Fanani na Hadhira

Fanani na Hadhira Fanani atasimulia, na hadhira itasikiliza. Simulizi | Makala | Chambuzi | Vitabu

JENEZA LA TAIFA (Sura ya Saba)Mtunzi: Maundu Mwingizi Januari 3, 1998, ikiwa ni Jumamosi ya mwisho kabla ya likizo kumal...
09/09/2025

JENEZA LA TAIFA (Sura ya Saba)
Mtunzi: Maundu Mwingizi

Januari 3, 1998, ikiwa ni Jumamosi ya mwisho kabla ya likizo kumalizika na kurejea shuleni kwa ajili kuanza darasa la pili, nilikwenda madrasa k**a ilivyo ada huku Dakota akienda mazoezini. Siku hiyo, madrasa hapakuwa na masomo, kwa sababu kulikuwa na kikao cha dharura baina ya wazazi na walimu, kilichofanyikia kwenye moja kati ya madarasa yaliyokuwa wazi, ambapo, ilikuwa rahisi kuwasikiliza wachangiaji mada kutokea katika darasa lingine tulilohifadhiwa kwa muda. Kikao kilitokana na baadhi ya watoto kukutwa wakichezea mipira ya kiume, waliyoiokota katika majalala ya jirani na mitaa ya Buguruni Danguroni.

“Binafsi naungana na hoja Mzee Bakari hapo. Hatupaswi kufanya subra kwa watu wanaotuharibia watoto wetu. Twendeni huko huko kwenye madanguro yao, tukawaadabishe wao pamoja na wateja wao,” mzazi mmoja, ambaye sikutambua sauti yake, alisikika akisema.

“Mimi, msisitizo wangu bado ni ulele. Hatutopungukiwa chochote kwenda kutoa taarifa Kituo cha Polisi,” Bwana mmoja, aliyetajwa k**a Mjumbe wa Serikali ya Mtaa, alisikika akisema. “Tukisema tujichukulie sheria mkononi, ndugu zangu, tutajiletea matatizo bure bileshi. Haya sawa, mwenzetu hapa amesema hiyo mipira ya kiume inatupwa ovyo majalalani na hao hao wanaojiuza, lakini hatuna ushahidi wa moja kwa moja kuwatia hatiani. Lau k**a watafanikiwa kujitetea, nasi tukashindwa kuthibitisha, basi wakitush*taki wallahi hatuchomoki. Tutajiingiza kwenye madhara makub…”

“Madhara gani makubwa kuliko maradhi wanayoweza kupata watoto wetu kwa kuchezea hiyo mipira–tena iliyokwishatumika!” Mchangiaji mwingine alisema. “Kuna madhara makubwa kuliko mmomonyoko wa maadili kwa vizazi vyetu unaosababishwa na upuuzi wa watu hawa wachache?”

“Ndugu zangu, nimekuwa nikifuatilia mjadala huu kwa utulivu ili kunasa hisia za kila mmoja,” Sheikh Ramiya, Imam wa Msikiti ulioko sanjari na madrasa yetu, alisikika akisema. “Ni kweli, kadhia hii inatokea kwa mara ya pili sasa. Mara ya kwanza, tulitoa taarifa Kituo cha Polisi, walakini hapakuwa na hatua madhubuti zilizochukuliwa. Sasa basi, pamoja na kwamba naafikiana na wachangiaji waliopendekeza kwenda kuwak**ata hao wahusika na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria, nachelea kupuuza angalizo tulilonasihiwa na Mjumbe wa Serikali ya Mtaa hapa, k**a tahadhari tu ya kujiweka upande salama endapo lolote litatokea. Sasa je, tunaliwekaje hili ili tutimize azma yetu na tubaki salama?”

“Mimi nashauri hivi,” Ustadh Ahmada, mwalimu wetu wa madrasa, alisema. “Leo, saa mbili usiku, sote tuwe Kituo cha Polisi ili kutoa taarifa juu ya uchafu huu unaoendelea mtaani kwetu. Taarifa hiyo itaambatana na maelezo kwamba, muda huo huo, tunaelekea eneo la tukio kuwatia nguvuni wahusika. Kwa wingi wetu, bila shaka polisi wataiona hatari ya kutuacha twende peke yetu, na kwa hivyo watatufuata nyuma. Hapo tutakuwa tumepiga ndege wawili kwa jiwe moja; tutawak**ata wahusika tukiwa na ulinzi wa Polisi.”

Licha ya wachangiaji kadhaa kushauri namna nyingine za kulishughulikia jambo lile, rai ya Ustadh Ahmada ilikubalika zaidi na kupitishwa. Baada ya kikao kufungwa na watu kutawanyika, Ustadh Ahmada alikuja darasani na kuturuhusu turejee nyumbani. Ilikwishatimu saa kumi na mbili jioni.

Bupe alikuwa akipika wakati niliporejea nyumbani toka madrasa. Alikuwa amezungukwa na masufuria takribani sita, majiko mawili ya mkaa, ndoo za maji, pamoja na vitu vingine vidogo vidogo vyenye munasaba na mapishi. Pamoja na kutapanya vyombo vyote hivyo, alichokuwa akipika ni wali na maharage tu. Hilo likutoshe kufahamu Bupe alikuwa ni mpishi wa namna gani. Binafsi, sikumbuki kumwona, kabla ya siku hiyo, akiingia jikoni kupika.

“Shikamoo ma’mkubwa,” nilimsalimu.

“Marahaba, Chiku. Mzima?”

“Mzima,” nilimjibu na kuingia ndani.

Dakota aliyekuwa amesharejea nyumbani, nilimpita bila kumsalimia, akiwa amejilaza kwenye kochi sebuleni. Hatukuwa na utamaduni wa kusalimiana katika umri ule wa utotoni. Baada ya kumkosa mama chumbani, nilitoka na kumwuliza, “Dakota, mama yuko wapi?”

“Sijamwona.”

Nikamfuata Bupe hapo nje alipokuwa anapika, “Eti ma’mkubwa, mama yuko wapi?”

“Mama bado hajarudi,” alisema huku akinitazama usoni. Sauti yake yenye kitetemeshi ilivyosikika ni k**a anaongelea ndani ya maji. “Kuna nini?”

Nilimweleza habari niliyoisikia madrasa. Bupe ni mtu wa kudharau na kupuuza mambo. Huwa hajali chochote. Unaweza kutumia kila lugha kumtahadharisha na jambo la hatari, lakini maneno yako yote yakaingilia sikio moja na kutokea sikio lingine. Lakini taarifa hiii mpya, ilipoingia sikioni mwake, ilikita kwenye ubongo wake na kugoma kutoka. Papo hapo alinyanyuka na kuanza kuingiza vyombo ndani, kisha akatupakulia chakula na kuondoka akituacha tunakula.

Haikupita hata nusu saa, tukiwa tunamaliza kula, tulisikia kelele na purukushani za watu barabarani. Nilikimbilia chumbani kwa mama na kuchungulia dirishani. Watu walikuwa wakikimbia kuelekea bondeni, mitaa ya Buguruni Danguroni. Nilirudi sebuleni kumwambia Dakota kilichokuwa kikiendelea huko nje, nikijaribu kukihusianisha na kile nilichokisikia kwenye kikao cha wazazi.

“Twende tukaangalie,” Dakota alisema, akijua fika tulishakatazwa kutoka nje usiku, achilia mbali kwenda kwenye vurugu k**a hizo.

