Njaro Media

Njaro Media Ukurasa Rasmi wa kutoka Tanzania. Kwa habari za ukweli kuhusu
Jamii | Serikali | Siasa | Michezo | Burudani | Uchumi
!

07/01/2026

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wafanya Biashara Tanzania (JWT), Abdallah Mohamed, ameipongeza Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kwa mchango wake mkubwa katika kukuza ujuzi wa vitendo na kuimarisha uzalishaji wa bidhaa nchini.

Pongezi hizo alizitoa Januari 6, 2026, alipotembelea banda la VETA katika Viwanja vya Dimani, Mkoa wa Mjini Magharibi, Zanzibar, wakati wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara Zanzibar (ZITF).

Mohamed alipata fursa ya kuelezwa namna VETA inavyotoa mafunzo ya ufundi stadi na jinsi walimu, wanafunzi pamoja na wahitimu wake wanavyoshiriki kikamilifu katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zinazozalishwa na kuuzwa kupitia Kampuni ya Ujuzi.

Maelezo hayo yalitolewa na Ofisa Masoko wa Kampuni Tanzu ya VETA, Ujuzi Incorporated Company Limited, Janeth Nkondora, aliyebainisha kuwa kampuni hiyo hutumia ujuzi wa vitendo unaotokana na mafunzo ya VETA kuzalisha bidhaa zenye ubora na ushindani sokoni.

Kwa mujibu wa waandaaji, Maonesho ya ZITF yalianza Desemba 29, 2025 na yanatarajiwa kufungwa Januari 16, 2026, yakivutia wageni wengi wanaotembelea banda la VETA kwa ajili ya kupata elimu kuhusu mafunzo ya ufundi stadi, fursa za ajira na ujasiriamali, pamoja na kununua bidhaa zinazozalishwa na Kampuni ya Ujuzi.


07/01/2026

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Kinondoni imefanikiwa kuwak**ata raia wawili wa China, Yao Licong na Wang Weisi, wakikutwa na kiasi kikubwa cha fedha kinachozidi Shilingi bilioni 2, kinachodaiwa kuwa cha uhalifu.

Watuhumiwa hao, wanaoishi Oysterbay jijini Dar es Salaam, walinaswa Januari 5, 2026 wakiwa na Dola za Kimarekani 707,075 pamoja na fedha taslimu za Kitanzania, zilizokuwa zimehifadhiwa kwenye mifuko ya sandarusi ndani ya gari walilokuwa wakitumia.

Uk**ataji huo umetokana na operesheni maalum ya miezi saba iliyoanza Mei 2025, ikishirikisha Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na mabenki mbalimbali, kwa lengo la kuvunja mtandao wa uhalifu wa kimtandao unaohusisha matumizi haramu ya kadi za benki.

Kwa mujibu wa uchunguzi wa awali, fedha hizo zinahusishwa na utakatishaji wa fedha uliotokana na wizi wa taarifa za kadi za benki za raia wa nje. Inadaiwa kuwa taarifa hizo hutumika kuchota fedha kwenye akaunti za wahanga, kisha kuoneshwa kana kwamba zimetumika kulipia huduma mbalimbali ndani ya Tanzania kinyume cha sheria.

TAKUKURU imeeleza kuwa watuhumiwa hao wameshindwa kuthibitisha uhalali wa fedha walizokutwa nazo, baada ya kukosa nyaraka muhimu ikiwemo uthibitisho wa biashara halali au stakabadhi za kubadilisha fedha za kigeni.

Katika taarifa yake iliyotolewa leo Januari 7, 2026, TAKUKURU imesema uchunguzi bado unaendelea kwa lengo la kuwabaini na kuwak**ata wanachama wengine wa mtandao huo. Watuhumiwa waliok**atwa tayari wamefikishwa mahak**ani kujibu tuhuma zinazowakabili kwa mujibu wa sheria za nchi.


07/01/2026

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. George Simbachawene, amewataka askari wa Idara ya Uhamiaji nchini kuongeza ufanisi, weledi na kutoa huduma zenye heshima kwa wageni wanaoingia nchini, hususan watalii, ili kuendelea kuilinda na kuitangaza taswira chanya ya Tanzania kimataifa.

