03/11/2023
Sekta ya Maji kupitia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) imekabidhi majengo ya vyoo kwa shule 11 pamoja na vituo vya afya vinne katika wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza kwa lengo la kuimarisha hali ya usafi wa mazingira katika taasisi hizo.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa MWAUWASA, Bi. Neli Msuya amekabidhi kwa Diwani wa Kata ya Ilemela, Wakili Willbard Kilenzi aliyepokea kwa niaba ya Mstahiki Meya wa Manispaa ya Ilemela, Mhe. Renatus Malungu.
Bi. Neli amesema hatua hiyo itaimarisha hali ya usafi wa mazingira katika taasisi hizo.
"Katika mradi huu wa vyoo tumeweka pia matenki ya maji hii itasaidia watumiaji kunawa mikono kwa majisafi na sabuni ili kulinda afya zao k**a muongozo wa afya unavyoelekeza pia kujiepusha na magonjwa yasababishwayo na uchafu,” Bi. Nelly amesema
Diwani wa Kata ya Ilemela, Wakili Willbard Kilenzi ameipongeza MWAUWASA kwa mradi huo ambapo amesema utakuwa msaada katika kuimarisha hali ya usafi wa mazingira katika taasisi hizo.
"Kwa niaba ya Manispaa ya Ilemela tunasema asante sana MWAUWASA kwa mradi huu wa vyoo pamoja na miradi mingine mnayoendelea kuitekeleza katika wilaya yetu, mmejenga vyoo hivi kwa ubora na tuwaahidi tutavitunza ili vidumu na kuendelea kuwa msaada kwa watumiaji," Wakili Kilenzi amesema.
Mradi huo umetekelezwa na MWAUWASA chini ya Mkandarasi kampuni ya M/s. URSINO LIMITED kwa fedha iliyotolewa na Serikali pamoja na Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD) kwa gharama ya shilingi bilion 2.26.
Mradi umetekelezwa kwa muda wa miezi 15 ukitarajiwa kunufaisha walimu na wanafunzi wapatao 14,233 katika shule za msingi za Nyamwilolela, Mhonze, Umoja, Mihama, Bugongwa, Chabusi, Sangabuye, Bugungumuki, Tumaini, Kabangaja pamoja na shule ya msingi Igombe.
Vituo vya Afya vilivyonufaika na mradi huo ni pamoja na kituo cha afya Karume, Sangabuye, Nyamwilolela pamoja na Lumala.