15/07/2026
Watu watatu wamefariki dunia na wengine wawili kujeruhiwa kufuatia ajali ya barabarani iliyohusisha magari mawili kugongana uso kwa uso katika barabara ya Handeni-Korogwe, eneo la Kata ya Sindeni, Tarafa ya Mzundu, Wilaya ya Handeni mkoani Tanga.
Ajali hiyo ilitokea usiku wa Julai 14, 2026 majira ya saa 4:30 usiku, kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga.
Kwa mujibu wa Polisi, ajali hiyo ilihusisha gari lenye namba za usajili T.712 ABH aina ya Mitsubishi Fuso lililokuwa likitoka Handeni kuelekea Korogwe na gari lenye namba za usajili T.519 EMM aina ya Eicher lililokuwa likitoka Korogwe kuelekea Handeni.
Waliopoteza maisha ni madereva wa magari hayo mawili ambao ni Yahaya Miraji (28), mkazi wa Handeni, na Japhary Ramadhan maarufu Ally (47), mkazi wa Tanga, pamoja na mwanaume mwingine mwenye umri unaokadiriwa kuwa kati ya miaka 46 na 50 ambaye bado hajafahamika.
Aidha, watu wawili ambao ni Chenga Herbet (55) na Salama Ally (56), wote wakazi wa Muheza, walijeruhiwa katika ajali hiyo na wamelazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Handeni wakipatiwa matibabu.
Uchunguzi wa awali wa Jeshi la Polisi umebaini kuwa chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi uliosababisha madereva kushindwa kuyamudu magari yao na hatimaye kugongana uso kwa uso, huku miili ya marehemu ikihifadhiwa hospitalini kwa ajili ya uchunguzi na taratibu nyingine za kisheria.