14/09/2025
Mgombea wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Mkoa wa Kigoma ni miongoni mwa mikoa ya kimkakati nchini na ameahidi kuusimamia k**a kitovu cha biashara na uwekezaji endapo ataaminiwa kuongoza baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.
Akizungumza leo Jumapili Septemba 14, 2025, katika viwanja vya Katosho, Kigoma Mjini, Dkt. Samia amesema serikali ya awamu ya sita imejidhatiti kuunganisha Kigoma kwa njia zote kuu za usafirishaji- reli, anga, barabara na maji ili kuhakikisha uchumi wa mkoa huo unakua kwa kasi na kufunguka kwa fursa nyingi za uwekezaji.
โKigoma hii ya sasa siyo mwisho wa reli, ni kitovu cha biashara na maendeleo. Na ili kufikia lengo hilo, kwenye miundombinu ya usafiri na usafirishaji, ambao ndio muhimili mkubwa wa kukuza uchumi, tumejidhatiti kuunganisha mkoa huu kwa njia zote. Tayari maboresho ya uwanja wa ndege yanaendelea na jengo la abiria linaendelea kujengwa,โ amesema Dkt. Samia.
Kuhusu sekta ya usafiri wa reli, Dkt. Samia amesema ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) kutoka Tabora hadi Kigoma utaunganisha pia Tanzania na mataifa jirani ya Burundi na mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Sambamba na hilo, serikali inaendelea na maboresho ya reli ya zamani ya MGR, ikiwemo ununuzi wa vichwa vitatu vipya vya treni, mabehewa 22 ya abiria na 44 ya mizigo, pamoja na ukarabati wa mabehewa 350 ya mizigo na 33 ya abiria. Pia, mabehewa maalumu ya kuhifadhi baridi yatanunuliwa ili kuwezesha usafirishaji wa mbogamboga na matunda.