09/06/2026
Tanzania na Singapore zimekubaliana kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, biashara na uwekezaji katika jitihada za kuongeza manufaa kwa wananchi wa nchi hizo mbili, kufuatia mazungumzo yaliyofanyika kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Tharman Shanmugaratnam.
Akizungumza leo Jumanne Juni 09, 2026 baada ya kumpokea Rais Tharman aliyewasili nchini kwa ziara ya kitaifa, Rais Samia amesema viongozi hao wamejadili namna ya kuufanya ushirikiano kati ya Tanzania na Singapore kuwa wenye tija zaidi na kutoa matokeo yanayoonekana katika maendeleo ya mataifa hayo mawili.
Rais Samia amesema pamoja na ukuaji wa biashara kati ya nchi hizo, bado kiwango kilichofikiwa hakijakidhi matarajio ya pande zote mbili.
Amebainisha kuwa kwa sasa biashara kati ya Tanzania na Singapore inafikia dola za Marekani milioni 299 huku Singapore ikiwa imewekeza kupitia miradi 36 nchini Tanzania.
Amesema makubaliano yaliyofikiwa yanalenga kuongeza biashara, kuvutia uwekezaji zaidi na kufungua fursa mpya za ushirikiano katika sekta mbalimbali za uchumi.
Kwa upande wa ushirikiano wa kidiplomasia, Rais Samia amesema Tanzania imeiomba Singapore kufungua ubalozi wake nchini ili kuimarisha zaidi mahusiano ya kidiplomasia na kiuchumi kati ya mataifa hayo.
Aidha, amesema nchi hizo mbili zimeanzisha mfumo wa mashauriano ya mara kwa mara ambao utasaidia kuratibu mikakati ya maendeleo na kushughulikia changamoto zinazoweza kujitokeza katika utekelezaji wa maeneo ya ushirikiano.
Katika sekta ya kilimo, Rais Samia amesema Tanzania imeonesha nia ya kushirikiana na Singapore katika mpango wa kuimarisha usalama wa chakula, hatua inayolenga kuongeza fursa za biashara ya mazao ya chakula na kuhakikisha upatikanaji wa chakula kwa uhakika katika nchi zote mbili.
Rais Samia pia amesisitiza umuhimu wa vijana katika maendeleo ya taifa, akieleza kuwa Dira ya Taifa 2050 imeweka mkazo mkubwa katika kuwawezesha vijana kwa kuwa ndio watakaobeba dhamana ya uongozi na maendeleo ya nchi katika miaka ijayo.
Ziara ya Rais Tharman Shanmugaratnam imeandika historia mpya katika mahusiano ya Tanzania na Singapore.