Mpambano mkali baina ya moyo na akili uliibuka ndani yangu. Kimoja kilitaka niende na kingine kikitaka nibaki nyumbani. Mara kwa mara ndani ya ubongo wa kila mtoto, huibuka mpambano baina ya umakini na upumbavu. Na mara nyingi upumbavu ndiyo hushinda. Hivyo, pamoja na kufikiria hatua ambazo mama atatuchukulia, endapo atakuta tumeacha nyumba bila mtu na kukimbilia huko Danguroni kushangaa vurugu, hatukujali.

“Twende, lakini tuwahi kurudi,” nilisema. Kabla hata sijamaliza kusema, tayari Dakota alikuwa ameshasimama nje ya mlango.

Tulifunga mlango na kushika njia. Dakota alikuwa mwenyeji wa mitaa ya Danguroni zaidi yangu, hivyo, nilimfuata nyuma bila kuuliza uhakika wa njia alizonipisha. Badala ya kutumia njia ya mzunguko, ambayo mama yangu hutumia, tulikatiza kichochoro cha kwanza, kisha tukanyoosha hadi kichochoro cha pili, kilichotuchukua hadi mtaa wa Danguroni.

Watu walikuwa wametawanyika huku na kule kushuhudia uk**ataji. Pamoja na idadi kubwa ya watu, ambapo kila mmoja alikuwa na jasho lake, bado harufu ya udi wa Danguroni ilisikika wazi wazi. Akina dada wanaojiuza walikuwa wanatoka kwenye vyumba vyao na kutimua mbio kukwepa polisi, huku baadhi yao wakik**atwa. Mtu wa kwanza kumwona akiwa amedhibitiwa na wak**ataji ni huyu mwanamke mnene, mweupe, aliyevaa gauni fupi na jepesi bila kitu ndani. Alifanana sana na yule tuliyemwona akimwingiza mwanaume chumbani mwake siku ile ya kwanza tulipokuja kwa Bupe. Alikuwa amek**atwa pamoja na mteja wake, bwana mmoja wa kati ya miaka 45 mpaka 50.

Jirani na chumba alichok**atiwa huyu mwanamke mnene, palikuwa na mwanamke mwingine mwembamba, mrefu, aliyegoma kuk**atwa baada ya kutolewa chumbani alikokuwa na mteja wake. Alikuwa akipigana na vijana waliokuwa wamekunja kanzu zao viunoni. Zilipiganwa ngumi za bila mpangilio hadi askari walipofika kumchukua wenyewe. Watu walikuwa wakishangilia na kuzomea kwa wakati mmoja.

Wote waliok**atwa walipelekwa kwenye karandinga ya polisi, iliyokuwa imeegeshwa mbele ya ile nyumba ambayo Bupe alimwambia mama yangu kuwa Dakota alikuwa akilala kwa rafiki yake. “Twende kule,” Dakota alisema, akinionesha kwa kidole kule lilipokuwa gari la polisi.

Kwenye karandinga ya polisi mlikuwa na wanawake kadhaa wanaojiuza pamoja na wateja waliok**atwa nao. Wakati tukiliambaa gari na kuhamia upande wa pili, ndipo nikamwona mama yangu akiwa miongoni mwa wanawake waliowekwa chini ya ulinzi. Ilikuwa picha mbaya sana machoni mwangu. Kwanza sikuamini, lakini baada ya kutulia kwa sekunde kadhaa, nilijihakikishia kuwa ni yeye. “Mama! Mama!” nilimwita ili walau nimpungie mkono, lakini sauti yangu ilimezwa na kelele zilizokuwa zimehanikiza eneo hilo.

Alikuwa ameinamisha kichwa chini k**a anayekwepa watu kumtambua. Nilijaribu kumwita tena bila mafanikio. Dakota alinishika mkono na kunivuta ili tuondoke eneo hilo ambalo ghasia na msongamano vilishtadi kweli kweli. Tuliondoka na kwenda kusimama mbele ya ile nyumba aliyokuwa akilala Dakota.

“Chiku!” Nilisikia sauti ambayo si ngeni masikioni mwangu ikinipigia kele. “Chiku! We Dakota!”

Tulipogeuka kufuata mwelekeo wa sauti tukakutanisha macho na Bupe, aliyekuwa ndani ya uzio wa nyumba hiyo, akichungulia kila kinachoendelea hapo barabarani. Tulimfuata tukiwa tumenywea k**a p**o lililotiwa mwiba.

“Mmefuata nini huku,” Bupe alisema, huku akimchapa kofi Dakota na kisha akafuata kwangu. Sikuwahi kumwona Bupe amekasirika k**a siku ile.

Alituondoa eneo la tukio na kuturejesha nyumbani muda huo huo. Njia nzima alikwenda anatukemea na kutusukuma k**a vibaka. Laiti k**a tungekuwa hatujala, siku hiyo tungelala na njaa, kwani alipotufikisha tu nyumbani, alitoa amri kila mmoja apitilize chumbani kulala kisha yeye akatoka tena. Sidhani k**a siku hiyo Bupe alilala. Alikuwa akizunguka k**a pia. Alitoka na kurudi nyumbani kila baada ya nusu saa. Na aliendelea na utaratibu huo kwa saa kadhaa hadi pale nilipopitiwa na usingizi.
*****

Jumatatu asubuhi, ikiwa ni siku ya tatu bila kumwona mama nyumbani, nish*tuka usingizini na kumwona mtu akiwa amesimama chumbani mwetu, mbele ya masanduku ya nguo. Nilishindwa kumtambua kwa haraka kutokana na mwanga uliopenya kwenye dirisha lililofunguliwa. Alikuwa Bupe. Alikuja kuniamsha kwa ajili ya kwenda shule.

Ilikuwa ni Jumatatu ya kufungua shule baada ya likizo ya mwezi wa kumi na mbili kutamatika. Lakini kulikuwa na haja gani ya kuniamsha kwa mtindo ule wa kufungua madirisha, niliwaza. Alishindwaje kuniamsha k**a alivyokuwa akituamsha mama?

Asubuhi hiyo niliota ndoto ya ajabu: Niliingia chumbani nikitokea bafuni kuoga. Mama yangu hakuwemo chumbani, lakini mezani palikuwa na kioo kidogo cha kujitazama. Siku zote mama alikificha mbali kioo chake ili nisikiguse, akidai kuwa mtoto akianza kupenda kujitazama kwenye kioo ataharibika tabia mapema. Niliangaza kulia na kushoto kisha nikakichukua na kujitazama. Badala ya kujiona sura yangu, nilimwona mtu mmoja ambaye sikumtambua kwa haraka akiwa amempiga kabali mama yangu. Pembeni yake alikuwapo Baruti, mtoto wa mama Sandra, akimpiga na kumng’oa nywele mama yangu huku akipambana kumpokonya madaftari yangu ya shule. Mvulana mwingine alikuwa amesimama upande wa pili wa barabara, akifuatilia kwa mbali mwenendo wa tukio zima na kutoa maelekezo ambayo, sikuweza kumwelewa alikusudia kumhami mama yangu au kuwawezesha akina Baruti. Kila nilipojaribu kukiweka kioo vizuri ili nimtambue, aligeuka pembeni na kujificha uso. Niliendelea kukigeuza kioo kushoto na kulia hadi nilipomnasa sura yake. Alikuwa ni Dakota. Kwa namna alivyokuwa akijificha uso ili nisimtambue ni dhahiri alikuwa anashirikiana na akina Baruti kumdhuru mama yangu. Kwa nini Dakota anafanya hivi? nilijiuliza.

Nilijaribu kufumba tena macho ili kujaribu kuimalizia, lakini Bupe akanisemesha. “Haya muda wa shule, Chiku.”

Nilifumbua tena macho na kumtazama hali ya kuwa mawenge ya usingizi yakiniandama. “Shikamoo ma’mdogo,” nilimsabahi.

