Wasafi FM

Wasafi FM The leading radio station in Tanzania specializing in the latest music & entertainment news.
(1)

17/01/2026

Mkuu wa Utumishi wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania Meja Jenerali Marco Gaguti amewataka Kuruti kuzingatia mafunzo waliyoyapata kwa nadharia na vitendo, na kusema kuwa zoezi la EX- MALIZA limefanikiwa kwa kiasi kikubwa.

Kabla ya kufunga rasmi Zoezi la Medani la EX-MALIZA lililohusisha Kuruti wa Kundi la 44/2025, Meja Jenerali Gaguti amesema Mazoezi ya Medani na mafunzo ya kijeshi ndio Msingi wa JWTZ na kuongeza kuwa dhamira ya JWTZ ni kuona kuruti wote wanamaliza na kuhitimu Mafunzo.

Naye mkuu wa Shule ya Mafunzo ya awali ya Kijeshi RTS Kihangaiko Brigedia Jenerali Sijaona Michael Myalla amesema, wanafunzi wa kozi ya Kuruti kundi la 44/2025 wameonyesha uwezo wa kukabiliana na adui muda wote wa zoezi.

@

17/01/2026

MGOMO WA WAFANYAKAZI KIWANDANI ARUSHA DC ATOA MAAGIZO MATANO

Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Joseph Mkude, ametoa maagizo matano yakiwemo kuundwa kwa tume maalumu ya kushughulikia na kutatua malalamiko ya wafanyakazi wa kiwanda cha kuchakata chuma na kutengeneza nondo cha Lodhia kilichopo mkoani Arusha. Hatua hiyo imechukuliwa kufuatia mgomo wa wafanyakazi wa kiwanda hicho uliotokana na changamoto mbalimbali ikiwemo madai ya mshahara.

Akizungumza na viongozi na wafanyakazi wa kiwanda hicho, Mkude amesema tume hiyo inatarajiwa kuanza kazi mara moja na ndani ya wiki mbili itawasilisha majibu na suluhisho la changamoto zinazowakabili wafanyakazi. Aidha, amewataka wafanyakazi kurejea kazini na kiwanda kuendelea na shughuli za uzalishaji.

Kwa upande wake, Afisa Kazi wa Mkoa wa Arusha, Deusdatus Munishi, amesema kima cha chini cha mshahara kinachotangazwa na serikali hutofautiana kulingana na sekta husika, akisisitiza umuhimu wa kufuata miongozo ya kisheria.

17/01/2026

WADAU WAOMBA ELIMU TOZO ZA HAKIMILIKI IONGEZWE, COSOTA WAFAFANUA

Wadau wa sanaa wakiwemo Sanaa za ufundi na kazi za maandishi, wachoraji na wachonga vinyago wameiomba serikali kuwapa kipaumbele katika fursa mbalimbali zinazowahusu, ikiwemo kushirikishwa katika makongamano mbalimbali na kupewa elimu ya mambo kadhaa yanayoweza kuwanufaisha ikiwemo elimu ya mirabaha.

Wadau hao wametoa maombi hayo ikiwa ni Siku chache baada ya serikali kuridhia kuanza kwa utekelezaji wa tozo mpya ya hakimiliki nchini, ambapo Taasisi ya Hakimiliki Tanzania (COSOTA) inajiandaa kugawa mrahaba wa kwanza, unaotokana na tozo ya asilimia 1.5 ya thamani ya vifaa vinavyotumika katika kuzalisha, kuhifadhi na kusambaza kazi za sanaa na kazi za maandishi nchini, inayotozwa wakati wa uingizwaji au uzalishaji wa vifaa hivyo ambavyi ni pamoja na DVD, Recorder, Radio zinazorekodi na Televisheni zinazorekodi.

