22/05/2026
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Lameck Nchemba, anatarajiwa kuendelea na ziara yake mkoani Iringa kuanzia Mei 23 hadi 24, 2026, kwa lengo la kukagua miradi ya maendeleo, kuzungumza na wananchi pamoja na kusikiliza kero mbalimbali zinazowakabili wananchi wa mkoa huo.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa Mhe.Kheri James amesema Waziri Mkuu atatembelea wilaya mbili ambazo ni Wilaya ya Iringa na Wilaya ya Kilolo,akisema kuwa Mei 23 Waziri Mkuu atakuwa katika eneo la Kichangani, Manispaa ya Iringa, huku Mei 24 akitarajiwa kuzungumza na wananchi katika eneo la stendi ya Kilolo.
Mkuu huyo wa Mkoa amewaomba wananchi wa wilaya hizo mbili kujitokeza kwa wingi kushiriki katika mikutano hiyo ili kupata nafasi ya kusikiliza maelekezo mbalimbali kutoka kwa Waziri Mkuu, yatakayochochea maendeleo na ustawi wa Taifa.
Katika ziara hiyo, Waziri Mkuu pia anatarajiwa kutembelea mradi wa Barabara ya Mchepuko wa Iringa (Iringa Bypass), ambao ni miongoni mwa miradi ya kimkakati inayotekelezwa mkoani humo chini ya usimamizi wa Wakala wa Barabara Tanzania yaani ''Tanzania National Roads Agency'' (TANROADS).
Aidha, akiwa wilayani Kilolo , Waziri Mkuu atakagua mradi wa barabara ya IpogoloโKilolo, ambao unaelezwa kuwa kiungo muhimu cha biashara, uchumi na shughuli za kijamii kati ya Wilaya ya Iringa na Kilolo.
Ziara ya Waziri Mkuu mkoani Iringa inatarajiwa kuleta chachu mpya ya maendeleo kwa wananchi kupitia ukaguzi wa miradi mbalimbali pamoja na kusikiliza changamoto zinazowakabili wananchi moja kwa moja.