10/10/2025                                                                            
                                    
                                                                            
                                            RAS LINDI SPORTS CLUB YAKABIDHI KOMBE LA SHIMIWI KWA RAS. RAS AWAPONGEZA .
Timu ya RAS Lindi Sports Club imekabidhi Kombe la Nidhamu kwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi (RAS), baada ya kushiriki mashindano ya michezo ya SHIMIWI 2025 yaliyofanyika jijini Mwanza.
Katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa timu Ndugu. Ramadhan Khatibu amemshukuru Katibu Tawala Mkoa kwa kuiwezesha timu kushiriki kikamilifu katika mashindano hayo, pamoja na kutoa shukrani za dhati kwa niaba ya familia ya marehemu Afisa Michezo wa Mkoa, Bw. Chiza Gwidegembya, aliyefariki dunia wakati timu ikiwa kwenye mashindano.
Kwa upande wake, Katibu Tawala Mkoa wa Lindi Bi. Zuwena Omary amewapongeza wanamichezo wa timu hiyo kwa Kuonesha mfano bora kinidhamu na kurejea wakiwa na Kombe la Nidhamu, Medali na Cheti vya Ushiriki pamoja na medali ya mshindi wa mbio za mita 800.
“Niwapongeze kwa namna mlivyoshiriki mashindano haya na kwa mafanikio haya mliyoyapata. Kombe hili la nidhamu nalipokea k**a msingi wa kuhakikisha Lindi tunaendelea kuwa na nidhamu, uwajibikaji na umoja katika kazi na michezo ili tuweze kufikia malengo tuliyojiwekea” alisema RAS Lindi. 
Aidha, RAS aliwataka watumishi wa serikali kuendelea kumuenzi marehemu Chiza Gwidegembya kwa kuendeleza yale yote mema aliyoyaacha,hasa katika uongozi, utendaji kazi, na mapenzi kwa michezo na kusisitiza umuhimu wa kuwa na mipango endelevu ya mashindano na hafla za michezo ili kuimarisha ushirikiano na kuongeza ari ya ushindani.
“Tuwasaidie viongozi wetu wa klabu kuandaa hafla za kimichezo kwa bajeti zilizo ndani ya uwezo wetu ambazo zitatujenga kimichezo na kujenga ushawishi miongoni mwa watumishi wenzetu kwa kupata matokeo mazuri na kuweka nia thabiti ya kushindana” Ameongeza.