Savvy Media Live

Savvy Media Live MAONI YAKO FB,INSTAGRAM@SAVVY MEDIA LIVE. SIKILIZA SAVVY FM 105.3
LISTEN ONLINE: SAVVY FM ARUSHA.

15/08/2026

Washiriki mbalimbali wa mafunzo ya usimamizi wa ujenzi yaliyoandaliwa na Tanzania Roads Association (TARA) kwa kushirikiana na TANROADS na TARURA wamewashukuru waandaaji wa mafunzo hayo, wakisema yamekuwa chachu ya kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Baadhi ya washiriki waliozungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumalizika kwa mafunzo hayo kwa siku ya tatu , hususan mada kuhusu matumizi ya Akili Bandia (Artificial Intelligence - AI) iliyowasilishwa na mtaalamu kutoka Afrika Kusini, Mhandisi Peter, wamesema teknolojia hiyo itarahisisha utekelezaji wa kazi na kupunguza muda unaotumika kuandaa nyaraka na makabrasha ya miradi ya ujenzi.

Akizungumza baada ya kupokea mafunzo hayo, mshiriki kutoka Bodi ya Wasajili wa Wahandisi (ERB)Dododma,Mhandisi Lightness Mrema, amesema mafunzo hayo yataleta tija kubwa kwa wakandarasi, wasimamizi wa miradi na wadau wengine wa sekta ya ujenzi kwa kuboresha utunzaji wa kumbukumbu, kuongeza ufanisi na kurahisisha utatuzi wa changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika utekelezaji wa miradi.

Naye mshiriki kutoka Namibia, Mhandisi Jonas, amesema ameridhishwa na mafunzo hayo na kueleza kuwa yameongeza uelewa wake kuhusu matumizi ya teknolojia katika usimamizi wa miradi ya ujenzi.

Aidha, Mhandisi Jonas amesema matumizi ya Akili Bandia (AI) yana uwezo wa kuleta matokeo chanya katika sekta ya barabara na ujenzi kwa kuongeza kasi, usahihi na ubora wa utekelezaji wa miradi.

Tanzania Roads Association(TARA) Wakala ya Barabara Vijijini na Mijini - TARURA

Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR)  na kampuni ya Fitch Ratings Ltd wamefanya mazungumzo Agosti 11/2026 ikiwa ni sehemu ya...
12/08/2026

Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) na kampuni ya Fitch Ratings Ltd wamefanya mazungumzo Agosti 11/2026 ikiwa ni sehemu ya mapitio ya pili ya mwaka 2026 ya tathmini ya Fitch Ratings, katika mchakato unaohusisha taasisi mbalimbali za Serikali.

Mazungumzo hayo yanalenga kuwapa wachambuzi wa Fitch Ratings fursa ya kupata taarifa za kina kuhusu mwenendo wa uchumi wa Tanzania, utekelezaji wa sera za kibajeti na fedha, pamoja na mikakati ya Serikali katika usimamizi wa deni la Taifa.

Kwa upande wa OTR, mjadala ulijikita katika utendaji wa taasisi za umma, mageuzi yanayoendelea, vihatarishi vya kifedha, pamoja na mtiririko wa fedha kati ya Serikali na taasisi za Umma.

Mapema mwaka huu, Fitch Ratings iliendelea kuipa Tanzania daraja ‘B+’ kwa hadhi ya ulipaji wa madeni ya muda mrefu ya fedha za kigeni, ikitaja mwelekeo imara wa ukuaji wa uchumi na uwezo wa Serikali kukabiliana na changamoto za kifedha baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

Fitch inakadiria kuwa uchumi wa Tanzania utakua kwa asilimia 6 kwa mwaka 2026, kiwango ambacho ni kikubwa zaidi ya wastani wa asilimia 4.5 kwa nchi zenye daraja la ‘B’.

Katika muktadha huo, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, aliyeongoza timu ya OTR, aliieleza timu ya Fitch kuhusu mageuzi yanayolenga kuboresha utendaji na ufanisi wa taasisi za umma, kuimarisha utawala bora na uwajibikaji, pamoja na kupunguza utegemezi wa taasisi hizo kwa Serikali.