“Marahaba.”

“Mama ameshaachiliwa?”

“Atarudi leo.”

Namna alivyotamka utadhani mama alikuwa safarini kurejea nyumbani. Ingawaje alijua fika kwamba, mimi na Dakota tunafahamu kuwa mama amek**atwa na polisi, hakutaka kabisa kututhibitishia hilo kwa kauli wala vitendo. Hata alipokuwa akimpelekea chakula polisi tangu alipok**atwa, hakutuambia anapeleka wapi chakula. Kufikiria tu kwamba, mama yangu pamoja na wahalifu wengine, alikuwa chini ya polisi kulitosha kunipa homa. Nilinyanyuka kitandani na kutembea hadi dirishani. Nikasimama na kutazama nje. Anga lilikwishakuwa pevu likinururishwa na weupe wa mawingu ya asubuhi.

Siku hiyo shuleni, kinyume na shauku na matarajio yetu, hatukuingia darasani. Badala yake tulipokelewa na zoezi la usafi wa shule, lililoanza asubuhi hadi mchana tuliporuhusiwa.

“Eti mama yako amek**atwa na polisi?” Sandra aliniuliza tulipokuwa tukirejea nyumbani toka shuleni.

“Nani kakwambia?” nilimwuliza, ingawaje nilikuwa na hisia kwamba atakuwa amesikia kwa mama yake.

“Nimewasikia akina Edna wakati tunafanya usafi.” Edna ni mtoto wa rafiki yake Bupe, anayeishi kwenye ile nyumba tulipomkuta Bupe akichungulia siku mama alipok**atwa.

Nilitamani kumwuliza, wamesema amek**atwa kwa kosa gani? Lakini nilijionya, k**a wameshajua kuwa amek**atwa, bila shaka watakuwa wanaijua sababu pia. Hivyo, sikukubali wala sikukataa. Nilibaki kimya nikitazama hewani ilhali fedheha ikinitafuna moyoni.

Sandra aliendelea kunitazama akitaraji majibu. Nilipokutanisha naye macho, nikageuka pembeni kuficha msawajiko wa uso wangu. “Amek**atwa kweli?” aliniuliza tena.

“Nilidhani ma’mkubwa ndiye amekwambia!” nilisema– nikimaanisha mama yake. Hakunijibu. Nami sikuendeleza majadala.

Siku iliyofuata, kwa mara ya kwanza, tulifika shuleni kwa kuchelewa. Bupe hakutuamsha kwa wakati. Wanafunzi wote walikwishaingia madarasani. Tuliingia darasani kwa kunyata na kusita, tukihofia kumkuta mwalimu. Tulipoingia darasani, wanafunzi wote walitugeukia mlangoni, wakidhani mwalimu ameingia.

“Humu ndani kuna watu wananuka udi wa Danguroni,” James alisema huku akijiziba pua kwa mkono.

Karibu nusu nzima ya darasa walicheka na kutuangalia. Kwa kawaida, udi hunukia. Hivyo, kitendo cha James kusema kuna watu wananuka udi wa Danguroni, baada ya kutuona tukiingia darasani kilibeba dhihaka dhidi yetu; mimi na Dakota. Hatukujali. Tukaketi kwenye madawati yetu.

Haikuchukua muda mrefu, Mwalimu Rehani Mkonongo aliingia darasani na kujitambulisha k**a mwalimu wa darasa. Alivaa shati jeupe la mikono mirefu na suruali nyeusi ambayo sehemu kubwa ya mapajani ilitapakaa vumbi la chaki. Zoezi la kwanza lilikuwa ni kutupanga kwenye madawati. Utaratibu ulikuwa ni ule ule wa kuchanganya jinsi. Mimi na Bijou tulipangwa pamoja na Bilal Kaisi. Papo hapo Bilal alijiinamia na kuanza kulia.

“Unalia nini, Bilal?” Mwalimu Rehani aliuliza huku akikunja mikono ya shati lake na kufanya bangili yake ya shaba katika mkono wa kushoto ionekane.

“Mimi sitaki kukaa dawati moja na huyu,” alisema–akiniashiria mimi.

“Kwa nini hutaki kukaa naye?”

“Atanifundisha tabia mbaya,” alisema kwa sauti ya chini, akijifuta machozi kwa kiganja cha mkono. “Mama yake am…” Kabla hajalifikisha mwisho neno lake, kicheko cha haja kililipuka baina ya wanafunzi wenzangu na kumfanya Bilal kusita.

Mwalimu Rehani alinyanyua uso na kulitazama darasa na kimya kikatanda. “Mnacheka nini?”

Hakuna aliyejibu.

“Haya endelea,” alisema huku akimgeukia Bilal. “Atakufundisha tabia gani?” Bila aliinamisha kichwa chini. “Sasa k**a hujibu, utakaa hapo hapo na wenzako. Na nikikuta umebadili nafasi utajuta kuzaliwa.”

Siku iliyofuata tulipoingia darasani, James aliwahi kuketi kwenye nafasi yangu, akifuatiwa na Bilal kisha Bijou. Hata aliponiona hakutaka kunipisha. Kila nilipotaka kumwambia anipishe kwenye nafasi yangu nilihisi vinyweleo vya hofu vikinitutumka.

“Naomba kukaa,” hatimaye nilisema, huku nikilainisha mdomo wangu kwa ulimi.

“Mnf! Mnf!” James alifanya k**a anayejiziba pua kwa kutumia mdomo huku akitoa pumzi nzito–ishara ya harufu mbaya. Papo hapo Bilal naye alijiziba pua kwa kutumia kola ya sweta lake.

James aliendelea kuketi pale pale ilhali nami nikisimama vile vile hadi aliposikia mwalimu akiingia darasani ndipo alinyanyuka haraka na kwenda kwenye dawati lao nami nikaketi. Mwalimu alipotoka baada ya kumaliza kufundisha, James alirudi tena na kuniamuru nimpishe kwenye nafasi yangu. Nilijihisi machozi yakinilenga machoni.

“We mtoto wewe,” Dakota, aliyekuwa ameketi kwenye moja kati ya madawati ya safu ya kulia, alisema huku akimnyooshea James kidole cha onyo. “Mwache mwenziyo akae.”

“Nani ni mtoto?” James alisema, akiniacha na kumfuata Dakota. “Unataka mchezo?” Alikunja ngumi tayari kwa kupigana. “Njoo nikuue! Njoo!”

Dakota alimtazama James wakati wanafunzi wengine wakichekelea. “Miye sitaki ugomvi na mtu. Mwalimu akitukuta tunapigana atatuchapa,” alisema.

“Poa. Tukitoka basi… saa saba… pale mwembeni,” James alisisitiza huku akikunjua ngumi na kunigeukia. “Na wewe ujiandae.”

Sikuwa na cha kujibu. Nilikosa raha kabisa. Nilitamani hata kumwomba msamaha japo sikulijua kosa langu.

***** Kabla ya kujiuliza ni ipi hatma ya Chiku na Dakota dhidi ya James Manonga, kwanza tujiulize ni nini hatma ya Maya (Mama Chiku) aliyeko mikononi mwa polisi? Lakini pia, ni ipi hatma ya shughuli iwaingiziayo kipato akina Bupe? TUKUTANE TENA kesho saa 12:30 jioni.

