
01/09/2025
Jeshi la Polisi nchini limesema si kila taarifa ya utekaji au kupotea kwa mtu inayoripotiwa ina uhusiano wa moja kwa moja na vitendo vya uhalifu.
Msemaji wa Jeshi la Polisi, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) David Misime, amesema baada ya uchungu*i wa kina, imebainika kuwa baadhi ya matukio yamesababishwa na sababu binafsi au mambo ya kijamii ikiwemo wivu wa kimapenzi, imani za kishirikina, migogoro ya mali, kisasi, na hata visa vya watu kujiteka wenyewe.
“Polisi wataendelea kuchunguza kwa makini kila taarifa inayotolewa ili ukweli ujulikane na hatua stahiki zichukuliwe. Wananchi wanapaswa kuepuka kutumia hila au kujichukulia sheria mikononi, badala yake washirikiane na vyombo vya dola kusuluhisha matatizo yao,” amesema DCP Misime.
Hata hivyo, mjadala unaendelea miongoni mwa wananchi, hususan ndugu na jamaa za waliotekwa au kupotea bila kupatikana hadi leo, k**a vile Deus Soka, Mdude Nyagali, Ally Kibao, Sativa, Roma Mkatoliki na wengine, wakijiuliza iwapo kauli hizo za polisi zinaweza kuleta faraja kwao.