Alisema ajenda ya mageuzi ya OTR katika kipindi cha miaka miwili iliyopita imeweka mkazo zaidi katika uongozi, usimamizi wa utendaji na uwajibikaji, ikiwemo kuboresha ubora wa Bodi na timu za menejimenti na kuimarisha tathmini za Bodi ili kubaini mapungufu ya ujuzi.

Bw. Mchechu alisema matokeo ya mageuzi hayo yanaendelea kuonekana katika mchango wa kifedha wa taasisi za umma kwa Serikali.

Katika mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, 2026, taasisi zilizo chini ya Msajili wa Hazina zilichangia takribani Sh1.881 trilioni kwa Serikali kupitia gawio na michango mingine, ikilinganishwa na Sh1.028 trilioni katika mwaka wa fedha uliotangulia.

OFISI YA MSAJILI WA HAZINA fitchrating

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umefanikiwa kusambaza takribani mitungi laki saba ya gesi ya kupikia (LPG) nchini kote,...
12/08/2026

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umefanikiwa kusambaza takribani mitungi laki saba ya gesi ya kupikia (LPG) nchini kote, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa kasi wa Mkakati wa Kitaifa wa Nishati Safi ya Kupikia. Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Nishati Jadidifu na Teknolojia za Nishati Jadidifu kutoka REA, Mhandisi, Advera Mwijage, wakati akizungumza kwenye mdaharo maalum uliofanyika katika Tamasha la Kizimkazi mkoani wa Kusini Unguja, Zanzibar;

Mhandisi Advera alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy. Mhandisi Advera alieleza kuwa mafanikio hayo yametokana na uwezeshaji mkubwa kutoka kwa Serikali ya Awamu ya Sita, pamoja na uwepo wa vyanzo vingi vya nishati nchini. Alibainisha kuwa REA ilitumia majukwaa ya Waheshimiwa Wabunge kusambaza mitungi hiyo ili kuwafikia wananchi wa ngazi ya chini na kutoa elimu ya matumizi ya nishati hiyo.

Kuhusu utunzaji wa mazingira, Mhandisi Advera alisema REA imeanzisha mradi wa kusambaza majiko banifu ili kupunguza kasi ya uharibifu wa misitu. Inakadiriwa kuwa takribani hekta 470,000 za misitu hukatwa kila mwaka nchini kwa ajili ya kuni na mkaa.

Ili kukabiliana na changamoto hiyo, REA imeshirikiana na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kufungua viwanda vya kuzalisha mkaa mbadala maeneo ya vijijini, tofauti na hapo awali ambapo viwanda hivyo vilikuwa vimejificha mijini.

Hatua hiyo imefanya mkaa mbadala kupatikana kwa gharama nafuu vijijini. Katika hatua nyingine, REA kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), imefanikiwa kuunganisha jumla ya wateja 1,001 wa majumbani na taasisi kwenye mkuza wa mabomba ya Gesi Asilia katika mikoa ya Lindi na Pwani.

Mhandisi Advera alitoa wito kwa wananchi ambao bado hawajafikiwa na miradi hiyo kuendelea kuwa wavumilivu, kwani utekelezaji unaenda kwa awamu kulingana na ukomo wa bajeti ya serikali. Lengo kuu la serikali ni kuhakikisha zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia.

Wizara Ya Nishati Wakala wa Nishati Vijijini (REA)

Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) yenye Makao Makuu jijini Arusha, kwa kushirikiana na Serikali ya Ujerumani (GIZ) imezi...
12/08/2026

Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) yenye Makao Makuu jijini Arusha, kwa kushirikiana na Serikali ya Ujerumani (GIZ) imezindua awamu ya pili ya Shindano la Akili Bandia la EAC, linalojulikana k**a AI4EAC yanayolenga kufikia zaidi ya wananchi 20,000 kwa mafunzo na ujuzi wa teknolojia hiyo.

