21/05/2026
Mbunge wa Jimbo la Msalala Mabula Magangila ameitaka Serikali kufikiria upya matumizi ya bandari kavu ikiwemo Bandari ya Isaka wilayani Kahama, akisema matumizi makubwa ya malori kusafirisha mizigo kwenda na kutoka nchi jirani yanaendelea kuharibu barabara huku Serikali ikitumia mabilioni ya fedha kwenye matengenezo.
Akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha 2026/27, Magangila amesema hakuna sababu ya malori kutoka nchi za Rwanda, Burundi, Congo DRC na Uganda kufuata mizigo hadi Dar es Salaam wakati mizigo hiyo inaweza kusafirishwa kwa reli kupitia bandari kavu ya Isaka.
“Ni kitu gani kinatusababisha mizigo yetu yote ya transit ambayo inakwenda Rwanda, Burundi, Congo DRC na Uganda kwanini maroli yanaifuata Dar es Salaam wakati tuna bandari kavu ya Isaka na ilishawahi kuwa hivyo huko nyuma? Kwanini tunaendelea kutumia gharama kubwa ya matengenezo ya barabara kipande hiki? Reli ya kati inapita pale, SGR inapita hapo kwanini Serikali haifikirii kupunguza mzigo kwa kuanza kutumia bandari kavu ya Isaka? Hivi kweli magari kutoka Rwanda, Burundi, Congo DRC na Uganda yanafuata nini Dar es Salaam?” Mabula Magangila - Mbunge wa Jimbo la Msalala.
“Serikali chukueni mawazo yetu sisi vijana na sisi tuweze kuokoa hili taifa, mnufaike na wakati wetu wa sasa tukumie njia mbadala kuokoa gharama inayotumika kwenye matengenezo ya barabara zetu ili pesa tutakayo kwenda kuiokoa twende tukajenge mtandao mwingine wa lami kwenye barabara zetu nyingi ambazo sasa ni za changarawe,” amesema Magangila.