29/05/2026
Na OWM - TAMISEMI, Kahama
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema Serikali haitomuongezea muda Mkandarasi M/s China Civil Engineering Construction Corporation wa kukamilisha miradi ya ujenzi wa barabara na mitaro katika Manispaa ya Kahama, inayotekelezwa kupitia Mradi wa Uendelezaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) kwani ubovu wa miundombinu ya barabara imekuwa ni kero ya muda mrefu kwa wananchi wa manispaa hiyo.
Prof. Shemdoe amesema hayo leo Mei 27, 2026 Katika Manispaa ya Kahama wakati wa hafla ya Utiaji Saini wa Mkataba wa Umaliziaji wa Ujenzi wa Barabara na Mitaro kupitia Mradi wa TACTIC, iliyofanyika katika eneo la Phantom kwenye manispaa hiyo.
“Ninamueelekeza Mkandarasi Kampuni ya M/s China Civil Engineering Construction Corporation kumaliza ujenzi ndani ya muda ulioanishwa katika mkataba ambao wameusaini leo, hakutakuwa na nyongeza ya muda,” amesisitiza Prof. Shemdoe.
Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amemtaka Mtaalamu Mshauri kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama pamoja na TARURA katika kuhakikisha mikataba iliyosainiwa inatekelezwa kikamilifu na inakamilika ndani ya muda uliopangwa na kwa ubora uliokubalika ili thamani ya fedha ionekane.
Prof. Shemdoe ameanisha kuwa Mei 27, 2026 imekuwa ni siku yenye furaha kwani kitendo cha kusainiwa kwa mikataba hiyo kinasadifu nia ya dhati ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwaboreshea miundombinu ya barabara wananchi wa Kahama, na kuongeza kuwa k**a lilivyo jina lake amekuwa ni suluhu ya changamoto iliyokuwa ikiwakabili wananchi wa Manispaa ya Kahama.
“Tumeshuhudia utiaji saini wa mradi huu mkubwa wa zaidi ya Shilingi Bilioni 25 ambazo Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameridhia zitumike kujenga miundombinu ya barabara katika Manispaa ya Kahama, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu 2025 hivyo tunamshukuru sana na kumuahidi kwamba ofisi yangu itasasimamia kikamilifu utekelezaji wa mkataba huo,” amesema Prof. Shemdoe.