10/06/2026
‎Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anamringi Macha, ameupongeza Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kwa hatua yake ya kutoa mafunzo kwa waajiri, huku akiwataka washiriki kuhakikisha elimu hiyo inaleta tija na kukata mzizi wa urasimu kwa wastaafu katika maeneo yao ya kazi.
‎
‎
‎Macha ametoa pongezi na msisitizo huo mjini Bariadi Juni 10, 2026, wakati akifungua semina maalum ya waajiri iliyoandaliwa na PSSSF, iliyolenga kuwajengea uwezo maafisa wanaoshughulikia masuala ya wanachama mkoa wa Simiyu ili kuboresha utoaji wa huduma.
‎
‎Akizungumza juu ya maboresho ya huduma, Mkuu wa Mkoa alieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Dk. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imewekeza kwa kiasi kikubwa kwenye mifumo ya kidigitali na kusisitiza kuwa maafisa hao wanapaswa kutumia teknolojia hiyo kwa weledi ili kuondoa visingizio vinavyokwamisha na kuchelewesha huduma kwa wastaafu.
‎
‎
‎Ili kuhakikisha watumishi wanapata haki zao kwa wakati pindi wanapostaafu bila usumbufu.
‎
‎
‎Macha aliwaagiza waajiri wote mkoani Simiyu kuhakikisha kuwa michango ya watumishi inawasilishwa kwa wakati ili kuzuia changamoto ya mapengo ya michango.
‎
‎
‎Mkuu huyo wa mkoa alitoa onyo kwa watumishi wanaobadili majina kiholela wanapokaribia kustaafu, akibainisha kuwa jambo hilo linarudisha nyuma michakato ya kiserikali na kuongeza ugumu na kuleta ulazima wa kuwepo viapo vya ziada.
‎
‎
‎Katika kuunga mkono hitaji la kuwa na utendaji wenye tija na uadilifu, Mkuu wa Mkoa aliwakumbusha washiriki kuwa uzee haukwepeki, na kwamba maandalizi ya kustaafu salama yanategemea jinsi wanavyowatendea haki wastaafu wa sasa.
‎
‎
‎"Nawaasa washiriki kuachana kabisa na vitendo vya rushwa, hasa kwa hawa wazee ambao haki wanayoitafuta ni kwa ajili ya kuweza kujikimu na maisha yao yaliyosalia. Rushwa ya namna hii haiwezi kuwaacha salama wale walioipokea," alionya.
‎
‎
‎Kwa upande wake, Meneja wa PSSSF Mkoa wa Simiyu, Salumu Miraji, alimshukuru Mkuu wa Mkoa kwa utayari wake wa kuunga mkono juhudi za Mfuko na kufungua semina hiyo, huku akibainisha kuwa washiriki watapata elimu ya kina itakayowawezesha kuwaongezea ufanisi zaidi katika kuwahudumia wanachama na wastaafu.
‎
‎Miraji alisisitiza kuwa mafunzo hayo yatawafanya maafisa hao kuwa mabalozi wazuri wa PSSSF katika maeneo yao ya kazi, jambo ambalo litarahisisha utatuzi wa changamoto za wanachama na kusogeza huduma bora karibu zaidi na watumishi na wastaafu wa mkoa huo.
‎
‎Imeandikwa| Mwandishi Wetu
‎
‎Tembelea http://epaper.ippmedia.com kusoma gazeti lako au wasiliana nasi 📞+255 745 -700 710 au 0677- 020 701 kwa maelezo zaidi.
‎
‎
‎