11/01/2026
Lucy Antony Michael (35), mkazi wa Yombo Dovya, Mtaa wa Makangarawe wilayani Temeke, Dar es Salaam, amevamiwa na kushambuliwa na watu wasiojulikana akiwa anatoka nyumbani kwake. Tukio hilo limemsababishia majeraha katika maeneo mbalimbali ya mwili.
Lucy ni miongoni mwa waumini wa Kanisa Katoliki waliowahi kwenda katika Ubalozi wa Vatican nchini kuwasilisha barua ya malalamiko kuhusu mwenendo wa baadhi ya viongozi wa kanisa hilo. Amedai kuwa kabla ya kushambuliwa alikuwa akipokea simu na jumbe za vitisho, matusi na kejeli kutoka kwa watu mbalimbali.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumapili Januari 11, 2026, Lucy amehusisha tukio hilo na maoni aliyoyatoa hadharani kwa nia ya kujenga na kurekebisha mwenendo wa viongozi wa kanisa, maoni ambayo amesema yamepokelewa kwa hisia hasi na baadhi ya watu katika jamii.
Baada ya tukio hilo, Lucy amefungua malalamiko katika Kituo cha Polisi Makangarawe na kupewa RB No. MAR/RB/49/2026.
Mashuhuda wa tukio hilo wameelezea kusikitishwa na tukio hilo na kuitaka polisi kuchukua hatua stahiki dhidi ya wahusika pamoja na kuimarisha ulinzi na usalama katika eneo hilo. ⚖️