Njaro Media

Njaro Media Ukurasa Rasmi wa kutoka Tanzania. Kwa habari za ukweli kuhusu
Jamii | Serikali | Siasa | Michezo | Burudani | Uchumi
!

14/01/2026

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi nchini Uganda, Simon Byabak**a, amesema tume hiyo itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa uhuru na kwa kuzingatia sheria, huku akikanusha madai kuwa kuna shinikizo la kuzuia kutangazwa kwa mshindi fulani wa uchaguzi ujao.

Byabak**a amezungumza kufuatia kusambaa kwa video kwenye mitandao ya kijamii ikimuonesha mshauri wa Rais akidai kuwa Tume ya Uchaguzi haitamtangaza mgombea wa upinzani, Robert Kyagulanyi maarufu k**a Bobi Wine, endapo atashinda. Akijibu hoja hiyo, Byabak**a amesema tume itamtangaza mshindi yeyote kulingana na matokeo halali yatakayohesabiwa.

Ameeleza kuwa licha ya mijadala na hofu zinazoenezwa, yeye binafsi hana woga bali analenga kutimiza wajibu wake kwa raia wa Uganda. Aidha, amesisitiza kuwa uchaguzi huo hautavuruga amani ya nchi, akiahidi kuwa mchakato mzima utaendeshwa kwa uwazi na haki.

Raia wa Uganda wanatarajiwa kupiga kura kesho Alhamisi, Januari 15, kuwachagua Rais na Wabunge. Wagombea wanane wanachuana kuwania kiti cha Urais, akiwemo Rais wa sasa Yoweri Museveni mwenye umri wa miaka 81 anayewania muhula wa saba, huku mpinzani wake mkuu akiwa ni Bobi Wine.


14/01/2026

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. M***a Azzan Zungu, amewasili jijini New Delhi, nchini India, leo Januari 14, 2026, kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 28 wa Maspika wa Mabunge ya Jumuiya ya Madola.

Mhe. Spika amepokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Indira Gandhi na Balozi wa India nchini Tanzania, Mhe. Anisa Mbega, mara baada ya kuwasili kwake.

Mkutano huo wa siku tatu unatarajiwa kufunguliwa rasmi kesho, Januari 15, 2026, na Waziri Mkuu wa India, Mhe. Narendra Modi, na utawakutanisha Maspika wa Mabunge kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali yanayohusu uimarishaji wa demokrasia, utawala bora na ushirikiano wa kibunge.

Ushiriki wa Tanzania katika mkutano huo unaendelea kuimarisha nafasi ya nchi katika majukwaa ya kimataifa ya kibunge na kuendeleza diplomasia ya kimataifa kupitia Bunge.


14/01/2026

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amezitaka wizara na taasisi zote zinazohusika na masuala ya ajira kusimamia kikamilifu utekelezaji wa sheria zinazolinda nafasi za kazi za Watanzania, akisisitiza kuwa kazi zinazoweza kufanywa na Watanzania hazipaswi kufanywa na wageni isipokuwa pale tu kunapokuwepo na upungufu wa utaalamu wa ndani.

Aidha, Dkt. Mwigulu amekemea vikali tabia ya baadhi ya wamiliki wa nyumba kuwakodishia wageni kisha kuwaruhusu wageni hao kuwapangisha watu wengine wengi ndani ya nyumba hizo, akieleza kuwa mwenendo huo ni tishio kwa usalama wa taifa na pia unawakosesha Watanzania manufaa ya kiuchumi.

Agizo hilo limetolewa leo Jumatano, Januari 14, 2026, wakati akifungua kikao cha pamoja cha Mawaziri, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu na Manaibu Makatibu Wakuu wa Wizara za Kisekta kilicholenga kujadili fursa za ajira ndani na nje ya nchi.

Waziri Mkuu amesema kuwepo kwa idadi kubwa ya wageni wanaojihusisha na ajira au biashara zinazoweza kufanywa na Watanzania kunachangia kuongeza changamoto ya ajira nchini, hivyo ni wajibu wa wataalamu wa ndani kuhakikisha sheria zinatekelezwa ipasavyo. Ameongeza kuwa endapo kuna mianya au vikwazo vya kisheria vinavyokwamisha utekelezaji, viharakishwe kubainishwa na kufanyiwa marekebisho.

“Hatuwezi kuendelea kuleta watu kufanya kazi ambazo Watanzania wanaziweza. Ni lazima tuwe na uzalendo na kulinda maslahi ya nchi yetu,” amesema Dkt. Mwigulu.

Ametoa mfano wa mmiliki wa nyumba anayemkodishia mgeni kwa gharama ndogo, kisha mgeni huyo kuwakodisha watu wengi kwa gharama kubwa zaidi, hali inayosababisha Mtanzania kupata hasara huku kukiwa na hatari za kiusalama.

Kauli hiyo inalenga kuimarisha usimamizi wa ajira, kuongeza fursa kwa Watanzania na kulinda uchumi pamoja na usalama wa taifa.