JENEZA LATAIFA (Sura ya sita)Mtunzi: Maundu Mwingizi “Nina hakika haitokuwa kisonono,” Bupe alisema, akimwambia mama wak...
08/09/2025

JENEZA LATAIFA (Sura ya sita)
Mtunzi: Maundu Mwingizi

“Nina hakika haitokuwa kisonono,” Bupe alisema, akimwambia mama wakati tulipoingia ndani tukitokea shuleni–japo machoni akimaanisha kinyume chake. Alikuwa amelala kwenye kochi huku mama yangu akiwa amekaa kwenye kochi hilo hilo, usawa wa miguu ya Bupe.

Aghalabu, Bupe huwa na namna yake ya kipekee ya kuelezea jambo kinyumenyume. Ili kumwelewa inahitaji utulivu wa akili pamoja na kumzoea kwa muda mrefu. anaweza kukuuliza, je, una wasiwasi na afya ya mtoto? Na kumbe hapo ni yeye ndiye mwenye wasiwasi–na si wewe. Anachotaka ni ithibati juu ya huo wasiwasi wake au ahueni na faraja kutoka katika majibu yako.

“Kwani unajisikiaje?” mama yangu alimwuliza, akiwa amemwekea mkono begani na macho amemkazia usoni.

“Mmh,” aliguna na kupitisha sekunde kadhaa za ukimya kabla ya kuendelea. “Sasa hivi maumivu ya tumbo hadi najihisi kuchemka mwili. Pia, maumivu makali wakati wa kukojoa.”

“Bupe,” mama yangu alisema huku akimsuta kwa macho. “Sasa hapo usichoelewa ni nini? Kumbe hata wakongwe huwa mnavunja kanuni ya kinga?”

“Unadhani itakuwa ni kisonono?” Bupe aliuliza tena, huku akijiinua taratibu na kuketi.

“Hebu acha utoto, Bupe. Kisonono kikikomaa husababisha utasa na hata kansa ya kizazi. Wahi hospitali sasa hivi ukapatiwe matibabu.”

“Mmh.”

Dakota aliketi kwenye kochi dogo, akimtazama mama yake aliyeonekana kuchoka mno, ilhali mimi nikiingia chumbani kuvua nguo za shule. Nilipotoka sebuleni, Bupe alikuwa ameshaanza kujiandaa kwa ajili ya kuelekea hospitalini. Siku hiyo, tofauti na siku nyingine, mama yangu hakutuuliuza chochote tulichojifunza shuleni. Ni k**a vile akili yake ilishughulishwa na afya ya Bupe.
*****

Siku iliyofuata, mama alituamsha k**a kawaida na kutuandaa kwa ajili ya kwenda shule, lakini hakutupeleka. “Mmeshakuwa wakubwa sasa, mnaweza kwenda shule na kurudi nyumbani peke yenu,” alisema na kutuacha tukitoka nyumbani peke yetu.

Tulipofika shuleni na kuingia darasani, ndipo kumbukumbu za kichapo nilichopewa na mama K**au zikaanza kujirejea kichwani mwangu. Hali ya kujiamini ikayeyushwa na hofu. Nikiwa nimeduwaa kwenye dawati langu, macho nikiwa nimeyaelekeza nje, bila kujua ni mwalimu gani atakayeingia darasani asubuhi hiyo, ghafla James Manonga, yule mvulana aliyetaja majina matatu, alikuja na kusimama mbele yangu. Nywele zake ndogo zilijisokota mithili ya uchafu wa sumaku. Sare zake za shule ni k**a zilitafunwa na ng’ombe kwa namna zilivyojikunja.

Nilipokutanisha naye macho, uso wake ulitengeneza makunyazi ya ghadhabu. “Kwa nini siku ile ulinicheka?” alisema bila kufunua kinywa chote, ni k**a meno yake yaligandana kiasi cha kufanya maneno yake yasikike kupitia katikati ya meno.

Nilijikuta nikiingiwa na hofu bila kujua kosa langu. K**a ni kucheka kutokana na vile alivyotaja majina yake matatu, tukio lile lilikwishapita zaidi ya juma moja nyuma. Lakini pia, sikucheka peke yangu, karibu darasa zima tuligeuka nyuma na kucheka. Kwa nini anikasirikie peke yangu? Bila shaka alinichukia mimi zaidi kwa kuwa ndiye sababu ya yeye kujichanganya baada ya kujaribu kuniiga.

“We mtoto,” Dakota, aliyekuwa dawati la nyuma yangu, alisema, “mwache mwenzako.”

“Yeye alivyonicheka siku ile,” James alisema na kuyapiga madaftari yangu yaliyokuwa juu ya dawati. “Leo tukitoka nitakukata hayo masikio yako marefu k**a popo.”

Dakota alisimama na kunisaidia kukusanya madaftari yangu yaliyokuwa yametawanyika sakafuni. James alilisukuma kwa mguu daftari moja kutokea pale chini kuelekea nyuma anakokaa yeye. Nilinyanyuka na kuanza kufuata daftari alilokuwa akiendelea kulisukuma kwa mguu wakati Dakota akinisaidia kuyapanga madaftari mengine aliyokuwa anayakusanya. Kadri nilivyokuwa nikimsogelea James, ndivyo alivyoendelea kulisukuma kwa mguu hadi alipofika mwisho wa darasa. Akalichukua kwa mkono na kumrushia rafiki yake aitwaye Bilal Kaisi, ambaye alilidaka na kulirusha tena kwa James.

Kwa haiba na tajriba, James na Bilal ni mbingu na ardhi. Bilal alikuwa nadhifu wa mwili na mavazi, kinyume kabisa na James ambaye, alikuwa k**a Kuruta wa Jeshi la Idd Amin aliyewekwa safu ya mbele kwenye Vita vya Kagera. Si tu mbele ya James, bali Bilal alijipambanua tofauti mbele yetu sote. Pamoja na kwamba, sote tulivaa sare zenye kushabihiana, bado Bilal alichomoza k**a mtoto kutoka kwenye familia yenye ukwasi au madaraka. Begi lake la madaftari tu peke yake lilikuwa na thamani sawa na sare zangu ukichanganya na za Dakota.

Waliendelea kurushiana huku wanafunzi wengine wakichekelea namna nilivyokuwa nikitaabika kuliwania daftari langu. Sandra na Dakota walisimama wakiniangalia kwa uchungu bila ya kujua hatua ya kuchukua. Kimya cha ghafla kilitanda. James na Bilal wakarudi kuketi kwenye madawati yao kwa utulivu k**a si wao waliokuwa wakinifanyia vurugu. Nikachutama chini ya dawati kuchukua daftari langu walilolitelekeza, likiwa limekwishachanika na kuchomoka ile pini ya katikati. Niliponyanyua ndipo nikakutanisha macho na Mama K**au. Nilihisi moyo ukichoropoka kifuani na kutuzama tumboni.

“Kuna nini huko? alisema huku akiangalia kule nilipokuwa nikichukua daftari langu. Na alipojua ni mimi, akaweka vitabu vyake mezani na kunifuata kule kule. “Unafanya nini huku we Chuki?”

Nilitamani kumwambia jina langu ni Chiku na si Chuki, lakini sikuwa na ujasiri huo. Badala yake nikasema, “Hawa watoto walichukua daftari langu wakawa wanarushiana.”

“Wewe ulifuata nini huku nyuma kucheza na wavulana,” alisema huku akinisogelea na kunifinya sikio la kulia. Akanikokota kuelekea kule mbele lilipo dawati langu. “Umeanza kuwa na tabia k**a za mama yako.”

Aliponifikisha kwenye dawati langu akaniachia sikio na kunichapa kofi la kichwa. “Nikikukuta tena unakimbizana na wavulana huko nyuma nitakupasua hiki kichwa chako.”