Amesema sekta ya utalii ni nguzo muhimu ya uchumi wa taifa kutokana na mapato makubwa yanayoingizwa, ambayo yamekuwa yakisaidia maendeleo ya sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu, ujenzi wa barabara na viwanja vya ndege. Kwa msingi huo, Simbachawene amesisitiza kuwa askari wa uhamiaji wana wajibu mkubwa wa kuhakikisha wageni wanapata huduma bora, za haraka na zenye staha tangu wanapowasili nchini.

Waziri huyo ametoa kauli hiyo wakati wa kikao chake na uongozi wa juu wa Idara ya Uhamiaji kilichofanyika visiwani Zanzibar, ambapo pia alihimiza kuzingatiwa kwa maadili ya kazi, uzalendo na matumizi sahihi ya mamlaka katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

Katika kikao hicho, ilielezwa kuwa sekta ya utalii imeendelea kukua kwa kasi, ambapo mwaka 2024 Tanzania iliingiza watalii 1,924,240, huku idadi hiyo ikiongezeka na kufikia watalii 2,097,823 mwaka 2025, hali inayoonesha mwelekeo chanya wa ukuaji wa sekta hiyo.

Mhe. Simbachawene amesema ukuaji huo unapaswa kwenda sambamba na uboreshaji wa huduma katika maeneo ya mipakani, viwanja vya ndege na bandari, akisisitiza kuwa uhamiaji ni lango la kwanza la mgeni nchini na mchango wao ni muhimu katika kuendeleza utalii endelevu.


07/01/2026

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, ametoa wito kwa wananchi kujenga utamaduni wa kufuatilia na kuzingatia sheria pamoja na miongozo mbalimbali iliyopo nchini ili kuepuka migogoro na matatizo yasiyo ya lazima.

Wito huo umetolewa leo Jumatano Januari 7, 2026, akiwa Kunduchi jijini Dar es Salaam, alipofika kutatua mgogoro wa ardhi baina ya wananchi, ikiwa ni siku moja baada ya tukio la kuk**atwa kwa raia wa China katika eneo la Oysterbay, Dar es Salaam.

Tukio hilo lilizua mjadala mkubwa baada ya kusambaa kwa picha mjongeo mitandaoni ikimuonesha raia huyo akiwa na kiasi kikubwa cha fedha kinachodaiwa kufikia mabilioni ya shilingi, hali iliyosababisha vyombo vya usalama kuingilia kati na kumchukua kwa mahojiano.

Akizungumza na wananchi, Mkuu wa Mkoa amesisitiza kuwa kutofuata taratibu za kisheria, hasa katika masuala ya ardhi na umiliki wa mali, kunaweza kusababisha migogoro mikubwa na kuhusisha vyombo vya dola pasipo ulazima.

Amesema Serikali itaendelea kusimamia sheria kwa usawa kwa raia wote bila kujali uraia au hadhi ya mtu, huku akiwahimiza wananchi kutoa taarifa sahihi kwa mamlaka husika pindi wanapobaini vitendo vinavyokiuka sheria.


07/01/2026

Januari 7, 2026 — Raia wa Ethiopia wameungana kuadhimisha Sikukuu ya Krismasi leo Januari 7, huku maelfu ya Wakristo wa Kanisa la Orthodox wakishiriki ibada na sherehe za kiimani zilizoanza kwa mkesha mkubwa uliofanyika jana Jumanne Januari 6 katika Uwanja wa Meskel, jijini Addis Ababa.

Waumini, wengi wao wakiwa wamevalia mavazi meupe ya kitamaduni, walishiriki hafla ya kuwasha mishumaa iliyofuatwa na ibada ya kanisani iliyodumu usiku kucha. Ibada hiyo imeashiria kumalizika kwa siku 43 za mfungo wa Krismasi kwa waumini wa Kanisa la Orthodox la Ethiopia.

Kanisa hilo hutumia kalenda ya Juliani, ambayo iko nyuma kwa siku 13 ikilinganishwa na kalenda ya Gregori inayotumiwa na madhehebu mengi ya Kikristo duniani, ikiwemo Wakatoliki na Waprotestanti. Tofauti hiyo ya kalenda ndiyo sababu Krismasi ya Ethiopia huadhimishwa Januari 7 kila mwaka.

Sherehe hizo zimefanyika katika kipindi ambacho Ethiopia imekuwa ikikabiliwa na changamoto za kiusalama katika baadhi ya maeneo. Licha ya kumalizika kwa vita vya Tigray mwaka 2022, mikoa ya Amhara na Oromia bado inakabiliwa na machafuko yanayochochewa na waasi wenye misingi ya kikabila.