14/01/2026

Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) inaanza rasmi utekelezaji wa mpango wa kuwarejesha nchini wakimbizi zaidi ya 80,000 waliopo katika Kambi ya Nyarugusu, wilayani Kasulu mkoani Kigoma, waliokimbilia Tanzania tangu mwaka 1996.

Mpango huo unalenga kuwapatia fursa wakimbizi walio tayari kurejea kwa hiari yao kushiriki moja kwa moja katika ujenzi wa taifa lao na kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi baada ya kuishi uhamishoni kwa zaidi ya miongo mitatu.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii wa DRC, Bi. Ève Bazaiba, amesema hayo wakati wa ziara yake ya kwanza katika Kambi ya Wakimbizi ya Nyarugusu, akisisitiza kuwa serikali yake imejipanga kikamilifu kuhakikisha zoezi la urejeaji linafanyika kwa usalama, kwa heshima na kwa kuzingatia matakwa ya wahusika wenyewe.

Kwa mujibu wa Waziri Bazaiba, urejeaji huo ni sehemu ya mkakati mpana wa serikali ya DRC wa kuimarisha umoja wa kitaifa, kurejesha matumaini kwa raia wake na kuharakisha maendeleo endelevu nchini humo, hasa katika maeneo yaliyokumbwa na migogoro kwa miaka mingi.

Serikali ya DRC inaeleza kuwa itaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania pamoja na mashirika ya kimataifa ili kuhakikisha mchakato huo unatekelezwa kwa mafanikio na kwa kuzingatia haki za wakimbizi wote wanaochagua kurejea nyumbani.


14/01/2026

Waziri wa zamani wa Burkina Faso, Yolande Viviane Compaoré, ameuawa katika makazi yake jijini Ouagadougou, tukio lililozua taharuki nchini humo.

Maafisa wa usalama wamesema mwili wa Compaoré uligunduliwa nyumbani kwake Jumamosi iliyopita, huku dalili za awali zikionyesha kuwa alishambuliwa kabla ya kuuawa. Mamlaka za mahak**a zimeanzisha uchunguzi rasmi na kutoa wito kwa mtu yeyote mwenye taarifa zinazoweza kusaidia uchunguzi huo kujitokeza.

Compaoré alikuwa mmoja wa wanasiasa wenye ushawishi mkubwa wakati wa utawala wa Rais wa zamani Blaise Compaoré. Aliwahi kuhudumu k**a gavana wa Mkoa wa Kaskazini, mbunge wa chama tawala cha zamani cha CDP, na kushika nyadhifa mbalimbali za uwaziri zikiwemo Uchukuzi na Utalii. Pia aliwahi kuwa mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje na Ulinzi.

Utawala wa Blaise Compaoré ulimalizika mwaka 2014 baada ya maandamano makubwa ya wananchi, hali iliyomlazimu rais huyo wa zamani kukimbilia Côte d’Ivoire. Baada ya kuondoka kwake, Burkina Faso ilipitia kipindi cha uongozi wa mpito kilichoanza chini ya Isaac Zida na baadaye Michel Kafando, kabla ya uchaguzi wa 2015 uliomuingiza madarakani Roch Marc Christian Kaboré.

Hata hivyo, Kaboré aliondolewa madarakani kupitia mapinduzi ya kijeshi Januari 2022, yakamleta Luteni Kanali Paul-Henri Sandaogo Damiba, ambaye naye alipinduliwa Septemba 2022 na Kapteni Ibrahim Traoré. Kapteni Traoré ndiye kiongozi wa Burkina Faso hadi sasa.

Kifo cha Yolande Viviane Compaoré kinaongeza orodha ya matukio yanayoibua maswali kuhusu usalama na mivutano ya kisiasa nchini Burkina Faso.


14/01/2026

Jeshi la Polisi Mkoa wa Kilimanjaro limesema linaendelea na uchunguzi kuhusu kifo cha mtuhumiwa Michael Lambau (18), aliyefariki dunia baada ya kujinyonga akiwa mahabusu ya Kituo cha Polisi Moshi Kati.

Kwa mujibu wa Polisi, Lambau alikuwa akishikiliwa kwa tuhuma za kumshambulia baba yake mdogo kwa kutumia mabapa ya panga. Aidha, imeelezwa kuwa kabla ya tukio hilo, mtuhumiwa huyo aliwahi kuhusishwa na mauaji ya baba yake mzazi, anayedaiwa kuchomwa shingoni kwa kitu chenye ncha kali, kisha mtuhumiwa kutoroka.

Polisi wamesema mtuhumiwa alik**atwa baadaye kufuatia tukio la kumshambulia baba yake mdogo, kabla ya kujinyonga akiwa mahabusu. Uchunguzi unaendelea kubaini mazingira kamili ya tukio hilo, huku Jeshi la Polisi likitoa wito kwa wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa vyombo vya dola.


