07/01/2026
Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wafanya Biashara Tanzania (JWT), Abdallah Mohamed, ameipongeza Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kwa mchango wake mkubwa katika kukuza ujuzi wa vitendo na kuimarisha uzalishaji wa bidhaa nchini.
Pongezi hizo alizitoa Januari 6, 2026, alipotembelea banda la VETA katika Viwanja vya Dimani, Mkoa wa Mjini Magharibi, Zanzibar, wakati wa Maonesho ya Kimataifa ya Biashara Zanzibar (ZITF).
Mohamed alipata fursa ya kuelezwa namna VETA inavyotoa mafunzo ya ufundi stadi na jinsi walimu, wanafunzi pamoja na wahitimu wake wanavyoshiriki kikamilifu katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zinazozalishwa na kuuzwa kupitia Kampuni ya Ujuzi.
Maelezo hayo yalitolewa na Ofisa Masoko wa Kampuni Tanzu ya VETA, Ujuzi Incorporated Company Limited, Janeth Nkondora, aliyebainisha kuwa kampuni hiyo hutumia ujuzi wa vitendo unaotokana na mafunzo ya VETA kuzalisha bidhaa zenye ubora na ushindani sokoni.
Kwa mujibu wa waandaaji, Maonesho ya ZITF yalianza Desemba 29, 2025 na yanatarajiwa kufungwa Januari 16, 2026, yakivutia wageni wengi wanaotembelea banda la VETA kwa ajili ya kupata elimu kuhusu mafunzo ya ufundi stadi, fursa za ajira na ujasiriamali, pamoja na kununua bidhaa zinazozalishwa na Kampuni ya Ujuzi.