapo na akapata utajiri mkubwa.
Latham ilifanywa rasmi kuwa sehemu ya Zanzibar kuanzia tarehe 19 October, 1898. Sir Lloyd Mathews ndiye aliyepewa kazi hiyo na Sultani na akaenda kupachika bendera ya Zanzibar na kuweka tangazo rasmi tarehe hiyo.
Sir Lloyd Mathews alikuwa ndiye First Minister (kwa lugha ya sasa ni k**a Prime Minister) wa mwanzo wa Zanzibar na anatajwa kuwa ndiye aliyeunda jeshi la mwanzo la Zanzibar. Ingawa riwaya nyengine inasema Sir John Kirk ndiye aliyeunda jeshi la mwanzo kukabiliana na Karl Peters (wa Tanganyika) hapo August 1885 lakini akazuiwa na Sir Salisbury, Foreign Secretary (Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza zama hizo) asipigane na Karl na akavunjika moyo sana.
Wajerumani waliwahi kukidai mwaka 1910 na kujibiwa rasmi na Serikali ya Uingereza tarehe 13 April, 1911 kuwa ni cha Zanzibar; tokea hapo hakijawahi kudaiwa tena na dola yoyote.
Mwaka 1959 kupitia Legal Notice No. 56 Zanzibar ilikitangaza Latham Island kuwa ni Bird Sanctuary chini ya Sheria ya Wild Bird Prorection.