04/06/2026
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amesema dunia ipo katika kipindi cha mabadiliko makubwa ya kiteknolojia yanayofungua fursa mpya kwa vijana, akiwataka kuwa tayari kujifunza na kuendana na kasi ya maendeleo hayo ili wasibaki nyuma.
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo jijini Moscow, Urusi, mara baada ya kutunukiwa Shahada ya Heshima ya Uzamivu na Peoples’ Friendship University of Russia (RUDN), ambapo alisisitiza kuwa maendeleo ya teknolojia k**a Akili Mnemba (AI), sayansi za mashine na maroboti yanaibadilisha dunia kwa kasi kubwa.
Amesema hakuna taifa linalotaka kubaki nyuma katika mapinduzi hayo ya kiteknolojia, huku akibainisha kuwa mafanikio yatapatikana kwa wale watakaokuwa tayari kujifunza, kuendana na mabadiliko na kutumia fursa zinazojitokeza.
Katika hotuba yake iliyopokelewa kwa makofi kutoka kwa washiriki wa hafla hiyo, Rais Samia alieleza kuwa elimu imeendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo duniani, ikichochea mabadiliko katika familia, jamii na taifa kwa ujumla.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na Naibu Waziri wa Sayansi na Elimu ya Juu wa Urusi, Konstantin Mogilevsky, ambaye alimpongeza Rais Samia kwa mchango wake katika kuimarisha sekta ya elimu nchini Tanzania.
Chuo Kikuu cha RUDN kina historia ya muda mrefu ya ushirikiano na Tanzania, ambapo tangu kuanzishwa kwake mwaka 1960 kimesomesha zaidi ya Watanzania 1,100, huku wanafunzi wengine 72 kutoka Tanzania wakiendelea na masomo yao katika ngazi mbalimbali chuoni hapo.
Kwa kutunukiwa heshima hiyo, Rais Samia anaungana na viongozi wengine wa Afrika waliowahi kutambuliwa na chuo hicho, akiwemo Sam Nujoma, Thabo Mbeki na Olusegun Obasanjo.