Mashindano yalizinduliwa jana Makao Makuu ya EAC jijini Arusha, yakilenga kuwezesha vijana, watafiti, wanafunzi na wajasiriamali katika nchi wanachama wa EAC kuunda suluhisho za kiteknolojia zitakazosaidia kutatua changamoto mbalimbali za maendeleo katika ukanda huo.

Katika awamu hiyo, washindi watapata jumla ya dola za Marekani 50,000 k**a zawadi na mtaji wa kusaidia kuendeleza suluhisho zao zinazotumia AI kukabiliana na changamoto za kikanda. - Miongoni mwa maeneo mapya yaliyoingizwa katika mashindano hayo ni changamoto ya kukabiliana na ebola, inayowaalika watafiti, wanafunzi na wabunifu kuandaa mifumo ya AI inayoweza kusaidia kugundua mapema milipuko ya magonjwa, maandalizi na hatua za kukabiliana nayo.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa EAC, Naibu Katibu Mkuu anayesimamia Sekta za Miundombinu, Uzalishaji, Kijamii na Kisiasa, Aguer Malueth alisema kuwa mpango huo unaonyesha dhamira ya EAC ya kuwaandaa raia wake kwa fursa zinazotokana na Akili Bandia, lengo likiwa ni kupanua fursa kwa vijana, watafiti na wajasiriamali katika kanda ya Afrika Mashariki ili kupata ya ujuzi wa Akili Bandia na kubuni suluhisho za vitendo kwa changamoto zinazoikabili Kanda hiyo.

Mhe.Aguer alisema kupitia Muungano huo wanawekeza katika rasilimali watu, huku wakijenga mfumo wa kikanda wa uvumbuzi unaoiwezesha Afrika Mashariki kushindana katika uchumi wa kidijitali wa kimataifa ambapo katika awamu hiyo ya pili imelenga kuwafikia wananchi zaidi ya 20,000 wa Afrika Mashariki kupitia mafunzo ya ujuzi wa AI katika Nchi Wanachama wa EAC.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Afrika Mashariki na Kati katika Wizara ya Shirikisho ya Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo ya Ujerumani (BMZ), Joachim Schmitt, alisema msaada wa Ujerumani kwa tukio hilo unatokana na umuhimu wa kuwa na mkakati wa kikanda katika kuendeleza teknolojia ya AI.

12/08/2026

Katika Siku hii ya Kimataifa ya Vijana, tunasherehekea uwezo wa vijana kuunda mfumo endelevu zaidi wa chakula.

Vijana wanapowezeshwa kwa maarifa, ujuzi, teknolojia, na fursa, wanakuwa vichochezi vikali vya mambo ikiwemo kilimo-ikolojia .

Afrika na Dunia inahitaji uvumbuzi zaidi kwenye kilimo katika suluhisho mbalimbali ili kurejesha afya ya udongo, kulinda bayoanuwai.

Pia kuimarisha mifumo ya chakula ya ndani, na kujenga maisha ya kustahimili hali ya hewa.

Hakuna namna ila kuwekeza kwa vijana.

Hamasisha uvumbuzi. Na kubadilisha kilimo.

Heri ya Siku ya Kimataifa ya Vijana.



11/08/2026

Wataalamu wa sekta ya ujenzi wa barabara nchini wamekutana jijini Arusha kushiriki mafunzo maalumu ya Construction and Supervision of Roads Works yenye lengo la kuimarisha usimamizi wa miradi ya ujenzi wa barabara na kuhakikisha miundombinu inayojengwa inakidhi viwango vya ubora.

Mafunzo hayo yanayofanyika kuanzia Agosti 10 hadi 15, 2026 katika Hoteli ya Gold Crest, Arusha, yameandaliwa na Wizara ya Ujenzi kwa kushirikiana na Tanzania Roads Association (TARA) na Tanzania Transportation Technology Transfer Centre (TanT² Centre), kwa ushirikiano na taasisi mbalimbali za ndani na kimataifa.

