08/06/2026
Wataalam wa sheria kutoka Wizara ya Katiba na Sheria leo, Juni 8, 2026, wamewapatia mafunzo maalumu waandishi wa habari mkoani Lindi kwa lengo la kuwawezesha kutoa elimu kwa wananchi kuhusu uwepo wa Kituo cha Huduma kwa Mteja pamoja na huduma mbalimbali za kisheria zinazotolewa kupitia kituo hicho, hatua inayolenga kuongeza uelewa wa wananchi na kuimarisha upatikanaji wa taarifa sahihi za masuala ya kisheria.
Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Wakili wa Serikali kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Erick Salila, amesema kuwa kituo hicho kimeanzishwa kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma za kisheria kwa wananchi, hususan wananchi wanaohitaji msaada wa kisheria au kuwasilisha malalamiko yanayohusiana na ukiukwaji wa sheria, vitendo vya uhalifu, pamoja na masuala ya rushwa.
Ameeleza kuwa kupitia mafunzo hayo, waandishi wa habari wanatarajiwa kuwa mabalozi wa kuifikia jamii kwa kuhamasisha wananchi kutambua na kutumia huduma zinazopatikana katika kituo hicho.
Aidha, wananchi wenye malalamiko, maoni au wanaohitaji ushauri kuhusu masuala ya sheria wametakiwa kutumia Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Wizara ya Katiba na Sheria kwa kuwasiliana kupitia Sanduku la Posta 315, Dodoma, simu ya bure 0800 004 004, simu ya kawaida 026 216 0360, barua pepe [email protected] au WhatsApp namba 0739 101 910.