03/08/2026
Na Berensi China
Tabora: Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Urambo mkoani Tabora wamepinga uamuzi wa Mkuu wa Wilaya hiyo, Hamisi Mkanachi, wa kuwasimamisha kazi viongozi wa Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori ya Uyumbu, wakidai hatua hiyo haikuzingatia haki na imeathiri utendaji wa jumuiya hiyo.
Hoja hiyo iliibuliwa katika kikao cha Kamati ya Uchumi na baadaye kuwasilishwa katika kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika Julai 30 na 31, 2026, chini ya Mwenyekiti wa Halmashauri, Athumani Mwiniko.
Baada ya kujadili taarifa ya kusimamishwa kwa viongozi hao, madiwani walieleza kutoridhishwa na uamuzi huo, wakidai ulifanyika bila kufuata utaratibu unaostahili.
Akizungumza katika kikao hicho, Diwani wa Kata ya Uyumbu, Gabriel Mkandala, alisema viongozi hao wamekuwa wakitekeleza majukumu yao kwa ufanisi tangu walipochaguliwa na kwamba hakuna sababu za msingi za kuwaondoa madarakani.
«"Sisi k**a madiwani tunapingana na uamuzi wa Mkuu wa Wilaya. Viongozi hawa wamekuwa wakifanya kazi vizuri tangu walipochaguliwa na jumuiya imekuwa ikifanya kazi vizuri. Hatuwezi kukubali kuona jumuiya ikivurugwa. Tunahitaji Kamati ya Uchumi na Fedha ifike eneo husika kujionea kinachoendelea," alisema Mkandala.»
Hoja hiyo iliungwa mkono na Diwani wa Kata ya Kasisi, ambaye alitaka kusimamishwa kwa viongozi hao kufutwe ili warejee kazini na kuendelea na shughuli za jumuiya k**a ilivyokuwa awali.
Kwa mujibu wa baadhi ya madiwani, chanzo cha mgogoro huo kinadaiwa kuwa ni hatua ya viongozi hao kuk**ata magunia ya mkaa na magogo yanayodaiwa kuhusishwa na mtu mwenye ushawishi mkubwa, madai ambayo hayajathibitishwa rasmi.
Aidha, ilielezwa kuwa viongozi hao walisafiri kwenda mkoani Manyara kwa ajili ya mafunzo ya kujifunza utendaji wa jumuiya nyingine ya hifadhi ya wanyamapori. Inadaiwa kuwa Mkuu wa Wilaya hakuridhia safari hiyo, na waliporejea walikuta wamesimamishwa kazi kuanzia Julai 7, 2026, bila kupewa barua rasmi. Baadaye, Julai 21, 2026, alitangaza uongozi mpya.