Katika mada zilizowasilishwa,na mhandisi,Deogratius Mugishagwe, washiriki wamejifunza misingi ya ujenzi wa barabara ikiwemo hatua za ujenzi, usimamizi wa kazi za eneo la mradi, tabaka za lami, matumizi ya vifaa vinavyokidhi viwango, vipimo vya udhibiti wa ubora, mifumo ya mifereji ya maji, pamoja na wajibu wa msimamizi wa mradi katika kuhakikisha kazi zinafanyika kwa ubora.

Aidha, mafunzo hayo yameangazia kanuni za usanifu wa barabara, uainishaji wa barabara, usanifu wa madaraja na mifumo ya kupitisha maji, pamoja na viwango vya ujenzi wa barabara vinavyotumika katika Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mafunzo hayo yanatarajiwa kuongeza uwezo wa wasimamizi wa miradi ya ujenzi wa barabara na wadau wengine wa sekta hiyo, ili kuboresha ubora wa miundombinu na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa miradi ya barabara nchini.

Washiriki wa mafunzo hayo ni wahandisi watanzania,zimbabwe,Ethiopia na wengine wakishiriki kwa njia ya mtandao nchini Africa ya kusini na wanachama wa Africa Mashariki.Mafunzo haya yatamalizika kwa ziara ya kutembelea miradi ya Tarura katika mradi ya ujenzi wa miundo mbinu ya Afcon.

Wizara ya Ujenzi Tanzania Roads Association(TARA)
Wakala ya Barabara Vijijini na Mijini - TARURA Yann Chin Tan

Tanzania na Marekani zimeendelea kusisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kimkakati katika sekta mbalimbali zikiw...
11/08/2026

Tanzania na Marekani zimeendelea kusisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kimkakati katika sekta mbalimbali zikiwemo madini adimu, nishati, afya, uwekezaji na maendeleo ya kiuchumi, pamoja na dhamira ya kuendeleza mazungumzo na ushirikiano wa kitaalamu kwa manufaa ya nchi hizo mbili.

Hayo yameafikiwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis M***a Omar (Mb) na Kaimu Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Mhe. Andrew Lentz, walipokutana na kufanya mazungumzo ya katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo pia walieleza umuhimu wa kuendelea kutumia majadiliano ya kitaalamu na ushirikiano wa Serikali kwa Serikali katika kushughulikia maeneo yenye umuhimu wa kimkakati, ikiwemo maendeleo ya sekta ya Nishati ya Gesi Asilia (Liquefied Natural Gas (LNG).

Kaimu Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Mhe. Andrew Lentz, alisisitiza kuwa mawasiliano ya karibu na ushirikiano kati ya wataalamu wa pande zote ni muhimu katika kuwezesha utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati.

Aidha, walijadili fursa za kuendelea kuimarisha mazingira ya uwekezaji nchini, ikiwemo miradi mikubwa ya madini na kuongeza thamani ya rasilimali nchini, ambapo walikubaliana kuhusu umuhimu wa kuwa na uratibu mzuri wa Serikali na wawekezaji ili kuhakikisha miradi ya kimkakati inatekelezwa kwa ufanisi na kutoa manufaa kwa uchumi na wananchi.

Kwa upande wa afya, alisema kuwa hivi karibuni, Marekani na Tanzaniaa zimesaini makubaliano ya kuendeleza sekta ya afya yatakayogharimu dola za Marekani bilioni 3.1 katika kipindi cha miaka mitano ijayo kwa ajili ya kuimarisha mifumo ya afya, kukabiliana na magonjwa mbalimbali na kujenga uwezo wa ndani, kuelekea kwenye mifumo endelevu ya afya inayoongeza uwezo wa Tanzania kugharamia na kusimamia huduma za afya kwa muda mrefu, sambamba na kuimarisha uwezo wa kitaifa katika kinga, ufuatiliaji na udhibiti wa magonjwa.