Hata hivyo, mji mkuu wa Addis Ababa umeendelea kuimarika kiuchumi na kimazingira, kufuatia uwekezaji mkubwa uliofanywa na Waziri Mkuu Abiy Ahmed Ali. Miradi hiyo inajumuisha ujenzi wa njia za baiskeli, vituo vya mikutano, bustani za kisasa na makumbusho, hatua zinazolenga kuubadilisha uso wa jiji hilo.

Ethiopia inatarajia kufanya uchaguzi mkuu mwezi Juni 2026, huku sherehe za Krismasi zikionekana k**a ishara ya mshik**ano wa kitaifa na matumaini ya amani katika taifa hilo la Pembe ya Afrika.


07/01/2026

Rais wa Marekani, Donald Trump, ametangaza kuwa Venezuela imekubali kutoa mafuta kati ya mapipa milioni 30 hadi 50 kwa ajili ya kuuzwa nchini Marekani, kufuatia mabadiliko makubwa ya kisiasa yaliyotokea baada ya operesheni ya kijeshi ya Marekani iliyomuondoa madarakani Rais wa zamani wa nchi hiyo, Nicolás Maduro.

Kupitia ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wake wa kijamii wa Truth Social, Trump amesema mafuta hayo yatauzwa kwa bei ya soko la kimataifa, huku mapato yake yakisimamiwa moja kwa moja chini ya uangalizi wake k**a Rais wa Marekani. Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha fedha hizo zinatumika kwa maslahi ya Marekani na kusaidia uthabiti wa kiuchumi wa Venezuela katika kipindi cha mpito.

Trump ameeleza kuwa amemuagiza Waziri wa Nishati wa Marekani, Chris Wright, kusimamia utekelezaji wa mpango huo kwa kutumia meli maalum za kuhifadhi mafuta na kuzisafirisha moja kwa moja hadi katika bandari za Marekani. Mpango huo unatarajiwa kuanza mara moja ili kuhakikisha upatikanaji wa mafuta hayo bila kuchelewa.

Aidha, Rais Trump amesema hatua hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa Marekani kuifufua sekta ya mafuta ya Venezuela, ambayo imekuwa ikidorora kwa miaka kadhaa kutokana na vikwazo, ukosefu wa uwekezaji na changamoto za kiutawala. Amebainisha kuwa Marekani inapanga kushirikiana na makampuni makubwa ya mafuta ya Marekani, yakiwemo ExxonMobil, Chevron na ConocoPhillips, ili kusaidia kurejesha uzalishaji na kuimarisha miundombinu ya mafuta nchini Venezuela.

Tamko hilo limeibua mjadala mpana kimataifa, huku wachambuzi wakisema mpango huo unaweza kubadilisha kwa kiasi kikubwa mwelekeo wa kisiasa na kiuchumi wa Venezuela pamoja na nafasi ya Marekani katika soko la nishati duniani.


07/01/2026

Uingereza na Ufaransa zimetia saini azimio la pamoja linalolenga kupeleka wanajeshi nchini Ukraine endapo makubaliano ya amani yatafikiwa kumaliza vita kati ya Ukraine na Urusi, Waziri Mkuu wa Uingereza Sir Keir Starmer ametangaza.

Akizungumza baada ya mazungumzo na washirika wa Ukraine yaliyofanyika mjini Paris, Sir Starmer amesema makubaliano hayo yanalenga kuimarisha usalama wa Ukraine na kuzuia uvamizi wowote wa baadaye.

Kwa mujibu wa Starmer, nchi hizo mbili zimepanga kuanzisha kambi za kijeshi katika maeneo mbalimbali ya Ukraine mara tu makubaliano ya amani yatakapoanza kutekelezwa, hatua inayolenga kutoa dhamana ya usalama wa muda mrefu kwa taifa hilo.

“Tumeafikiana kwamba endapo amani itapatikana, tutachukua jukumu la kusaidia kulinda Ukraine dhidi ya vitisho vya baadaye,” amesema Starmer.

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amesema maelfu ya wanajeshi wa nchi yake wako tayari kupelekwa Ukraine k**a sehemu ya utekelezaji wa makubaliano ya usalama yatakayokubaliwa.

