14/09/2025
MTIKISIKO WA HIRIZI
SEHEMU YA 2
Kwa hesabu ya muuzaji, hata k**a angeuza mavazi hayo kwa shilingi 12,000 bado angekuwa na faida. Isitoshe, hakuwa ameuza hata nguo moja katika nguo hizo tangu alipozileta kiasi cha mwezi mmoja uliopita. Hivyo, hakuwa na sababu ya kukataa.
“Leta pesa.”
Muda mfupi baadaye Shaka alikuwa katika mwonekano tofauti. Alitumia chini ya dakika mbili kuvaa zile nguo za uraiani juu ya mavazi ya jela huku yule muuzaji akiwa amepigwa butwaa.
Bado Shaka hakuwa amehitimisha kilichomleta humo. Akaendelea kuangaza huku na kule. Macho yakagota sehemu ambayo kulitundikwa visu vya aina mbalimbali na vya ukubwa uliotofautiana.
“Kile kisu bei gani?”
“Alfu mbili na mia tano.”
“Nipe.”
Kisu kikatua mfukoni mwake. Akatoka hapo kwa mwendo wake uleule, mwendo wa taratibu na wa kujiamini. Na sasa hakutaka kuchelewa katika eneo hilo, alikodi teksi iliyomfikisha Magomeni Kondoa ambako alipata chumba katika gesti moja isiyokuwa na hadhi.
Mara tu alipokwishaingia chumbani na kujifungia, alizivua zile sare za jela na kuzifutika chini ya kitanda. Akabaki na zile nguo mpya pekee. Kisha akatoka na kwenda dukani ambako alinunua lita moja ya mafuta ya taa na kurejea pale gesti.
“Nionyeshe sehemu ya kuweza kuchomea makabrasha nisiyoyahitaji,” alimwambia mhudumu wa gesti.
Mhudumu huyo, akiwa hajui hili wala lile, alimwonesha sehemu kulikokuwa na shimo dogo lililotumika kwa kutupia taka. Shaka aliporudi chumbani alizitwaa zile nguo za jela, zilizokuwa ndani ya fuko la nailoni, akatokanazo hadi huko shimoni ambako alizimwagia mafuta na kuzitia moto.
Alirudi chumbani mwake baada ya kuhakikisha kuwa zile nguo zote za jela zimeteketea.
ASKARI jela aliyesimamia kundi la wafungwa waliopaswa kwenda Viwanja vya Maonesho, aliendelea kuduwaa huku akimtazama Shaka aliyekuwa akiyoyoma taratibu machoni pake. Huenda alipaswa kuchukua hatua pale tu Shaka alipokaidi amri ya kuingia garini, lakini hakufanya hivyo. Na alipokuja kuzinduka, Shaka alikuwa ameshatokomea machoni pake.
Akakurupuka kupuliza filimbi. Eneo hilo lote likazingirwa na askari, na wengine wakamwagwa mitaani kumsaka mfungwa aliyetoroka katika mazingira ya kutatanisha.
Pamoja na msaada wa raia wema waliowaonesha njia alizopita mtu aliyekuwa amevaa nguo zilizoshabihiana kwa kila kitu na sare za wafungwa wa jela, na pamoja na mwanamke muuza duka kuthibitisha kufikiwa na mteja aliyevaa sare za jela na kuongeza kuwa mteja huyo alinunua nguo mpya na kuzivalia humohumo dukani, juu ya mavazi ya jela, bado haukuwa msaada ulioweza kutoa matunda mema.
Shaka hakuonekana, japo msako mkali uliendelea takriban kitongoji chote cha Keko.
Naam, kilikuwa ni kizungumkuti cha aina yake!
AKITAMBUA fika kuwa lazima msako mkali dhidi yake ungefanyika, Shaka hakutoka nje ya gesti hiyo siku nzima. Njaa ilipomsak**a alimtuma chipsi mhudumu wa gesti. Koo lilipomkauka aliagiza bia. Kwa jumla alihakikisha hafanyi kosa atakalolijutia baadaye. Japo aliamini kuwa kwa ‘nguvu’ za baba yake, Mzee Songoro, asingepatwa na baya lolote, hata hivyo aliamua kuwa makini.
Usiku ulipoingia alihitaji faraja ya mwanamke. Ndiyo, usiku kucha awe na mwanamke mrembo, mwanamke anayeyajua majukumu yake pale anapokumbana na mwanamume mwenye njaa ya mwanamke.
Bia tano zilizosambaa katika mishipa yake ya damu zilimpa mhemuko kiasi cha kuamua kuzungumza kiutu uzima na mhudumu mmoja wa k**e wa gesti hiyo, mazungumzo yaliyoanzia kwa ‘gia’ ndogo tu, bia mbili, chipsi-kuku na shilingi 10,000.
Usiku huo ukawa wao. Wakakesha wakizungumza kwa furaha, wakanywa kwa kujidai na wakaikanda miili yao kwa fahari, wakifanya kila walichopenda kukifanya, na wakafanya kwa namna ya kipekee kiasi cha kujikuta kukipambazuka huku kila mmoja bado akimhitaji mwenzie.
Hata hivyo, Shaka hakuwa limbukeni wa mapenzi. Kwa siku hii, zikiwa ni saa zisizozidi ishirini na nne tangu alipotoroka gerezani, aliamua kuwa makini zaidi na kuzitumia fedha zake chache alizonazo kwa uangalifu ili awe na uhakika wa kuliacha jiji hilo na aweze kufika mwisho wa safari yake.
Akiwa bado kitandani, mkono wake mmoja ukilipapasa paja la Rukia, alikuwa akiwaza hili na lile kuhusu ratiba yake ya siku hiyo huku pia akifikiria ni hatua gani ambayo askari watakuwa wameichukua baada ya kutoroka gerezani jana katika mazingira ya kutatanisha.
Aliamini kuwa kwa vyovyote vile nguvu ya msako dhidi yake itakuwa kubwa na ikiambatana na hasira kali kutoka kwa hao askari. Kwa kiasi fulani itachukuliwa kuwa amelidhalilisha Jeshi la Magereza.
Itakuwa ni habari kubwa kwa vyombo mbalimbali vya habari hususan vile vyenye sera ya kuishambulia serikali kwa dosari yoyote itakayojitokeza katika taasisi zake. Itakuwa ni kashfa kwa Jeshi la Magereza. Kwa hali hiyo alipaswa kuwa makini zaidi katika muda atakaokuwa jijini Dar es Salaam.
Alipaswa kuchukua tahadhari kubwa!
Ni Rukia aliyemwingilia katika fikra zake. “Vipi, mpenzi, na jioni tutakuwa wote?” alimuuliza..
HII SEHEMU YA PILI HAIJAFIKA MWISHO K**A UNAITAJI MWENDELEZO WA SEHEMU HII YA PILI TUTAFUTE :-
1) whatsapp tukuunge kwenye channel ya FULL STORY Bonyeza link hii👉👇
wa.me/qr/XEAQUXEYQNCEB1 TUKUUNGE KWENYE CHANNEL YETU
2) Jiunge na channel yetu ya bure kwa kubonyeza link hii 👉 whatsapp.com/channel/0029VbB2NaAA2pLGdeJDzo29
3) Tufollow kwenye page yetu ya clubzila kwa kubonyeza link hii 👉 clubzila.com/STORY?ref=11084 upate simulizi kali