Wizara ya Fedha

Kampuni ya Mainstream Group Limited imeshinda tuzo mbili katika Tuzo za Tehama Awards 2026, ikiwemo nafasi ya pili katik...
11/08/2026

Kampuni ya Mainstream Group Limited imeshinda tuzo mbili katika Tuzo za Tehama Awards 2026, ikiwemo nafasi ya pili katika kipengele cha Ubunifu wa Teknolojia katika Mifumo ya Malipo, huku Mkurugenzi wake, Deogratius Lazari Mosha, akitambuliwa miongoni mwa viongozi bora wa kampuni zinazofanya vizuri katika sekta ya TEHAMA nchini.

Tuzo hizo zimetolewa usiku wa Agosti 9, 2026 katika Ukumbi wa Johari Rotana jijini Dar es Salaam, katika hafla iliyowakutanisha wadau wa teknolojia na uchumi wa kidijitali. Mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Angela Kairuki.
Katika kipengele cha Ubunifu wa Teknolojia katika Mifumo ya Malipo, Mainstream Group imepata nafasi ya pili baada ya kushindanishwa na taasisi mbalimbali, ikiwemo NMB Bank. Tuzo hiyo inaangazia jitihada za kutumia teknolojia kuboresha na kurahisisha huduma za kifedha.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Deogratius Lazari Mosha, ametambuliwa kutokana na mchango wake katika sekta ya TEHAMA.

Mosha pia aliwahi kutunukiwa tuzo ya Kiongozi Bora katika Ubunifu Barani Afrika mwaka 2024 kupitia tuzo za Forty Under 40 Africa zilizoandaliwa na Xodus Communications Limited.

Hii ni mara ya pili kwa Mainstream Group kutambuliwa katika Tuzo za Tehama nchini Tanzania. Mwaka 2024, kampuni hiyo ilishinda tuzo katika kipengele cha Ubunifu katika Matumizi ya TEHAMA kwenye Sekta ya Fedha.

Ushindi huo umekuja miezi kadhaa baada ya kampuni hiyo kushinda zabuni ya kutengeneza mfumo wa usajili wa wanachama wa Simba Sports Club, unaolenga kurahisisha mchakato wa usajili wa wanachama na utoaji wa kadi zao.

Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Mainstream Group, Pascal William, amesema kutambuliwa huko kunatoa msukumo wa kuendelea kutengeneza mifumo inayolenga kutatua changamoto katika sekta mbalimbali, ikiwemo huduma za kifedha na elimu ya juu.

William amesema kampuni hiyo imeshiriki katika utengenezaji wa mifumo ya kurahisisha huduma za benki pamoja na mifumo ya elimu katika vyuo vikuu, ikiwemo Smarti Uni.

Amesema shughuli hizo zimekuwa na mchango pia katika ajira kwa vijana, ambapo kampuni hiyo inatoa ajira rasmi na zisizo rasmi kwa zaidi ya vijana 100 nchini

Mainstream Group Limited TEHAMAwards

Mkuu wa mkoa wa Arusha Mhe.CPA Amos Gabriel Makalla, amefunga rasmi Maonesho ya 32 ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na sherehe...
08/08/2026

Mkuu wa mkoa wa Arusha Mhe.CPA Amos Gabriel Makalla, amefunga rasmi Maonesho ya 32 ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na sherehe zaWakulima Nanenane Kanda ya Kaskazini yanayojumuisha mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Manyara kwenye viwanja vya Themi -Njiro mkoani Arusha leo Agosti 08,2026.

Akizungumza kwa niaba ya Mgeni rasmi Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, Mhe.Makalla amesema kuwa maonesho hayo ya 32 Kanda ya Kaskazini yamekuwa na mabadiliko makubwa kwa kulinganisha na miaka ya nyuma, yakiwa yamesheheni bunifu na teknolojia za kisasa, mbegu bora, zana rahisi na bora za kilimo na mifugo huku wakulima, taasisi na makampuni yakiotoa elimu kwa wakulima, wafugaji na wananchi waliotembelea kwenye Maonesho hayo.

Amesema kuwa, waoneshaji wamejitokeza kwa wingi huku vijana wakipamba mabanda hayo kwa kutoa elimu ya kilimo na ufugaji kwa lengo la kuhakikisha wakulima wanapata elimu ya matumizi ya sahihi ya teknolojia za kisasa, inayokwenda kuongeza uzalishaji kwa kuzingatia uhataji wa soko na ubora wa mazao unaokidhi ushindani wa soko la ndani pamoja na soko la kimataifa.