Viongozi hao pia wameeleza umuhimu wa kuwepo kwa dhamana thabiti ya usalama kwa Ukraine, wakipendekeza Marekani ichukue jukumu la kuongoza na kufuatilia utekelezaji wa mkataba wowote wa amani utakaoafikiwa.

Hata hivyo, licha ya makubaliano hayo ya awali, suala la umiliki wa baadhi ya maeneo yenye mgogoro bado linaendelea kujadiliwa na halijapatiwa suluhu ya moja kwa moja.

Wakati huo huo, Urusi imeendelea kuonya vikali dhidi ya uwepo wa wanajeshi wa kigeni nchini Ukraine, ikisisitiza kuwa hatua hiyo itachukuliwa k**a tishio la moja kwa moja kwa usalama wake na kwamba wanajeshi wowote wa nje watakaoingia Ukraine “watakabiliwa” ipasavyo.


06/01/2026

Zaidi ya madereva 100 wa malori kutoka Tanzania wamekwama katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) kufuatia hali tete ya kiusalama iliyoibuka baada ya vurugu za wananchi dhidi ya Serikali ya nchi hiyo.

Kwa mujibu wa madereva waliokwama, vurugu hizo ziliripotiwa leo Jumanne Januari 6, 2026, zikihusisha wachimbaji wadogo wa madini waliopinga uamuzi wa Serikali wa kuwazuia kuendelea na shughuli zao. Hali hiyo imesababisha kusimamishwa kwa safari na kuwalazimu madereva kubaki katika maeneo ya migodi bila uhakika wa lini wataendelea na safari.

Akizungumza kwa njia ya simu, dereva Frank Egina amesema amekwama katika Mgodi wa Kisamu baada ya hali ya usalama kuzorota ghafla. Amesema aliwasili eneo hilo Jumapili na kushusha mzigo wake salama, lakini tangu kuzuka kwa vurugu hizo, madereva wamezuiwa kuondoka hadi hali itakapotulia.

Kwa upande wake, dereva mwingine Hassan Maganga amesema hali katika mitaa ya maeneo ya jirani ni mbaya, huku madereva wakilazimika kubaki ndani ya eneo la mgodi chini ya ulinzi mkali wa vyombo vya usalama vya DRC ili kulinda maisha yao.

Akizungumzia changamoto hiyo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mahmoud Thabit Kombo, amesema Serikali ya Tanzania imeanza kuchukua hatua mbalimbali kwa kushirikiana na mamlaka za DRC ili kuhakikisha usalama wa madereva hao na kuondoa vikwazo vinavyokwamisha shughuli zao.


06/01/2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya mazungumzo maalum na viongozi wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) katika Ikulu ndogo ya Tunguu, Zanzibar.

Mazungumzo hayo yalihusisha masuala mbalimbali ya ulinzi na usalama wa nchi pamoja na utekelezaji wa majukumu ya Jeshi la Kujenga Taifa katika kulinda na kuimarisha uzalendo miongoni mwa vijana wa Kitanzania.

Baada ya kikao hicho, Mhe. Rais Samia alipiga picha ya pamoja na viongozi hao, akiwemo Waziri wa Ulinzi na JKT, Mhe. Dkt. Rhimo Simeon Nyansaho, Katibu Mkuu Kiongozi, Mhe. Balozi Dkt. Moses Kusiluka, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na JKT, Dkt. Faraji Mnyepe, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania (JWTZ), Jenerali Jacob John Mkunda, pamoja na Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Meja Jenerali Rajabu Mabele.

Kikao hicho ni sehemu ya juhudi za Rais Samia kuendelea kuimarisha ufanisi wa vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na usimamizi wa rasilimali watu na miundombinu ya kijeshi nchini.


06/01/2026

Timu ya Taifa ya Kandanda ya Tanzania (Taifa Stars) ambayo ilikuwa irejee nchini kesho Januari 07, 2025 sasa itarejea Januari 08, 2026. Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, amesema mabadiliko hayo yamelenga kuiwezesha timu hiyo kuwasili katika muda mzuri utakaotoa nafasi kwa Watanzania kuwapokea na kuwapongeza wachezaji kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya kwenye mashindano ya AFCON 2025 yanayoendelea nchini Morocco.

Kwa mujibu wa mabadiliko hayo, Taifa Stars itawasili nchini keshokutwa majira ya saa 4:00 asubuhi na kupokelewa na wananchi wakiongozwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mheshimiwa Prof. Palamagamba Kabudi.

