06/06/2026
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) imeeleza kuridhishwa na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika Manispaa ya Temeke mkoani Dar es Salaam, ikisisitiza kuwa miradi hiyo inaonesha matumizi mazuri ya mapato ya ndani katika kuhudumia wananchi.
Kamati hiyo, ikiongozwa na Mwenyekiti wake Florent Kyombo, imekagua miradi minne ikiwemo ujenzi wa Shule ya Msingi Kibasila yenye thamani ya shilingi bilioni 4.4 na Shule ya Sekondari Kibondemaji inayojengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 7.
Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Kyombo amesema Kamati imevutiwa na matumizi ya majengo ya ghorofa ambayo yamesaidia kuongeza nafasi ya madarasa katika maeneo yenye uhaba wa ardhi mijini, hasa Jiji la Dar es Salaam.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Tumaini Nagu amesema maelekezo na ushauri wa Kamati umepokelewa na utekelezaji wake utaimarishwa ili kuhakikisha miradi inawanufaisha wananchi zaidi.