06/09/2025
Jeshi la Israel leo (Jumamosi) limeeleza kuwa wakaazi wa Jiji la Gaza wanapaswa kuondoka na kuelekea maeneo ya kusini, huku vikosi vyake vikiendeleza mashambulizi katika sehemu kubwa ya mji huo.
Taarifa ya msemaji wa jeshi hilo, Avichay Adraee, imetolewa kupitia mtandao wa X (zamani Twitter) ikiwataka wakaazi hao kuelekea Khan Younis, eneo la pwani lililoko kusini mwa Gaza, na kuwahakikishia kuwa watapatiwa huduma muhimu k**a chakula, makazi na matibabu.
Jeshi la Israel limedai kuwa kwa sasa linadhibiti karibu asilimia 75 ya Gaza, huku likiendelea na operesheni katika vitongoji vya mji wa Gaza ambavyo vimekuwa uwanja wa mapigano makali kwa wiki kadhaa. Siku ya Alhamisi, jeshi hilo lilitangaza kuwa linamiliki takribani nusu ya jiji hilo.
Hata hivyo, baadhi ya wakaazi wameripotiwa kukataa kuhamishwa, wakisema wamechoshwa na mizunguko ya kuhamia sehemu moja hadi nyingine tangu vita vilipoanza.
Taarifa kutoka mamlaka ya afya ya Gaza zinaeleza kuwa zaidi ya watu 64,000 wamepoteza maisha tangu mapigano hayo kuanza, huku maeneo makubwa ya Gaza yakiwa yameharibiwa vibaya na wakaazi wake wakikabiliana na hali ngumu ya kibinadamu.
Wakati huo huo, hatua ya Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, kuidhinisha operesheni ya kuteka mji wa Gaza kinyume na mapendekezo ya baadhi ya mak**anda wa kijeshi, imeendelea kuongeza mvutano na kuiacha Israel ikikabiliwa na upinzani wa kidiplomasia kutoka kwa baadhi ya washirika wake wa karibu.