04/06/2026
SAMIA AWAKUMBUKA LUMUMBA NA NYERERE
RAIS Dkt. Samia Suluhu Hassan amesifu mchango wa Chuo Kikuu cha Urafiki cha Watu wa Urusi (RUDN) katika ukombozi wa nchi za Afrika akisema kimesadifu maono ya viongozi wa zama za ukombozi wa Bara la Afrika.
Rais Samia ameyasema hayo jijini Moscow, Urusi wakati wa tukio la kutunukiwa kwake Shahada ya Heshima ya Uzamivu (Honoris Causa) na chuo hicho kutokana na uongozi uliotukuka na mchango wake katika maendeleo ya taifa.
Akizungumza mara baada ya kupewa heshima hiyo, Rais Samia alisema amepokea shahada hiyo kwa unyenyekevu mkubwa ukizingatia historia kubwa ya chuo hicho katika kipindi cha miaka 60 iliyopita.
“Jina la Patrice Lumumba ambalo chuo hiki kilipewa kilisadifu jukumu kubwa ambalo mwanamapinduzi huyo wa Afrika na viongozi wenzake wa Afrika waliona k**a wajibu mkubwa wa uongozi.
“Kwamba elimu inatakiwa isiwe tu kuingia darasani bali ni mlango wa ukombozi, utu, maendeleo na uhusiano wa kuheshimiana. Historia ya chuo hicho imesadifu maono yao na kwa hakika heshima waliyonipa ni kubwa” alisema.
RUDN imekuwa na mahusiano ya muda mrefu na Tanzania, kikiwa kimesomesha zaidi ya Watanzania 1,100 tangu kianzishwe mwaka 1960 iliyopita na sasa wanafunzi wa Kitanzania 72 wanapata mafunzo katika ngazi mbalimbali chuoni hapo.
Rais Samia anakuwa Rais wa karibuni zaidi kupewa heshima hiyo na chuo hicho, huku marais wengine sita wakiwa wamewahi kupewa tuzo hiyo. Baadhi ya marais hao ni Sam Nujoma wa Namibia, Thabo Mbeki wa Afrika Kusini na Olesegun Obasanjo wa Nigeria.
Vyuo vikuu vingine saba ambavyo vimewahi kumtunukia Rais Samia shahada za namna hiyo ni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Jawahral Nehru nchini India, Chuo Kikuu cha Ankara nchini Uturuki, Nasarawa nchini Nigeria, Chuo Kikuu cha Anga cha Korea Kusini, Chuo Kikuu cha Mzumbe na Chuo Kikuu cha Zanzibar (SUZA).
Rais Samia yuko nchini Urusi katika ziara ya kitaifa iliyoanza jana na itahitimishwa kesho baada ya kuhudhuria Mkutano wa Kimataifa wa Uchumi wa St. Peterburg nchini hapa.