Msigwa ametoa wito kwa wananchi wa Dar es Salaam kujitokeza kwa wingi kuwashangilia na kuwapongeza mashujaa hao kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya wakiwa nchini Morocco.


06/01/2026

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene, amewataka maafisa wakaguzi na askari wa Jeshi la Polisi wa ngazi mbalimbali kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia misingi ya haki, usawa, weledi na uadilifu, akisisitiza kuwa misingi hiyo ndiyo msingi wa ulinzi wa raia, mali zao na maendeleo ya taifa kwa ujumla.

Akizungumza katika Mkutano wa Baraza la Askari uliofanyika Chuo cha Polisi Zanzibar tarehe 5 Januari 2026, Waziri Simbachawene amewahimiza askari kutoka mikoa mitatu ya Unguja kuheshimu utawala wa sheria na kuonesha uwajibikaji wa hali ya juu katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku kwa wananchi.

Amesema Jeshi la Polisi lina dhamana kubwa ya kulinda usalama wa raia na mali zao, na kwamba utekelezaji wa jukumu hilo lazima uongozwe na haki, usawa, uwajibikaji na uadilifu ili kuhakikisha taifa linapiga hatua za kimaendeleo kwa misingi imara ya amani na utulivu.

Katika hotuba yake, Waziri Simbachawene amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kulitambua Jeshi la Polisi k**a nguzo muhimu ya usalama wa nchi kwa kutenga rasilimali kwa ajili ya kuboresha miundombinu, vitendea kazi na mazingira ya kazi ya askari.

Ameeleza kuwa Serikali inaendelea kulijenga na kuliboresha Jeshi la Polisi ili liendane na mahitaji ya sasa ya kiusalama, sambamba na kuboresha maslahi ya askari, hatua inayolenga kuongeza ufanisi katika kulinda raia na mali zao. Kwa mujibu wake, jitihada hizo ni sehemu ya mkakati mpana wa kuijenga polisi ya kisasa, yenye uwezo wa kukabiliana na changamoto mpya za kiusalama.


06/01/2026

Mjane wa Baba wa Taifa na Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Maria Nyerere, amepokea nishani ya heshima kutoka Jamhuri ya Angola k**a kutambua mchango mkubwa wa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika harakati za ukombozi na ujenzi wa amani nchini humo.

Nishani hiyo imekabidhiwa kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), aliyesema heshima hiyo ni ushuhuda wa mchango wa kipekee wa Mwalimu Nyerere kwa Angola na Bara la Afrika kwa ujumla.

Mhe. Kombo ameeleza kuwa Tanzania ilitoa ardhi yake k**a kitovu cha harakati za ukombozi kwa mataifa mbalimbali ya Afrika, ikiwemo Angola, kwa kutoa hifadhi, kupanga mikakati na kutoa mafunzo kwa wapigania uhuru.

Kwa upande wake, Balozi wa Angola nchini Tanzania, Mhe. Domingos de Almeida da Silva Coelho, amesema Angola inathamini kwa dhati mchango wa Mwalimu Nyerere katika kupatikana kwa uhuru wake, akibainisha kuwa nishani hiyo ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru wa Angola na ishara ya mshik**ano wa kweli wa Afrika.

Akizungumza baada ya kupokea nishani hiyo, Mama Maria Nyerere ameishukuru Angola kwa heshima hiyo kubwa, akisisitiza kuwa mafanikio ya Mwalimu Nyerere katika kuikomboa Afrika yalitokana pia na mshik**ano na ushirikiano wa viongozi wenzake wa Afrika.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhe. Makongoro Nyerere, akizungumza kwa niaba ya familia, amesema Mwalimu Nyerere aliamini kuwa uhuru wa Tanzania haukuwa kamili bila uhuru wa Afrika nzima, hivyo alijitoa kusaidia mataifa mengine kufikia ndoto hiyo. Ameishukuru Angola kwa kuendelea kuitambua na kuiheshimu familia ya Mwalimu Nyerere.

Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Ukombozi ya Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU) kuanzia mwaka 1964 hadi 1985, akiongoza juhudi zilizosaidia ukombozi wa nchi kadhaa ikiwemo Namibia, Msumbiji, Afrika Kusini, Zimbabwe, Guinea-Bissau na Cape Verde.


Address

S. L. P 2528
Dodoma

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Njaro Media posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Business

Send a message to Njaro Media:

Share