29/05/2026
Baada ya kukadiriwa kuwa, watu 1500 huwa wanapoteza maisha kila mwaka Nchini, kutokana na kuugua kichaa cha mbwa, hatimaye Uongozi wa hospitali ya Mbwa wa Afrika, umekuja na kampeni ya kuchanja chanjo ya ugonjwa huo kwa mbwa wote wa mitaa katika Jiji la Arusha, bila malipo, ikiwa nisehemu yakupunguza idadi ya vifo hivyo.
Uongozi huo ukizungumza na GADI TV Mei 28, 2026, umesema kuwa kampeni hiyo imekuja ikiwa sehemu ya mikakati ya kuhakikisha kuwa kila mbwa aliyepo kwenye mtaa anachanjwa ili kuepukana na ugonjwa huo hatari unaoweza kuambukizwa binadamu.
Aidha, inaelezwa kuwa chanjo hiyo itaanza kutolewa kuanzia Mei 30, 2026 kwenye vituo maalum vilivyotengwa kila kata ndani ya jiji hilo, k**a ambavyo inaonekana katika kipeperushi hiki, huku siku ya juma mosi na juma pili kwa kila wiki, ikiwa ndio siku zilizotengwa kwa ajili ya zoezi hilo.
Kadhalika, Uongozi huo umesema kuwa utendaji kazi wa hospitali hiyo, ni pamoja na kutibu mbwa koko wa mitaani ambao wamekuwa wakipata majeraha kutokana na kugongwa na magari barabarani, ambapo wakati mwingine baadhi ya mbwa hulazimika kulazwa wodini na baadae kuruhusiwa baada ya kupona.
Hata hivyo, uongozi huo unaeleza kuwa, hulazimika kupita mitaani nakuwakusanya mbwa wenye changamoto mbalimbali nakufikisha hospitalini hapo, ambapo wengine hutibiwa kwa kufanyiwa upasuaji, baada ya kufanyiwa vipimo kwa kutumia vifaa vya kisasa.