Nilijibwaga kwenye dawati na kuanza kulia kwa sauti ya chini. Kwa mara nyingine tena sikuelewa kosa langu hata nikastahili adhabu ile. Hatimaye mahaba yangu kwa Mama K**au yalisambaratika na kutengeneza hofu na chuki juu yake, kitu ambacho kilinifanya nichukie kila dakika ya masomo aliyoitumia darasani.
*****

Kwa takribani siku tatu mutawalia, Bupe hakwenda kazini, alibaki nyumbani akiendelea kujitibu. Yeye na Dakota wake wakawa wanalala kule chumbani kwangu, ilhali mimi nikirudi kulala chumbani kwa mama. Hata alipopona, hakuondoka tena. Akawa anakwenda kule kwake k**a kazini tu na usiku akirejea nyumbani. Rasmi tukawa familia ya watu wanne ndani.

Kitendo cha Bupe kuhamia nyumbani kwetu, baadhi ya majirani waliokuwa wakimfahamu kwa kazi yake ya kujiuza, moja kwa moja walimhusisha mama yangu na kazi hiyo pia. Minong’ono ikawa mingi mtaani. Wapo waliojitenga nao na wapo waliondelea kuamiliana nao kiujirani mwema bila kushughulishwa na kazi wanayofanya.

Jumatatu ya wiki iliyofuata, Mwalimu Regina alirejea darasani. Kwa namna sote tulivyosimama kumsalimia ndiyo nilijua, kumbe si mimi peke yangu, bali darasa zima tulimpenda na kumfurahia, kwa namna bashasha katika nyuso na shangwe katika sauti vilivyotamalaki kwa kila mmoja wetu. Licha ya upendo na kujali kwake, Mwalimu Regina alikuwa akijiheshimu yeye binafsi–mbele yetu–pamoja na kutuheshimu sisi licha ya umri wetu kuwa bado mdogo sana. Alikuwa mstahamilivu pale mwanafunzi anapochelewa kuelewa au hata pale mwanafunzi anapofanya uzembe.

Baada ya kuchangamsha miili kwa nyimbo mbili-tatu, Mwalimu Regina alipita akikagua madaftari ili kuhakiki mahali tulipofikishwa na Mwalimu Stella Njau (Mama K**au). Hapo ndipo alipokutana na daftari langu lililochanika na kuharibika. “Umelifanyaje daftari, Chiku?”

Nikamweleza namna James na Bilal walivyokuwa wakirushiana daftari langu huku wakiniita Chuki badala ya Chiku. Uso wa Mwalimu Regina ulibadilika mara moja. “James na Bilal piteni mbele haraka,” alisema. Walipopita mbele, akaniuliza tena, “Nani mwingine aliyeshirikiana nao?”

“Wengine walikuwa wananicheka wakati wanarushiana daftari langu,” nilijibu.

“Pigeni magoti hapo,” Mwalimu Regina aliwaambia James na Bilal huku akichukua fimbo iliyokuwa mezani. “Kwa nini mlichukua daftari la mwenzenu na kurushiana hadi mmeliharibu namna hii?”

James alirudia maneno yake yale yale, kwamba, hata mimi nilimcheka siku ile alivyotaja majina yake matatu.

“Na kwa nini mnamtania jina lake? Kwa nini mnamwita Chuki wakati mnajua jina lake ni Chiku.”

James alijitetea kuwa, si yeye aliyetunga jina hilo, bali ni Mwalimu Stella Njau. Bilal alikuwa kimya muda wote akionesha woga usoni, tofauti na James.

“Kwa nini Mwalimu Stella anakuita Chuki?” Mwalimu Regina aliniuliza.

Japo sikuweza kutongoa kwa utuo, kwa kuwa sikuijua kwa hakika sababu ya Mama K**au kunifanyia vile, nilijitahidi kumwelezea namna ilivyokuwa mpaka mwalimu alivyonichapa viboko. Mwalimu Regina alikunja ndita na kutikisa kichwa kadri nilivyokuwa nikieleza. Alikuwa k**a anayekaribia kulia kwa namna alivyokasirika, kitu ambacho sikutegemea kutoka kwake.

“Leo nitawachapa sana, wapumbavu nyie,” Mwalimu Regina alisema akiwatazama akina James. Papo hapo Bilal akaanza kulia. “Kutungana majina pamoja na kuharibina vitu ni tabia mabaya sana. Nani kawafundisha tabia mbaya namna hiyo?”

Mwalimu Regina aliwafuata James na Bilal pale walipokuwa wamepiga magoti. Nilitegemea angewapatia kipigo cha kukata na shoka, lakini fimbo alizowachapa hazikufikia japo robo–au hata thumni–ya kichapo nilichopewa na mwalimu Stella kwa kosa la kumtaja kwa jina la Mama K**au na kosa la kuliwania daftari langu lililokuwa mikononi mwa hao hao akina James. Alimchapa kila mmoja viboko viwili vya kawaida. Bilal alilia, si kwa maumivu, bali woga. Lakini James, hakuonesha ishara ya hofu wala dalili ya maumivu.

Baada ya James na Bilal kurejea kwenye madawati yao, Mwalimu Regina alisimama mbele akilitazama darasa. “Na wewe uliyekuwa unachekelea–au hata kunyamazia–badala ya kutoa taarifa, kitendo cha mwenzako kusumbuliwa kwa kutaniwa na kuharibiwa madaftari,” alisema kana kwamba kuna mtu mahsusi aliyemkusudia, japo alikusudia darasa zima, “huna tofauti na hawa wapuuzi waliokuwa wanamuonea mwenzao. Kwa hivyo, siku nyingine nikisikia mmechekelea au mmekalia kimya uonevu wa namna yoyote, nitawachapa darasa zima na kisha nawafukuza shule. Mmenisikia?”

Sote tukajibu, “Ndiyo mwalimu!”

“Sitaki watoto watukutu na waonevu katika darasa langu.”

Tuliendelea na masomo k**a kawaida, tukiwa na Mwalimu Regina, kwa muda wa wiki nzima, hadi wiki iliyofuata ambapo alirudi tena Mama K**au. Ulikuwa ni utaratibu mahsusi, ambapo, walikuwa wakipishana kwa kipindi cha wiki moja moja. Niliendelea kukabiliana na manyanyaso ya Mama K**au kila ilipowadia zamu yake darasani hadi tulipohitimu darasa la kwanza.

Katika masomo yote tuliyotahiniwa; Hisabati, Sanaa, Mwandiko, Kusoma na Afya, ni masomo mawili tu–Mwandiko na Afya–yaliyosahihishwa na Mama K**au, ndiyo nilipata alama 90% na 84%. Lakini yote yaliyosalia nilipata alama 100% na kufanya kila mwanafunzi asishangae pale nilipotangazwa kushika nafasi ya kwanza kati ya wanafunzi 50 wa darasani kwetu. Dakota alishika nafasi ya tatu, na Sandra nafasi ya kumi na moja.

“We Manonga si umerudia darasa mara ya pili hii?” Mama K**au alisema, akimwangalia James Manonga usoni. “Kwa nini umekuwa wa mwisho tena?”

James aliinamisha kichwa chini kwa aibu. Kwa mara ya kwanza ndiyo nilifahamu kuwa, James alikuwa amerudia darasa la kwanza kwa mara ya pili. Hapo ndipo nikapata picha kwa nini sare zake za shule, tangu siku ya kwanza, zilikuwa zimechakaa k**a mchanganya zege.

“Na wewe Sandra,” Mama Kakamu alisema, na kuhamishia macho yake kwenye dawati tulilokuwa tumeketi mimi, Sandra na Kapela, “umeshindwa kuingia hata kumi bora? Unakubali kuzidiwa akili mpaka na hawa watoto wa Danguroni?”

