08/06/2026
Rais wa Jumuiya ya wanafunzi wa elimu ya Vyuo na Vyuo Vikuu Nchini TAHLISO Bw. Geofrey Kiliba amewataka Vijana wa Vyuo na Vyuo Vikuu Nchini kutambua nafasi zao katika jamii na namna ambavyo Taifa linawategemea katika ujenzi wa Taifa lao.
“Nchi yetu inatutegemea sana sisi Vijana, hatuwezi tukasahau na tukapuuzia uhalisia wa matumaini na mategemeo ya Taifa hili juu ya sisi Vijana. Wanatutegemea sisi vijana kwasababu kwanza tuna nguvu lakini pia kwasababu tuna maarifa. Wanatutumainia pia kwasababu sisi vijana tuna muda mrefu zaidi wa kuendelea kuichunga na kuiendeleza Nchi yetu.” Amesema.
Kiliba amebainisha hayo Juni 06, 2026 wakati akihutubia Bunge la serikali ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Tumaini Dar Es Salaam (DarTUso), akisisitiza pia umuhimu wa utulivu na busara katika kuyaendea mambo na kusema Mungu ndiye tumaini la maisha kwani yeye pia ndio hupanga mambo katika maisha ya binadamu.
Kiliba kadhalika amesisitiza umuhimu wa vijana hao kutokata tamaa na kujihusisha na makundi yasiyofaa kwenye jamii, akimtaka kila mmoja kutoogopa mustakabali wa kesho zao na badala yake kuhakikisha wanapambana katika kutimiza ndoto zao bila ya kukatishwa tamaa na changamoto mbalimbali zinazotokea katika maisha.