14/01/2026
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi nchini Uganda, Simon Byabak**a, amesema tume hiyo itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa uhuru na kwa kuzingatia sheria, huku akikanusha madai kuwa kuna shinikizo la kuzuia kutangazwa kwa mshindi fulani wa uchaguzi ujao.
Byabak**a amezungumza kufuatia kusambaa kwa video kwenye mitandao ya kijamii ikimuonesha mshauri wa Rais akidai kuwa Tume ya Uchaguzi haitamtangaza mgombea wa upinzani, Robert Kyagulanyi maarufu k**a Bobi Wine, endapo atashinda. Akijibu hoja hiyo, Byabak**a amesema tume itamtangaza mshindi yeyote kulingana na matokeo halali yatakayohesabiwa.
Ameeleza kuwa licha ya mijadala na hofu zinazoenezwa, yeye binafsi hana woga bali analenga kutimiza wajibu wake kwa raia wa Uganda. Aidha, amesisitiza kuwa uchaguzi huo hautavuruga amani ya nchi, akiahidi kuwa mchakato mzima utaendeshwa kwa uwazi na haki.
Raia wa Uganda wanatarajiwa kupiga kura kesho Alhamisi, Januari 15, kuwachagua Rais na Wabunge. Wagombea wanane wanachuana kuwania kiti cha Urais, akiwemo Rais wa sasa Yoweri Museveni mwenye umri wa miaka 81 anayewania muhula wa saba, huku mpinzani wake mkuu akiwa ni Bobi Wine.