Kitendo cha mimi na Dakota kushika nafasi za juu, kilimwuuma sana Mama K**au, japo nina hakika hakuumia k**a tulivyoumia mimi na Dakota kwa kitendo chake cha kutuita watoto wa Danguroni, tena mbele ya kadamnasi. Pamoja na kwamba, bado sikuwa na ufahamu wa kutosha juu ya ubaya wa matendo yafanyikayo kule Buguruni Danguroni, lakini nilihisi kufedheheshwa mno.

*****Umewahi kufanyiwa au kushuhudia mtu akifanyiwa nyanyasaji, udhalilishaji, ufedheshaji? Unawezaje kuhusianisha na anachopitia Chiku? TUTAENDELEA KESHO

JENEZA LA TAIFA (Sura ya tano)Mtunzi: Maundu Mwingizi Urafiki baina ya Bupe na mama yangu ulishamiri. Ikawa kila siku as...
07/09/2025

JENEZA LA TAIFA (Sura ya tano)
Mtunzi: Maundu Mwingizi

Urafiki baina ya Bupe na mama yangu ulishamiri. Ikawa kila siku asubuhi Bupe na Dakota, wangekuja kushinda nyumbani mpaka jioni kabla ya Bupe kwenda kazini. Kwangu ilikuwa ni faida kumpata rafiki mpya. Tukawa tukicheza pamoja japo kila ilipofika saa tatu asubuhi, nilikuwa nikienda madrasa na kumwacha Dakota akicheza na Sandra. Ni katika kipindi hicho, kasi ya mama kwenda kwa Bupe iliongezeka maradufu. Karibu kila siku angeliondoka nyumbani majira ya saa mbili usiku, na kurejea saa nne–na wakati mwingine mpaka tano usiku. Mara kadhaa walirejea nyumbani wakiwa wamelewa. Wakati mwingine walitukuta tumeshalala, hivyo, ilimlazimu Bupe kumwamsha Dakota na kuondoka naye akiwa amembeba.

Siku moja, mama alimwambia Bupe, “Huu utaratibu wa kurudi usiku, sometimes tumelewa, halafu unaanza kubebana na Dakota, ni hatari kwako na kwa mtoto pia. Mimi ninafikiri sasa Dakota ungemwacha tu akawa anakaa hapa hapa.”

“Mwenye nyumba atakukubalia kweli?”

“Kwa nini akatae? Hatulishi wala hatuvishi,” mama alijibu, akiendelea kutandika kitanda. “Kwa bahati, nilishamwambia kuwa wewe ni ndugu yangu – mtoto wa mjomba wangu.”

Kuanzia siku hiyo Dakota akahamia rasmi nyumbani kwetu. Tulicheza na kukoga pamoja. Tulikula na kulala pamoja. Tulishikana urafiki na kushibana vilivyo, japo ni ule urafiki wa utoto; urafiki ambao huuchagui wala huutengenezi bali unaupokea baada ya kutengenezewa na mazingira. Urafiki wa bila sababu binafsi.

Kwa kuwa Dakota hakuwa Mwislamu, mama yake hakumpeleka madrasa. Muda ambao mimi nilikwenda madrasa, yeye alikwenda kwa Masta Msambati aliyekuwa na dojo ya kufundisha sanaa za mwili, maeneo ya Buguruni DownTown. Masta Msambati alikuwa ni mwalimu aliyebobea katika sanaa za mapigano, k**a vile, Tae Kwon do, Tae–Bo, na Jeet Kun Do. Alikuwa akifundisha watoto kuanzia miaka mitano na kuendelea.

Kila siku mchana au usiku tulipokuwa tukikutana nyumbani, nilikuwa nikimsomea Dakota Kuran pamoja na kumsimulia hadithi za Mtume, naye akinisimulia kuhusu mafundisho ya mbinu za kujihami na mapigo ya kushambulia aliyojifunza. Cha ajabu, wakati yeye akivutiwa na mafundisho ya dini niliyokuwa nikimsimulia hata akatamani kujiunga madrasa, mimi nilivutiwa na mafunzo ya sanaa za mapigano hata nikatamani kuacha madrasa ili kujiunga na dojo. Hakuna mwanadamu anayeridhika moja kwa moja na namna alivyo. Kila mmoja, kwa namna moja au nyingine, hutamani kuwa mtu mwingine au kufanya jambo lingine tofauti na lile ambalo amekuwa akilifanya.
*****

Nilipofikisha miaka saba, umri wa kuanza darasa la kwanza, Dakota alikuwa na miaka sita. Kwa hivyo, isingelikuwa busara mtoto mmoja kuanza shule ilhali mwingine akibaki nyumbani kwa tofauti ya mwaka mmoja tu. Mama yangu aliridhia kunisubirisha mpaka mwaka unaofuata Dakota atakapofikisha miaka saba ndipo tukaanze shule pamoja. Lakini kwa sababu umri ulithibitishwa kwa mwanafunzi kuzungusha mkono wake juu ya kichwa na kushika sikio la upande wa pili, Dakota alikuwa anaweza kushika sikio. Na hapo ndipo maandalizi yalifanywa kwa ajili yetu kuingizwa darasa la kwanza.

Siku hiyo, mama alituamsha saa kumi na mbili juu ya alama. Katika maisha yangu yote sikupata kuamshwa mapema namna ile. Niliamini mtu anapaswa kuamka baada ya usingizi wote kumalizika na mwangaza wa asubuhi kuhanikiza. Nilikuwa k**a zombi kwa namna nilivyokuwa nikiyumba kuanzia chumbani hadi sebuleni. Nilikuwa na usingizi utadhani sikulala mwaka mzima.

Anga bado lilikuwa la kijivu, ishara kwamba giza lilikuwa halijamalizika vizuri. Kumwona Dakota akiwa mwenye furaha na bashasha kukanikumbusha kuwa, ilikuwa ni siku yetu ya kupelekwa shuleni. Ilikuwa ni siku adhimu na adimu niliyoisubiri kwa hamu na ghamu. Mama alituogesha na kutupa chai kabla ya kutuvisha sare za shule.

Mimi nilivishwa viatu vyeusi vya soli fupi, soksi ndefu nyeupe, shati jeupe lililochomekwa kwenye sketi ya buluu, na mgongoni nilivishwa mfuko wa madaftari. Dakota alivishwa kaptula ya buluu, pamoja na viatu vyeusi vya kamba. Vingine vyote vilivyosalia tulifanana.

Shule haikuwa mbali sana kutokea hapo nyumbani. Ni chini ya kilometa moja. Dakota alitembea kwa miondoko ya madaha, akidunda utadhani kwenye viatu vyake amepachika moyo wa chura. Alijitanua makwapa k**a njiwa aliyepigwa manati, akiangalia kulia na kushoto mithili ya Mfalme anayekagua milki yake. Ilikuwa ni burudani tosha kumtazama.

Ukiniuliza nilikuwa najisikiaje sitoweza kuelezea. Lakini nina hakika, k**a ilivyo kwa watoto wengine wanapopelekwa shule kwa mara ya kwanza, ni furaha ya kwenda kuanza maisha mapya shuleni pamoja na wasiwasi wa kuachwa na wazazi mbali na nyumbani. K**a unaweza kuuelezea huo mchanganyiko wa furaha na wasiwasi utakuwa umenisaidia sana.

