24/09/2025
Imeelezwa kuwa mafanikio yaliyopatikana chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungani wa Tanzania kupitia CCM, yameridhisha mioyo ya watanzania wengi hivyo anastahili kuchaguliwa tena.
Akihutubia wakazi wa Mufindi leo Septemba 24, Mgombea mwenza wa urais kupitia Chama Cha Mapinduzi, Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema kipindi chote cha kampeni watanzania wameahidi kukipatia chama hicho ushindi mkubwa kwenye uchaguzi wa Oktoba 29.
"Hayo ndiyo yanayofanya watanzania waseme 'Rais Samia yeye ndiye anatudai sisi' kwa sababu watu wanapima kazi anazofanya. Mimi na wenzangu tumepita katika mikoa 13, mikoa yote tuliyopita wamesema wao ndio watakaoongoza kwa kura za Dkt. Samia," ameeleza Dkt. Nchimbi.
Akianza kwa kueleza mipango iliyopo kwenye Ilani ya CCM 2025 - 2030 kwa Mufindi, Dkt. Nchimbi amesema hospitali ya wilaya itaboreshwa kwa kuongezewa majengo, vitendea kazi pamoja na wataalamu wa afya. "Lakini vilevile tunakwenda kujenga vituo vya afya vitano na zahanati mpya nane," amesema.
Kuhusu sekta ya elimu, Mufindi patajengwa shule mpya nne za sekondari, shule saba za msingi pamoja na ujenzi wa madarasa 264 kwa shule za msingi za zamani, ujenzi wa nyumba 34 za walimu.
Dkt. Nchimbi amebainisha kuwa katika kilimo kutakuwa na ongezeko la ruzuku ya mbolea na mbegu, kujengwa kwa vituo vipya viwili vya kukusanyia na kuuza maziwa. "Tunakwenda pia kuanzisha mashamba darasa kwa ajili ya wakulima, wafugaji na wavuvi ili wanapofanya shughuli za kilimo na uvuvi wafanye kitaalamu na kupata tija zaidi," ameeleza Dkt. Nchimbi.
Kadhalika, Dkt. Nchimbi ameahidi kumaliza kabisa changamoto ya umeme Mufindi kwani licha ya kazi kubwa iliyofanyika, CCM hakijaridhika na hivyo kitajenga mradi wa Nyalawa wa usambazaji wa umeme.