12/11/2025
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linawashikilia watu 38 raia wa Ethiopia, wote wakiwa wanaume, kwa kosa la kuingia nchini kinyume cha sheria.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi Benjamini Kuzaga, watuhumiwa hao walik**atwa Novemba 11, 2025, katika pori la ranchi ya Matebete lililopo kijiji cha Igumbilo Shamba, Kata ya Chimala, Wilaya ya Mbarali.
Watuhumiwa hao walikuwa wakisafiri kwa gari aina ya Toyota Noah lenye namba za usajili T.953 DJF, mali ya Stanslaus Mazengo, ambaye ndiye anayetajwa kuwaongoza.
Taarifa hiyo inaeleza kuwa Mazengo alikiri kuwa alikuwa akiwapeleka wahamiaji hao kufichwa katika nyumba ya Jackline Malya, mkazi wa Chimala, kwa lengo la kuwaandalia safari ya kwenda Afrika Kusini kwa njia za kificho.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limewataka wananchi kuacha tamaa ya fedha na kuepuka kushiriki vitendo vya kuwawezesha raia wa kigeni kuingia au kupita nchini kinyume cha sheria, na badala yake wawashauri kufuata taratibu rasmi kupitia mamlaka husika ili kuepuka hatua kali za kisheria.