12/09/2025
Simulizi: NILIPEMDWA NA JINI BILA KUJUA
Mwandishi: Mwai Production
SEHEMU YA TATU
Nakiri kabisa… kuanzia pale, akili yangu ilianza kuchanganyikiwa. Niliishi k**a mtu aliyekumbatia kifo. Usiku haukuwa tena usingizi, mchana haukuwa tena mwanga. Nilitembea nikiwa roho yangu nje ya mwili. Na usiku ule ndio ulioandika kumbukumbu ya hofu ambayo sitasahau hata kaburini.
Jane alilala chumbani kwake hosteli, lakini usingizi wake haukuwa wa kawaida. Saa za usiku wa manane alijikuta ghafla ameamka akiwa si kitandani kwake… bali makaburini!
Udongo wa baridi ulikuwa umemfunika, na alipoinua kichwa, akagundua yupo juu ya kaburi jipya. Alipopepesa macho kusoma msalaba uliokuwa kichwani pa kaburi lile, damu yake iliganda. Maneno yaliyoandikwa yalichoma moyo wake moja kwa moja:
“JANE HAULE”
Tarehe ya kuzaliwa yake ilikuwa pale, na baada yake, tarehe ya kufa iliandikwa na kufunikwa kwa mstari wa deshiii —
Ndiyo, kifo chake kilikuwa bado hakijaandikwa!
Jane alipiga kelele kali, sauti ikapita katikati ya makaburi, ikitikisa utulivu wa usiku. Aliamka haraka akakimbia, lakini hapo ndipo maajabu ya hofu yalipoanza. Mikono mingi ya wafu ikaanza kujitokeza kutoka makaburini yaliyomzunguka—mikono myeupe, yenye udongo, yenye kucha ndefu na nyufa. Mikono hiyo ikaanza kumshika miguu, ikimvuta chini, taratibu ikimzonga, kana kwamba makaburi yote yalikuwa yanataka kummeza.
Jane akapiga kelele:
“Mwaaaaai! Nisaidieee! Mwaiiii!”
Ndipo giza likatikisika ghafla, na Carolina akajitokeza juu ya jiwe la kaburi, macho yake yakiwa k**a mianga ya moto. Akanena kwa sauti nzito, ikitikisa hewa yote:
“Jane! Nilikuonya. Kaa mbali na Mwai. Huyu si wa kwako, ni wangu! Ukithubutu tena… kaburi hili halitakaa liwe tupu!”
Mikono yote ya wafu ikatoweka ghafla, kana kwamba haikuwahi kuwepo. Jane akajirusha na kukimbia bila hata kuangalia nyuma. Miguu yake ikawa haina mwelekeo, macho yake yakijaa machozi ya hofu, hatimaye akajikuta amerudi hosteli, mwili wake wote ukitetemeka.
Wakati huo, mimi nilikuwa nyumbani kwangu, nikiandaa kikombe cha chai cha maziwa, nikijaribu kutuliza akili. Nilikuwa najidanganya kuwa yote ni ndoto tu. Ghafla, mlango wangu ukafunguka taratibu bila kuguswa.
Carolina akaingia.
Lakini sasa hakuwa yule kiumbe wa nyoka… alikuwa Carolina yule mrembo nilivyomzoea pale chuoni. Akavaa tabasamu la upole, akaja taratibu, na kwa sauti nyororo akasema:
“Mwai… usiogope. Siko hapa kukudhuru. Nakupenda.”
Nilihisi miguu yangu ikikataa kutembea. Nilihisi moyo wangu ukidunda kwa kasi kana kwamba unataka kuruka nje ya kifua changu. Nilihisi k**a natamani kukimbia, lakini miguu yangu ilikuwa mizito kana kwamba imenasa kwenye udongo wa kaburi. Nilishindwa hata kusogea.
Carolina akaja karibu zaidi, macho yake yakibadilika ghafla kutoka kwenye macho ya binadamu hadi ya mnyama—macho mekundu yanayowaka moto. Nilipojaribu kufumba macho, nguvu zikanipotea ghafla, nikajikuta nikiishiwa kabisa na kulala kitandani.
Ndipo jambo baya kabisa likatokea.
Nilijihisi nikibebwa na kiumbe huyo, nikilazwa kitandani, nikashindwa kupinga. Nilihisi mwili wangu ni mzito, akili yangu ikikimbia huku ikilia, lakini mwili wangu ulikuwa mateka. Carolina alinitawala.
Sijui kilidumu kwa muda gani… Lakini nilipozinduka, nilikuta nipo uchi, jasho limenilowesha mwili. Niliangaza pembeni yangu—na pale… kulikuwa na bonge kubwa la Chatu, likiwa limejikunja, macho yake yakinichungulia. Nilishindwa kupiga kelele, pumzi yangu ikakata. Nilipiga yowe kwa nguvu niliyobaki:
“Aaaaahhhhhh! Mungu wangu!”
Lakini mara moja yule Chatu akatoweka mbele ya macho yangu.
Niligeuka ukutani, na ndipo nilipoona kitu kilichonifanya nihisi roho yangu inanitoka—michirizi ya damu ikitiririka ukutani, ikichora mistari kana kwamba kuna mtu alikuwa akiandika maandiko ya laana kwa damu. Harufu ya damu ilijaa chumba kizima.
Nilivaa boxer haraka, nikajirusha kukimbia nje ya nyumba… lakini jambo la ajabu lilitokea. Kila nilipofungua mlango, nikajikuta nimerudi pale pale chumbani kwangu. Nilikimbia mara mbili, mara tatu, mara nne—lakini sikutoka nje. Nilizunguka humo humo, nikikimbia k**a mwendawazimu ndani ya mduara wa giza lisilo na mwisho.
Mwisho wa yote, nguvu zikanishia. Nikaanguka chini, nikakaa sakafuni, nikijishika kichwa huku nikilia. Hofu ya kifo na giza ikanivamia, nikajua sasa Carolina ameniteka kabisa.
Hapo ndipo nilipoelewa… mapenzi ya jini siyo zawadi—ni kifungo cha roho, ni kaburi kabla ya kifo.