07/09/2026
Watumishi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini wamechangia fedha na kununua mashine ya kisasa ya kurudufu nyaraka (photocopy machine) kwa Shule ya Sekondari ya Sinde, Mbeya, ili kusaidia utayarishaji wa mitihani na kuondoa changamoto ya wanafunzi kufuata huduma hiyo nje ya shule.
Akikabidhi mashine hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali hiyo, Dkt. Godlove Mbwanji, amesema wameamua kuunga mkono sekta ya elimu kwa kuwa shule ndiko kunakotengenezwa wataalamu wa baadaye, wakiwemo madaktari na wauguzi. Mkuu wa Shule, Anatalia Valence Luwungo, ameshukuru msaada huo akisema utawanufaisha wanafunzi 1,196 na kuongeza ufanisi wa taaluma.
Wanafunzi Noel Sanga na Vanesa Kyando wamewashukuru watumishi hao, wakisema mashine hiyo itawachochea kuongeza bidii katika masomo na kuboresha ufaulu.