"Nimefurahishwa kuona vijana wakiwa kwenye mabanda ya teknolojia za kilimo na mifugo wakitoa elimu, hii inaonesha namna vijana wakitanzania wametambua fursa ya kujiajiri kwenye sekta ya kilimo, hasa ukizingatia ajira rasmi zimepungua duniani, vijana wanatoa hamasa kwa Serikali kuongeza fursa na kuimarisha utoaji wa mikopo isiyokuwa na riba kwa vijana ili waongeze mitaji kwenye shughuli zao za kilimo"Amesema CPA Makalla

Hata hivyo, amebainisha kuwa Serikali ya awamu ya sita chini ya Dkt.Samia Suluhu Hasaan imeendelea kutekeleza mageuzi makubwa katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi kwa kuwekeza katika umwagiliaji, uzalishaji wa mbegu bora, pembejeo, huduma za ugani, utafiti, miundombinu ya masoko, maghala, minada ya mifugo, kuongeza thamani ya mazao, ili kuongeza ushindani wa bidhaa zitokanazo na mazao ya masoko ya kikanda na kimataifa.

RS Arusha

Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Bias...
08/08/2026

Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Biashara na Maendeleo (TDB), Bw. Admassu Tadesse, kuhusu namna benki hiyo inavyoweza kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kuimarisha ufanisi wa uwekezaji wa Serikali.

Mazungumzo hayo yana umuhimu wa kipekee kwa Tanzania kwa kuzingatia kwamba Serikali, kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina, inamiliki asilimia 8.3 ya hisa katika TDB na hivyo kuwa miongoni mwa wanahisa wa benki hiyo ya maendeleo ya kikanda.

Mazungumzo hayo yaliyofanyika katika Ofisi ya Msajili wa Hazina jijini Dar es Salaam yalijikita katika maeneo mbalimbali ya ushirikiano, ikiwemo namna TDB inavyoweza kuongeza mchango wake katika maendeleo ya Tanzania na kuimarisha ufanisi wa uwekezaji wa Serikali.

Bw. Mchechu alisema ushirikiano kati ya Tanzania na TDB ni muhimu katika kuendeleza uwekezaji, biashara na upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya miradi yenye mchango katika maendeleo ya uchumi.

Alisema TDB, k**a taasisi ya fedha ya maendeleo ya kikanda, ina nafasi muhimu katika kusaidia Tanzania kutumia fursa zilizopo katika sekta mbalimbali na kuongeza thamani ya uwekezaji wa umma unaosimamiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina, wenye thamani ya Sh92.3 trilioni.

Bw. Mchechu alisema Serikali inaendelea na hatua mbalimbali za kuboresha utendaji wa taasisi za umma, huku akisisitiza uwajibikaji, ufanisi, uongozi wenye ufanisi na matumizi bora ya rasilimali za umma.

Alisema mageuzi hayo yanaenda sambamba na juhudi za kuhakikisha taasisi na kampuni zinazomilikiwa na Serikali zinafanya kazi kwa ufanisi zaidi, zinatimiza malengo ya kuanzishwa kwake na kutoa mchango mkubwa kwa uchumi wa taifa.

Kwa upande wake, Bw. Tadesse alisema TDB iko tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kusaidia juhudi za maendeleo ya kiuchumi na uwekezaji.

Alisema benki hiyo imeendelea kuimarisha uwezo wake wa kutoa masuluhisho mbalimbali ya kifedha, ikiwemo ufadhili wa kibiashara, fedha za masharti nafuu na mifumo ya ufadhili mseto, kwa ajili ya kusaidia miradi yenye mchango.

OFISI YA MSAJILI WA HAZINA
Bank of Tanzania (BoT)
Wizara ya Fedha TD Bank

Address

P. O. BOX 14070
Arusha

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Savvy Media Live posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Shortcuts

Share