Takribani dakika kumi na tano kwa mwendo wa kinyonga tuliifikia Barabara ya Uhuru. Tulipokunja kona upande wa kushoto tukaiona Shule ya Msingi Buguruni. Haikuwa na majengo mazuri k**a nilivyotarajia. Kwa nje, madarasa pamoja na ofisi za walimu vilipakwa rangi nyeupe kwa juu na kijani kwa chini. Katikati ya madarasa na ofisi palikuwa na uwazi mkubwa. Madarasa yote yalikuwa na milango ya mbao na madirisha ya nondo.

Wazazi walijumuika na watoto wao mbele ya Ofisi ya Mwalimu Mkuu, wakiwaandikisha na kuwakabidhisha watoto wao. Baadhi ya watoto tulikuwa na furaha ilhali wengine walikuwa wakilia kwa woga. Miongoni mwa waliokuwa wakilia ni pamoja na Sandra. Alikuwa hataki kumwachilia mama yake aliyekuwa akimkabidhisha kwa mwalimu. Nilitamani anione lakini alikuwa mbali kidogo.

“Sandra!” nilimwita kwa sauti ya juu. Wakageuka wote, yeye na mama yake. Alipotuona akanyamaza ghafla na kujifuta machozi. Mama yake aliteta jambo na mwalimu kisha akamwambia Sandra atufuate mahali tulikokuwa tumesimama. Alianza kutufuata huku mama yake akimpungia mkono mama yangu na kuondoka bila kutusogelea.

“Shikamoo ma’mdogo,” Sandra alisema baada ya kutufikia.

“Marahaba mtoto mzuri,” mama alisema huku akimchukua na kumfuta machozi. “Usiogope mtoto mzuri, sawa eeh? Leo ni siku yenu ya furaha. Si unaona mlivyopendeza? Mtaimba na kucheza na baadaye mtarudi nyumbani.”

Tuliendelea kupanga foleni hadi ilipofika zamu yetu. Mama alitukabidhisha kwa mwalimu na kuondoka. Saa moja na nusu kengele iligongwa. Wanafunzi wote, isipokuwa sisi wapya, walijumukia kwenye eneo la wazi katikati ya shule na kujipanga safu. Sisi tulichukuliwa na kupelekwa moja kwa moja darasani. Tuligawanywa katika madarasa mawili: Mkondo A na Mkondo B. kwa bahati, Sandra, Dakota pamoja nami, tulipangwa darasa moja.

Darasani palikuwa na madawati ya kuweza kukaa wanafunzi watatu, yaliyopangwa kwa safu tatu; kulia, katikati, na kushoto. Mimi, Sandra pamoja na mvulana mmoja tulipangwa dawati moja, Dakota na wasichana wengine wawili walipangwa dawati la nyuma yetu.

Saa mbili na nusu aliingia darasani Bi Regina Sikumbili, ambaye alijitambulisha k**a Mwalimu wa Darasa. Alivaa sketi nyeusi na blauzi ya chanikiwiti. Hakuwa mrefu wala mfupi lakini mnene kupindukia. Alikuwa akizungumza taratibu huku akilizunguka darasa. Kadri alivyokuwa akitembea huku na kule blauzi yake ilipanda juu na kumwacha wazi sehemu ya kiuno na tumbo. Alipotutaka kila mmoja ajitambulishe jina kamili na sehemu anayoishi, nilimfikiria Dakota. Nilijua atajichukulia sifa kwa mwalimu kutokana umahiri wake wa kutaja majina yake matatu. Hivyo, kwakuwa dawati letu lilikuwa mbele yake, nilikuwa wa kwanza kusimama na kujitambulisha kabla yake. “Naitwa Chiku Akida Magan, naishi Buguruni Madenge. Nyumba namba 23,” nilisema na kuketi.

“Safi kabisa. Mpigieni makofi,” Mwalimu Regina alisema. Kishindo cha makofi kilirindima darasa zima. Hata walipomaliza, bado macho ya mwalimu pamoja na tabasamu lake vilikuwa kwangu. Namna yake ya kukapua macho kila alipotabasamu ilikuwa ni kuyafumba kwa sekunde kadhaa na kuyafumbua kwa madaha. “Napenda watoto wa namna hii. Anajua majina yake yote, mahali anapoishi, pamoja na namba ya nyumba. Kuanzia leo huyu atakuwa rafiki yangu. Haya, anayefuata,” alisema.

Aliyefuata alikuwa Sandra. Kwa namna mwalimu alivyonisifia, bila shaka naye alitamani kufanya k**a mimi, lakini hakujua majina yote matatu, akaishia kusema. “Naitwa Sandra Mwamba. Naishi Buguruni.”

Waliofuata hawakufanya k**a nilivyofanya mimi mpaka ilipofika zamu ya Dakota aliyekuwa dawati la nyuma yangu. “Jina langu ni Dakota Alfred Kolikoli. Naishi Buguruni Madenge.”

“Baba yako ni yule mcheza mpira?” Mwalimu Regina aliuliza. Dakota akaafiki kwa kutingisha kichwa.

“Alishaacha kucheza mpira eeh?”

“Ndiyo.”

“Anafanya kazi gani?”

“Mwanajeshi,” Dakota alidanganya. Nilitamani kugeuka nimwulize mbona mama yako alisema amekuwa mlevi? Lakini sikufanya hivyo.

“Yupo mkoa gani?”

Dakota alipiga kimya kwa sekunde akilitafuta jibu. “Dar es Salaam,” alijibu.

“Safi,” mwalimu alisema. Sikuelewa hiyo ‘safi’ ni kwa ajili ya Dakota kutaja majina yake matatu k**a nilivyofanya mimi au ni kwa ajili ya baba yake kuwa mwanajeshi. “Haya mwingine anayefuata,” Mwalimu alisema.

Utambulisho uliendelea, waliofuata waliendelea kujitambulisha kwa majina mawili mawili hadi ilipofika kwa huyu mvulana aliyesimama na kusema, “Naitwa James Manonga Manonga…”

Mwalimu Regina alishindwa kukizuia kicheko chake. Alichokifanya James ni ujanja wa kulirudia jina lake la mwisho mara mbili ili awe ametaja majina matatu k**a mimi na Dakota. “Wewe jina lako ni..?” Mwalimu Rejina alimsaili.

Aliposimama tena na kusema: “Naitwa James Manonga Manonga!” darasa lote likarindima kwa kicheko. Tuliokuwa tumeketi mbele tukageuka nyuma kumtazama. Japo alikuwa nyuma kabisa, lakini niliweza kumwona, alikuwa mfupi na mweusi.

“Baba yako anaitwa nani?” mwalimu alimsaili.

“Anaitwa Manonga.”

“Manonga nani?”

“Sijui.”

“Sasa mbona umesema unaitwa James Manonga Manonga?”

Kimya.

“Haya sawa.” Mwalimu Regina alitabasamu–na kila alipotabasamu macho yake yalisinyaa mithili ya paka aliyesimama juani. “Mwingine… anayefuata!”

Utaratibu uliendelea hadi mwisho. Ukiondoa mimi na Dakota, na huyu James Manonga Manonga, hakuna mwingine aliyejitambulisha kwa majina yake matatu hadi zoezi lilipomalizika. Baada ya zoezi la utambulisho kukamilika, mwalimu alitufundisha nyimbo ambazo tuliimba na kucheza hadi muda wa kutoka ulipowadia.

Mama yangu alikuwa miongoni mwa wazazi waliofika kuchukua watoto wao. Ilikuwa ni saa nne na nusu asubuhi. Njia nzima, tulikwenda tukishindana kumsimulia mama yangu mambo yote yaliyojiri shuleni. Kila siku mama alitupeleka na kutufuata shuleni.