14/01/2026

Serikali za Denmark na Greenland zimeweka wazi msimamo wao thabiti wa kupinga vikali kauli za Rais wa Marekani, Donald Trump, zinazodai kuwa Marekani inapaswa kuichukua Greenland. Viongozi wa pande zote mbili wamesisitiza kuwa Greenland itaendelea kubaki ndani ya Ufalme wa Denmark na kuwa sehemu ya NATO pamoja na Umoja wa Ulaya.

Jumanne, Januari 13, 2026, Waziri Mkuu wa Denmark, Mette Frederiksen, na Waziri Mkuu wa Greenland, Jens-Frederik Nielsen, walikutana mjini Copenhagen na kuonesha mshik**ano wa kisiasa na kidiplomasia kabla ya mikutano muhimu inayotarajiwa kufanyika Jumatano jijini Washington.

Akizungumza na waandishi wa habari, Frederiksen alisema Denmark na Greenland zinasimama pamoja na wananchi wa Greenland na kusisitiza kuwa mustakabali wa kisiwa hicho upo ndani ya Ufalme wa Denmark, NATO na Umoja wa Ulaya, si chini ya udhibiti wa Marekani. Kauli hiyo ilikuja ikiwa ni majibu ya matamshi ya hivi karibuni ya Trump aliyedai kuwa Marekani inapaswa kudhibiti Greenland kwa “njia yoyote ile”.

Wakati huo huo, Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Denmark na Greenland, Lars Løkke Rasmussen na Vivian Motzfeldt, wamewasili Ikulu ya White House kwa mazungumzo na Makamu wa Rais wa Marekani, JD Vance, pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje, Marco Rubio.

Mvutano huu unaendelea kuchochewa na umuhimu wa kimkakati wa Greenland katika eneo la Aktiki, hasa katika masuala ya usalama na siasa za kimataifa. Hata hivyo, Denmark imesisitiza kuwa ulinzi wa Greenland tayari uko chini ya mwamvuli wa NATO, hivyo hakuna msingi wa hoja ya Trump kuhusu kile alichokiita mpango wa “kuichukua” Greenland.


14/01/2026

Shirikisho la Mpira wa Miguu Rwanda (FERWAFA) linamwondoa kocha Adel Amrouche katika nafasi ya kocha mkuu wa timu ya taifa ya wanaume ya Rwanda, Amavubi, baada ya kuhudumu kwa takribani miezi 10.

Uamuzi huo unafanywa jana Jumanne, Januari 13, 2025, huku FERWAFA ikieleza kuwa unatokana na ukiukwaji mkubwa wa masharti ya mkataba wa ajira, ingawa haijaweka wazi kwa undani masharti yaliyokiukwa.

Kupitia taarifa rasmi, FERWAFA linaeleza kuwa hatua hiyo imechukuliwa baada ya tathmini ya kina kwa mujibu wa kifungu cha 17.2 cha mkataba wa ajira wa kocha huyo, na kwamba Amrouche alipatiwa muda wa kutosha kurekebisha masuala yaliyoibuliwa kabla ya uamuzi wa kusitisha mkataba kufanyika.

Amrouche, aliyewahi kuinoa timu ya taifa ya Tanzania kabla ya kujiunga na Amavubi Machi 2, 2025, amepewa shukrani kwa mchango wake ndani ya muda aliokuwa akiinoa Rwanda, huku shirikisho likimtumia salamu za kila la heri katika majukumu yake yajayo.


13/01/2026

Wananchi wanaendelea na shangwe baada ya Yanga SC kukabidhiwa kombe la kufuatia ushindi wa mikwaju ya penalti 5-4 dhidi ya Azam FC.

Mchezo huo unamalizika kwa sare ya bila kufungana hadi dakika 120 (AET), kabla ya Yanga kuibuka kidedea kwenye penalti na kutwaa taji hilo.


13/01/2026

Fulltime ( PENALTY (4-5)


13/01/2026

Serikali ya Uganda imetangaza kusitisha huduma za intaneti kote nchini kuanzia saa 12 jioni leo, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika siku ya Alhamisi. Hatua hiyo imekuja wakati Rais Yoweri Museveni akiwania muhula wake wa saba wa uongozi.

Tangazo hilo limezua taharuki miongoni mwa vyama vya upinzani pamoja na mashirika ya haki za kiraia, yakionya kuwa kuzimwa kwa intaneti kunaweza kudhoofisha uwazi na uadilifu wa mchakato wa uchaguzi. Wanasiasa wa upinzani wanasema hatua hiyo itapunguza upatikanaji wa taarifa kwa wananchi, kuzuia mawasiliano ya haraka na kuathiri ufuatiliaji wa matukio ya uchaguzi kwa wakati halisi.

Kwa upande mwingine, wadau wa haki za binadamu wamedai kuwa kuzimwa kwa intaneti ni kinyume na misingi ya demokrasia na haki ya wananchi kupata taarifa, wakitaka mamlaka kurejesha huduma hizo ili kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa uwazi na amani.


Address

S. L. P 2528
Dodoma

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Njaro Media posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Business

Send a message to Njaro Media:

Share