11/06/2026
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, ameendelea na ziara ya kukagua miradi ya maendeleo katika Wilaya ya Kigamboni, ambapo leo alifika Kata ya Vijibweni kujionea changamoto ya ubovu wa barabara inayowakabili wakazi wa eneo hilo.
Akizungumza katika ziara hiyo, Chalamila alisema Serikali inatambua adha wanayopata wananchi na inaendelea kutafuta suluhisho la kudumu. Alieleza kuwa zaidi ya nyumba 300 zinatarajiwa kupisha ujenzi wa Barabara ya Soweto, huku akisisitiza kuwa zoezi hilo litafanyika kwa kuzingatia sheria, taratibu na maslahi ya wananchi.
Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa alimpa tahadhari mkandarasi wa mradi huo kuwa tayari kuanza utekelezaji mara baada ya mvua kupungua jijini Dar es Salaam. Alisema wananchi wamechoshwa na kuchelewa kwa mradi huo na hawatakuwa tayari kuvumilia ucheleweshaji zaidi.
Chalamila aliwataka wananchi kuwa na subira na kuendelea kuiamini Serikali, akiahidi kuwa maeneo yote yenye changamoto yatapatiwa ufumbuzi baada ya msimu wa mvua ili kuboresha huduma za usafiri na kuchochea maendeleo.
Kwa upande wao, wananchi wa eneo la Soweto walisema ubovu wa barabara hiyo umekuwa kero ya muda mrefu. Walidai kuwa mara nyingi matengenezo hufanyika kwa muda mfupi wakati wa ziara za viongozi, lakini husimama punde baada ya ziara hizo kumalizika.