Darasani tulikuwa tukiimba na kucheza–sipendi kutumia neno kunengua–japo ndicho tulichokuwa tukikifanya. Tuliimba nyimbo za kusifia ndege na wanyama, nyimbo za kusifia shule yetu na nchi yetu. Japo nilikuwa nikipenda sana kuimba, ilifikia hatua nikachoka. Hapakuwa na kingine zaidi ya kuimba. Wiki iliyofuata ndipo tulianza rasmi kufundishwa kusoma alfabeti – japo ilikuwa kwa mtindo ule ule wa kuimba. Tulipomudu kusozisoma–na kuziimba–kwa kwenda mbele, tukaanza kujifunza kuzisoma–na kuziimba–kwa kurudi nyuma.

Jumatatu ya wiki ya tatu, k**a kawaida, tuliingia darasani saa mbili kamili, lakini tulikaa bila mwalimu kwa takribani saa moja mbele hadi majira ya saa tatu ndipo tulimwona mwalimu, aliyekuwa amebeba vitabu, rula ndefu pamoja na viboko viwili, akiusukuma mlango kwa kutumia mgongo pamoja na kiwiko cha mkono, akiingia darasani. Katika hali iliyowash*tua wengi, hakuwa mwalimu Regina. Lakini katika hali iliyotufurahisha wachache, alikuwa ni Mama K**au. Alivalia sketi na blauzi vya rangi ya dongo pamoja viatu vyeusi vya soli ndefu. K**a kuna siku nilipatwa na furaha ya hali ya juu basi ni siku hiyo. Kila siku nilikuwa nikijiuliza, mama K**au yuko wapi! Nilitamani anione nikiwa darasani katika sare nadhifu za shule k**a mwanafunzi wake rasmi.

Nilimtazama Sandra kwa bashasha, kisha nikamgeukia Dakota aliyekuwa ameketi dawati la nyuma yetu. “Dakota,” nilimwita nikiwa nimetabasamu, “Mama K**au huyo.”

Nilipogeuza uso wangu mbele ilhali tabasamu langu likiwa limegoma kuyeyuka, nilikutanisha macho na Mama K**au akiwa amefura. “Huna adabu eeh?” alinikaripia huku akiweka vitabu vyake juu ya meza. “Nani amekwambia unite Mama K**au?” Sura ilimvimba kwa ghadhabu utadhani anataka kupasuka. “Haujibu eenh…haya njoo huku mbele.”

Nilinyanyuka na kupita mbele nisijue cha kufanya. Uso ulinisawajika ghafla. Nilipofika mbele akanipokea na viboko. Alianza kunichapa kwenye supu za miguuni, nilipoinama kujikinga kwa mikono akahamia kunichapa kwenye makalio. Nililia kwa sauti kubwa ya uchungu nikiwa nimehamanika.

“Haya toka hapa,” alisema huku akanimalizia na kiboko cha mgongo.

Nilikuwa mdogo nisiye na hatia, hivyo sikuwa na uwezo wa kujitetea wala mbinu ya kujipambania mbele ya mtu mzima aliyedhamiria kunishambulia. Nilirudi kwenye dawati nikiwa nimehamanika na kuchanganyikiwa. Niliketi na kujiinamia huku nikilia. Sandra naye alianza kulia, si kwa kunihurumia, bali kwa woga. Pengine alihisi anayefuata ni yeye. Darasa lilizizima kwa fadhaa. Nilijaribu kutafakari huku nikilia kwa sauti ya chini, nimetenda kosa gani hata nikastahili kichapo kile! Kichwa kiligoma kufanya kazi. Hata niliponyamaza kulia na kujiuliza, hivi kumwita kwa jina la mama K**au ilikuwa ni utovu wa adabu? Bado kichwa kilinigomea kufanya kazi.

“Naomba mnisikilize kwa makini,” Mama K**au alisema, akiwa amesimama katikati ya darasa, “kwa sababu sitorudia maelezo mara mbili.” Alijitambulisha kwa jina la Stella Abiud Njau, au kwa kifupi Mwalimu Stella Njau, na kututaka kila mmoja ajitambulishe kwa utaratibu ule ule tuliofundishwa na Mwalimu Regina: jina kamili na eneo unaloishi.

Walianza kujitambulisha walioketi safu ya kulia kabla ya kuja katikati na kumalizikia safu ya kushoto. Ilipofika zamu yangu, japo bado nilikuwa na dukuduku moyoni, nilisimama na kujaribu kulazimisha tabasamu usoni. “Naitwa Chiku Akida –” Oh, Mungu wangu, sauti ilikuwa ikitetemeka na kukwaruza mithili ya treni ya mizigo. Nilipojaribu tena kufunua mdomo ili nimalize kutaja sehemu ninayoishi, maneno yaligoma kutoka, na badala yake machozi yakaanza kunibubujika. Bado nilikuwa na uchungu. Nikainama na kujifuta kwa kiwiko.

“Unalia nini k**a zezeta,” Mama K**au alisema. “Ndo maana ukaitwa Chuki. Jina baya k**a sura yako.”

“Siyo Chuki,” nilisema kwa sauti ya chini, nikijaribu kumtazama usoni. “Ni Chiku.”

“Kaa chini,” alisema kwa kunikaripia. “Mwingine anayefuata…!”
Sikusubiri kuambiwa mara mbili kwa sababu nilijua kitakachotokea. Nikaketi. Siku hiyo sikuelewa chochote kilichoendelea darasani. Alfabeti zilinipita, na hata nyimbo nilizozipenda niliimba bila kujua naimba nini. Muda wa kutoka ulipowadia, alituruhusu tuondoke. Siku hiyo mama yangu hakuwepo kutuchukua. Japo hatukuwa na wasiwasi wa kufika nyumbani kwa sababu hapakuwa mbali sana – na njia tuliijua vizuri, lakini ilikuwa ni kawaida kwa mama kutufuata, na hakutujulisha k**a siku hiyo asingetufuata.

“Dakota! Dakota!” ilisikika sauti ya mtu, wakati tukiwa tunajaribu kumtafuta mama huku na kule.

Alipoita kwa mara ya pili tukamwona. Ni Kasongo. Alikuwa ameketi kwenye baiskeli yake – mguu moja ukiwa chini na mwingine kwenye pedeli. Miale ya jua iliyopiga kwenye mokasini yake iliyokolea dawa ya kiwi iling’aa. K**a kawaida yake, alivaa shati la mikono mirefu alilochomekea kwenye suruali yake ya kitambaa.

“Haya, mama amesema niwapige picha, kisha mwende nyumbani moja kwa moja. Leo hatokuja kuwachukueni.”

Siku hizo, upigaji picha haukuwa na tofauti kubwa na anasa nyinginezo. Ilihitaji fedha za ziada nje ya zile za mahitaji ya msingi, kitu ambacho familia nyingi za kipato cha chini hazikumudu. Kwa hivyo ilikuwa ni jambo la fahari kuonekana ukipiga picha mahali. Fahari hiyo haikuwa kwa wazazi pekee bali na kwa watoto pia. Hili lilinipunguzia machungu ya kichapo cha Mama K**au na kunisahaulisha fedheha yake.

Kasongo aliegesha baiskeli pembeni, akatoa kamera yake na kuunganisha lenzi, kisha akatupanga kwenye geti la kuingilia shule. Picha ya kwanza tulipiga wawili tu, mimi na Dakota. Picha ya pili tulijumuika kundi zima; mimi, Dakota, Sandra, Kapela, Faith na Jane.

*****Aaah banah eenh ITAENDELEA KESHO. Kumi na mbili na dakika thelathini.

Address

Ilala Boma
Dar Es Salaam
DARESSALAAM

Website

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Fanani na Hadhira posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Business

Send a message to Fanani na Hadhira:

Share

Category