Akizungumza kuhusu Tozo hizo za Hakimiliki, Afisa wa Hakimiliki kutoka Ofisi ya Hakimiliki Tanzania (COSOTA) Judith Komba, amesema kwa mujibu wa Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki, fedha hizo takribani bilioni 1 zilizokusanywa, zinazotarajiwa kugawiwa kwa makundi hayo, zinatajwa kuwa zitawanufaisha wabunifu wa makundi yote, Kuanzia muziki, filamu, Sanaa za ufundi na kazi za maandishi, ambapo Hatua hii inatajwa kuwa mkombozi wa kiuchumi kwa wasanii, k**a ambavyo anafafanua Afisa wa Hakimiliki kutoka Ofisi ya Hakimiliki Tanzania (COSOTA) Judith Komba.

Amesema kuwa licha ya kuwa ni mara ya kwanza kwa Tanzania kuanza kutoza tozo hiyo ya hakimiliki, si jambo geni kwa baadhi ya nchi nyingine za Afrika ambapo Kenya, Malawi, Morocco naTunisia ni baadhi ya nchi ambazo zimekuwa zikitoza tozo hizo.


17/01/2026

ZAIDI YA WANAFUNZI 1500 SHULE YA MALAMA HATARINI KUKUMBWA NA MAGONJWA YA MLIPUKO

Zaidi ya wanafunzi 1500 wa shule ya sekondari Malama iliyopo katika Mamlaka ya Mji mdogo wa Mbalizi mkoani Mbeya, wako hatarini kukumbwa na magonjwa ya mlipuko kutokana na kutumia miundombinu haba na mibovu ya vyoo.

Mwalimu Neema Mwakimenya ni Mkuu wa Shule hiyo anasema Malama Sekondari ina upungufu wa matundu 16 ya vyoo kwa upande wa wavulana, nakwamba miundombinu ya vyoo vinavyotumika kwa sasa haviko kwenye hali nzuri huku wazazi wakieleza hofu yao kiafya kwa watoto.

Ili kuinusuru hali hiyo mjumbe wa halmashauri kuu ya chama cha mapinduzi CCM Taifa anayewakilisha mkoa wa Mbeya Ndg. Ndele Mwaselela ametoa fedha na kuelekeza kuanza ujenzi wa vyoo vya shule hiyo haraka kuanzia wiki ijayo na kukamilisha ndani ya wiki moja ikienda sambamba na kukamilisha vyoo vilivyoanza kujengwa shuleni hapo kwaajili ya wavulana.

Wakati huo huo shule hiyo imepokea madawati 200 ili kupunguza mzigo kwa wazazi kuchangia shilingi elfu hamsini kwakila mmoja kwaajili hiyo kutokana na upungufu wa madawati zaidi ya 600, uliokuwepo hapo awali.

Cc

17/01/2026

HUU HAPA MWAROBAINI WA AJALI NA WIZI WA MIZIGO MLIMA NYOKA

Baada ya kuripotiwa kwa matukio mbalimbali ya ajali na uwepo wa wizi wa mizigo kwemye magari makubwa yanapo pandisha eneo la mlima nyoka jijini Mbeya, serikali imeanza upanuzi wa barabara eneo hilo unaoenda sambamba na ujenzi wa kituo cha ukaguzi wa magari ili kuongeza usalama na kuondoa msongamano jijini Mbeya.

Meneja wa Barabara kuu na barabara za mijini Nchini kutoka wakala ya barabara Tanzania (TANROADS) Mhandisi Nchama Wambura amesema kumekua na adha kubwa ya magari yanayo beba mizigo kutoka mkoani Dar es Salaam kwenda nchi jirani kupitia Tunduma, na sasa imekua na mzigo mkubwa hivyo upanuzi utasaidia kupata maeneo ya kupunzikia na ukaguzi kwenye eneo hilo.

Mhandisi Suleiman Bishanga ni meneja wa Wakala Ya barabara Nchini (TANROADS) mkoa wa Mbeya, amesema kupitia upanuzi huo wanakwenda kuongeza hali ya usalama kwenye eneo la mlima nyoka mlima ambao ni mrefu kwa magari ya mizigo kutumia muda mrefu kupandisha, huku akiwatoa hofu wananchi juu utekelezaji wa miradi mingine ikiwemo ujenzi wa barabara njia nne kuanzia Nsalaga hadi ifisi.

Itakumbukwa kwamba kwa nyakati tofauti Wasafi Media imeripoti matukio ya madereva kulalamika kuibiwa mizigo wakati wa kupanda mlima nyoka hasa nyakati za usiku na kuomba kuongezwa kwa ulinzi hatua ambazo tayari zimeanza kuchukuliwa na serikali kwa kupanua barabara, huku chief wa kabila la wasafwa akieleza kwanini eneo hilo limekua na jina la mlima nyoka.

Cc

17/01/2026

From - 🎵

Rate it From 1 to 10

16/01/2026

WASAFI YAMFUNGULIA MLANGO WA TABASAMU, WADAU WAJITOKEZA

Siku chache baada ya kujifungua pacha wanne katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji Korogwe Magunga, Mariam Shemaheze (26) na Kufikisha Jumla ya watoto saba, mkazi wa Kijiji cha Kwamatuku wilayani Handeni mkoani Tanga, ameanza kupokea msaada wa vifaa muhimu vya watoto kutoka kwa wadau mbalimbali.

Mariam alieleza awali kuwa hali ya kulea watoto hao wanne ilikuwa changamoto kubwa, na hivyo kuomba wananchi na wadau kujitokeza kumshika mkono kupitia namba ya Simu 0650957438 jina Miraji Mzuka Bakari

Akizungumza na Wasafi Media wakati wa kupokea baadhi ya msaada huo, Mariam ameishukuru Taasisi ya Binti Asimame kwa kujitokeza na kumpatia mahitaji muhimu ya watoto wake, huku akiwaomba wadau wengine kuendelea kumuunga mkono.

Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Halmashauri ya Mji Korogwe Magunga, Dkt. Yohana Peniel, amewapongeza wadau wote waliojitokeza kumsaidia mama huyo, akisema msaada huo ni ishara ya mshik**ano wa jamii na upendo kwa mama na watoto wachanga. Ameongeza kuwa wadau wengine bado wana nafasi ya kusaidia familia hiyo kwa namna mbalimbali.

Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Binti Asimame, Asha Maumba, ambaye ni miongoni mwa wadau waliojitokeza, amesema walipopata taarifa za Mariam kujifungua pacha wanne waliona ni baraka kubwa, lakini pia changamoto inayohitaji msaada wa haraka. Amesema taasisi yao imekabidhi nguo za watoto, pampasi, taulo, mafuta ya kupaka pamoja na mahitaji mengine ya msingi.

Asha ametoa wito kwa wadau wengine, taasisi na watu binafsi kujitokeza kuisaidia familia hiyo ili kuhakikisha watoto hao wanapata malezi bora na afya njema.

Cc

16/01/2026

VIJANA WASHAURI NCHI IWEKE MSUKUMO ELIMU YA UWEKEZAJI WA NDANI | WATAKA 50% YA MIRADI IMILIKIWE NA WATANZANIA KWA 100%

Serikali imeshauriwa kuongeza wigo wa Elimu ya uwekezaji itakayowashawishi Wazawa kufanya Uwekezaji wa ndani ya Nchi, na kuinua Uchumi wa Mtanzania wa kipato cha Kawaida na Kati, kupitia fursa ambazo zitapatikana kwenye uwekezaji huo.

Hayo yamesemwa Leo January 16 na baadhi ya wakazi wa Jiji la Dar es salaam walipozungumza na Wasafi Digital kufuatia Serikali kupitia Wizara ya Mipango na Uwekezaji kuzindua kampeni ya Kitaifa ikilenga kuhamasisha Uwekezaji wa ndani.

Kampeni hiyo imezinduliwa na Waziri wa Nchi ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo ambaye amesema mpango huo unalenga kutoa Elimu ya uwekezaji nchini ili kubadili mtazamo wa Watanzania wengi wanaoamini uwekezaji ni lazima ufanywe na watu kutoka nje ya Tanzania.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa 'TISEZA' Gilead Teri amesema k**a Taasisi ambayo inayosimamia uwekezaji lengo ni miradi ya uwekezaji inayosajiliwa mwaka huu angalau asilimia 50 imilikiwe na Watanzania Kwa asilimia mia Moja.


16/01/2026

WAFANYAKAZI KIWANDA CHA LODHIA ARUSHA WAGOMA WADAI NYONGEZA YA MSHAHARA

Wafanyakazi wa Kiwanda cha kuchakata chuma na kuzalisha nondo cha Lodhia kilichopo mkoani Arusha wamegoma kufanya kazi wakidai nyongeza ya mshahara, wakisema hatua hiyo inapaswa kutekelezwa kulingana na tangazo la Serikali lililotolewa mwishoni mwa mwaka jana kupitia wizara ya Ajira.

Wakiwa wamekusanyika kwa wingi nje ya geti la kiwanda hicho, wafanyakazi hao wameonekana wakipaza sauti wakisema “tunataka haki yetu, tunataka nyongeza ya mshahara”, wakisisitiza kuwa mishahara yao ya sasa haiendani na gharama za maisha.

Serikali imefika eneo la tukio na kuwatuliza wafanyakazi hao huku ikiahidi kushughulikia na kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa mgogoro huo kati ya uongozi wa kiwanda na wafanyakazi.

Akizungumza kuhusu mgomo huo Kwa njia ya Simu, Mwenyekiti wa Makampuni ya Lodhia Group, Harun Lodhia, amesema uongozi uko tayari kuketi meza moja na wafanyakazi ili kumaliza suala hilo kwa mazungumzo. Hata hivyo, ameonya kuwa endapo hali itaendelea kuwa mbaya, uongozi unaweza kulazimika kukifunga kiwanda hicho, akieleza kuwa kwa sasa uzalishaji umekuwa mdogo.

16/01/2026

VIJANA WATIA NENO MAAMUZI YA SERIKALI KWA VIJANA 5,746

Baadhi ya vijana wametoa maoni Yao juu ya maamuzi ya Serikali kuwachagua vijana 5,746 kati ya 20,247 ili kujiunga katika mafunzo ya uanagenzi kwa kipindi cha miezi nane.

Wakizungumza na Wasafi Media Kwa nyakati tofauti vijana hao ni Samira Nestory na Jofrey Kasia ambapo wameelezea matumaini yao kutokana na fursa zinazotolewa na serikali ya kuwajengea mahusiano mazuri kati yao.



Kwa upande wake waziri wa nchi ofisi ya waziri mkuu kazi ajira na mahusiano Mhe. Deus Sangu amesema serikali itafadhili mafunzo hayo kwa asilimia 100.

Mhe. Sangu amesema hayo Leo Jan 16,2026 Jijini Dodoma wakati wakati Akitangaza nafasi Kwa Waandishi wa Habari



“Napenda kusisitiza kuwa mafunzo hayo yanayotarajiwa kuanza januari 19 mwaka huu kupitia vyuo 47 vilivyoomba, yanafadhiliwa na serikali"amesema Mhe. Deus Sangu

Aidha Sangu imetoa wito kwa vyuo vilivyopata fursa ya kuwafundisha vijana hao kuhakikisha wanawasimamia katika kipindi chote cha mafunzo yao.

Cc:

16/01/2026

WANANCHI WA IBINZAMATA NA MWASELE WAONDOKANA NA ADHA YA KIVUKO

Kufuatia ripoti ya Wasafi Media iliyoibua changamoto ya kukosekana kwa kivuko cha waenda kwa miguu kinachounganisha kata za Masekelo na Ibinzamata katika Manispaa ya Shinyanga, wananchi wa kata hizo wameondokana na adha waliyoikuwa wakikumbana nayo baada ya kujengwa kwa kivuko katika Mto Kidalu.

Wakizungumza na Wasafi Media, wananchi wamesema hapo awali walikuwa wakikumbana na hofu kubwa ya usalama wa maisha yao kila walipolazimika kuvuka mto huo, hususan katika kipindi cha mvua ambapo maji hujaa na mkondo kuwa mkali, hali iliyokuwa ikihatarisha maisha yao, ikiwemo watoto na wazee.

Kukamilika kwa ujenzi wa kivuko hicho kumeleta faraja kubwa kwa wananchi hatua inayotarajiwa kuchochea maendeleo kwa kuimarisha shughuli mbalimbali za kiuchumi, ikiwemo usafirishaji wa abiria na mizigo K**a wanavyozungumza baadhi ya maafisa usafirishaji maarufu k**a boda 5boda jinsi kivuko hicho kinavyosaidia kuongeza usalama pamoja na kipato chao cha kila siku.

Akizungumza kuhusu mradi huo, Meneja wa Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) Wilaya ya Shinyanga, Mhandisi Samson Pamphili, amesema ujenzi wa kivuko hicho umegharimu kiasi cha fedha kilichotolewa na serikali kupitia TARURA, na kusisitiza kuwa daraja hilo limejengwa kwa viwango vinavyohakikisha usalama wa wananchi wanaolitumia, hususan wakati wa msimu wa mvua.

Aidha, Meneja wa TARURA Wilaya ya Shinyanga, Mhandisi Samson Pamphilio, amepiga marufuku madereva wa magari kuendelea kutumia kivuko hicho, akisema hatua hiyo imekuwa ikisababisha uharibifu wa miundombinu hiyo. nakufafanua kuwa kivuko hicho kimejengwa mahsusi kwa matumizi ya watembea kwa miguu, waendesha baiskeli, pikipiki pamoja na bajaji pekee, na si kwa magari makubwa.

Cc

16/01/2026

DOTO ASHIKILIWA KWA TUHUMA ZA MAUAJI YA WATOTO WA TATU WA FAMILIA MOJA

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linamshikilia Doto Lubongeja, mkazi wa Madundasi Wilayani Mbarali Mkoa wa Mbeya kwa tuhuma za mauaji ya watoto watatu wa familia moja kwa kuwanyonga shingo na kuiba ng’ombe 15 walizokuwa wakichunga watoto hao, kisha kuzificha nyumbani kwa Mjomba wake aitwaye Masoda K***a anayeishi Kijiji cha Madundasi “B”

Taarifa iliyotoleaa na k**anda wa polisi mkoa wa Mbeya Kamishna msaidizi mwandamizi wa polisi Benjamini Kuzaga imeeleza kwamba Tukio hilo limetokea Januari 15, 2026 katika Kijiji cha Madundasi, ambapo mtuhumiwa aliwaua watoto baada ya kuwakuta peke yao wakichunga ng’ombe eneo la jirani na nyumbani kwao, Watoto waliouwawa ni Petro Amosi, miaka 08, Samu Amosi, miaka 06 na Nkamba Amosi, miaka 04 wote wakazi wa Kijiji cha Madundasi.

Kufuatia tukio hilo, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kupitia Askari wa kuchunguza matukio ya mauaji, walianza msako mkali na kufanikiwa kumk**ata mtuhumiwa Doto Lubongeja pamoja na mtuhumiwa mwingine aitwaye Masoda K***a ambaye walishirikiana kuuza ng’ombe hao ambapo Askari hao walifanikiwa kuwapata Ng’ombe wote 15 waliokuwa wameibwa pamoja na fedha taslimu kiasi cha shilingi 5,100,000/= zilizopatikana baada ya kuuzwa kwa ng’ombe hao.

Uchunguzi wa awali umebaini kuwa chanzo cha tukio hilo ni tamaa ya kujipatia mali kwa njia isiyo halali Upelelezi unakamilishwa ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi ya watuhumiwa.

Cc

Address

Mbezi Beach
Dar Es Salaam

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Wasafi FM posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Share

Category