17/09/2025
Idara ya Uhamiaji Wilaya ya Mbogwe, mkoani Geita, imefanikiwa kuwakamata wahamiaji haramu 34 kutoka nchi za Burundi na Rwanda, kufuatia oparesheni maalum ya kiusalama iliyoendeshwa kwa weledi mkubwa.
Oparesheni hiyo ilisimamiwa na Afisa Uhamiaji wa Wilaya ya Mbogwe, Mrakibu wa Uhamiaji SI Amir Ally Abbasi, chini ya uratibu wa Kamishna Msaidizi Mwandamizi SACI James Andrew Mwanjotile, Afisa Uhamiaji wa Mkoa wa Geita.
Oparesheni hiyo inatekelezwa kwa mujibu wa maelekezo kutoka kwa Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Tanzania, CGI Dkt. Anna Peter Makakala Ili kuimarisha Ulinzi na Usalama wa Taifa kuelekea uchaguzi mkuu Oktoba 2025.
Wahamiaji hao walinaswa kupitia msako maalum uliolenga yombo vyote vya usafiri vinavyoingia Wilaya ya Mbogwe kupitia barabara kuu inayoelekea Kahama huku lengo kuu likiwa ni kudhibiti wimbi la uhamiaji haramu linaloathiri usalama wa taifa.
SI Abbasi, aliwaonya kwa msisitizo wamiliki wa vyombo vya usafiri – hususan mabasi madogo (Hiace) na malori – kuacha mara moja tabia ya kuwahifadhi au kuwabeba wahamiaji haramu, kwani elimu ya kutosha imeshatolewa kupitia maafisa wa uhamiaji, hivyo sasa ni wakati wa utekelezaji wa sheria bila shuruti.
Ofisi ya Uhamiaji Wilaya ya Mbogwe imeeleza kuwa itaendelea na misako, ukaguzi, na uchunguzi katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo na viunga vyake ili kukabiliana na tatizo la uhamiaji haramu, hasa kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu.