25/10/2025
Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko amesema utekelezaji wa mradi wa uendelezaji Miji Tanzania (TACTIC) kwenye Mji wa Mpanda utaleta mabadiliko chanya kwa wananchi wa Mji huo kwa kuimarisha huduma za usafiri na usafirishaji pamoja na kuboresha huduma za Kijamii na kiuchumi kwa wananchi.
Mhe. Mrindoko amebainisha hayo leo Jumamosi Oktoba 25, 2025, Mpanda Mjini mara baada ya kushuhudia utiaji saini wa kuanza kwa mradi wa TACTIC kati ya Halmashauri ya Mpanda na Mkandarasi M/s Chonqing International Construction Corporation, mradi ukijumuisha ujenzi wa barabara zenye urefu wa Kilomita 8.4 kwa kiwango cha lami, ujenzi wa jengo la usimamizi na ununuzi wa magari manne ya kusimamia utekelezaji wa mradi huo, Vyote vikitarajiwa kugharimu Shilingi Bilioni 21.9.
Kulingana na Mhe. Mrindoko barabara zitakazojengwa na mradi wa TACTIC ndani ya Manispaa ya Mpanda ni barabara za Mkumbo Junction- Nsemulwa health Center (Km1.68), Nsemulwa- Sokoine (Km1.23), barabara ya Kapufi (Mita 760), Sumri (Mita 460), Pinda (Mita 260), Fimbo ya Mnyonge (Mita 390), Fish Market (Mita330), Mpanda Hotel (Mita 760), Mikocheni Junction- White Girrafe (Km1.88) na Homeground yenye urefu wa Mita 730.
“Ni matumaini yangu kuwa mradi huu utakuwa chachu ya maendeleo na ustawi wa wananchi wa Mpanda na Mkoa wa Katavi kwa ujumla. Mradi huu utachochea biashara, kurahisisha shughuli za kiuchumi na Kijamii na zaidi kuuweka Mji wetu katika mandhari nzuri zaidi na kuzifanya barabara zetu zipitike muda wote.” Amesisitiza Mhe. Mrindoko.