26/05/2019
MICHUANO YA VINGUNGUTI SUPER CUP 2019 YAJA KIVINGINE
Kamati ya maandalizi ya michuano ya Vingunguti Super Cup leo tarehe 26 imekutana na wawakilishi wa timu mbalimbali katika kikao cha kwanza ili kuthibitisha ushiriki wao katika msimu huu wa 2019/2020
Michuano hiyo itakayofanyika katika uwanja cha Msikate Tamaa imejizolea umaarufu mkubwa katika kata ya vingunguti na maeneo ya jirani, inatarajiwa kuanza kutimua vumbi katikati mwa mwezi wa sita ambapo timu 48 zinategemewa kushiriki
Mkurugenzi wa michuano hiyo Bw. Spear Mbwembwe akiongea na waandishi wa habari, ametaja zawadi za washindi kwa msimu huu, ambapo mshindi wa kwanza atazawadiwa gari aina ya Noah pamoja na pea 20 za viatu, huku mshindi wa pili atakabidhiwa gari aina ya Noah vox wakati mshindi wa tatu atakabidhiwa pikipiki
Lakini k**a vile haitoshi timu zitakazofanikiwa kuingia 16 bora zitapewa jezi za kuchezea mashindano, pia mfungaji bora na mchezaji bora kuzawadiwa zawadi mbalimbali zikiwemo traki suti juu na chini, jezi pamoja na viatu huku golikipa bora atazawadiwa groves na traki suti
Pia Bw. Spear Mbwembwe amesema, mbali na kuboreshwa kwa michuano hiyo katika msimu huu, pia ameziomba taasisi, mashirika, makampuni pamoja na wadau mbalimbali kujitokeza katika kudhamini michuano hiyo ili kuweza kuwatia moyo vijana na kuinua vipaji vyao.
"Michuano ya mwaka huu ina utofauti mkubwa sana na mwaka jana, mwaka huu zawadi zimeboreshwa, mtindo wa kuendesha ligi umeboreshwa na tunatarajia katika kikao cha pili kuweza kuzipitia kanuni zote za michuano hii. Hivyo tunaomba mashirika, makampuni na wadau mbalimbali waje kudhamini hii michuano ili kwa pamoja tuweze kuwatia moyo vijana katika kuinua vipaji vyao"
Eidha Spear Mbwembwe amezishukuru timu zilizoweza kujitokeza leo katika kikao kilichofanyika katika ukumbi wa Itungi Lodge uliopo Vingunguti huku akizitaka timu nyingine kujitokeza katika kikao cha pili kitakachofanyika jumapili saa tano asubuhi katika ukumbi huo.