16/04/2026
HADITHI: 𝐊𝐈𝐒𝐀𝐒𝐈 𝐂𝐇𝐀 𝐌𝐍𝐘𝐎𝐍𝐆𝐄
MTUNZI: 𝑮𝑬𝑶𝑭𝑹𝑬𝒀 𝑫𝑰𝑺𝑴𝑨𝑺
MSIMU: 01
SEHEMU: 01
Ni majira ya saa moja asubuhi katika mtaa mmoja uliopo pembezoni mwa jiji la Dodoma. Machibya alikuwa amejilaza chali, macho yake yakiwa yameganda kwenye bati chakavu la chumba chake lililojaa madoa ya kutu, kana kwamba anasoma ramani ya hatma ya maisha yake.
Kichwa chake kilikuwa kizito. Aligeuka kulia na kutazama kideli cha kuwekea unga; kimekauka mpaka kimeanza kupata vumbi. Akatazama ngazi ya viungo; hakukuwa na hata ganda la kitunguu wala harufu ya nyanya.
"Maisha gani haya?" alijisemea kwa sauti iliyovunjika, kisha akasonya kwa uchungu. "Hivi leo nikidondoka hapa, hospitali nitaenda na nini? Sina bima, sina akiba... sina hata mia mbovu."
Mawazo yake yalirudi nyuma, miezi mitano iliyopita. Kipindi hicho Machibya alikuwa "mamba" wa barabara, dereva wa bajaji mahiri jijini Dodoma. Siku hiyo, akiwa kijiweni na washikaji zake wakipiga stori, kivuli cha Mzee mmoja kilifunika kijiwe chao.
Alikuwa Mwalimu Mwita Chacha, maarufu k**a "Mzee Kauzu". Mwalimu wa hesabu mstaafu ambaye sura yake haikuwahi kujua rangi ya tabasamu tangu akiwa darasani.
"Kijana... okoa muda. Lete funguo zangu!" sauti ya Mzee Mwita ilikata hewa k**a kisu.
Machibya aliduwaa. Mapigo ya moyo yalimwenda mbio k**a bajaji iliyofeli breki mteremko wa kuelekea mkoani.
"Mzee, sijakuelewa..."
"Kijana, unaelewa wazi huwa sipendi kurudia mara mbili!"
Bila maelezo, Mzee Kauzu alichukua chombo chake na kutokomea nacho, akimwacha Machibya akiwa ameshika hewa. Tangu siku hiyo, nyota ya Machibya ilizima.
****
Akiwa bado amezama kwenye dimbwi la mawazo, mlio wa simu yake ulimshtua. Ilikuwa namba ngeni. Aliipokea kwa kusita.
"Hallo!" Sauti ya mwanamke wa makamo ilisikika upande wa pili.
"Hallo, nani mwenzangu?" Machibya aliuliza kwa sauti ya kinyonge.
"Unaongea na Mama Hilda. Namba yako nimepewa na rafiki yako aitwaye Salma," sauti hiyo ilijitambulisha.
"Salma?" Machibya alishangaa. "Salma gani, mama?"
"Salma dereva wa bajaji. Amesema wewe ni kijana mwaminifu na unatafuta kazi kwa udi na uvumba. Nina kazi ya haraka, unapatikana?"
Machibya alikaa mkao wa kueshimu kitandani. "Napatikana Mama. Kazi gani hiyo?"
"Sihitaji maelezo mengi kwenye simu. Njoo eneo la Area D, nyumba namba 42. Nitakulipa shilingi laki tano kwa kazi ya saa nne tu."
Laki tano? Kwa saa nne? Machibya alihisi k**a anaota. Alivuta pumzi ndefu. "Sawa Mama, nakuja sasa hivi."
Machibya alivaa nguo zake zilizopauka kwa haraka, akajifuta uso kwa maji ya baridi na kuelekea Area D. Moyo ulimdunda kwa matumaini, lakini sehemu ndogo ya akili yake ilikuwa ikijiuliza; kazi gani hiyo ya laki tano kwa muda mfupi kiasi hicho?
Alipofika kwenye nyumba hiyo ya kifahari, alimkuta mwanamke mmoja aliyejifunga khanga moja, macho yake yakiwa mekundu k**a mtu aliyekuwa akilia.
"Wewe ndiye Machibya?" mwanamke huyo aliuliza kwa sauti ya chini huku akitazama huku na kule kuhakikisha hakuna anayewaona.
"Ndiyo mimi Mama."
"Ingia ndani haraka," mama huyo alimvuta mkono.
Walipoingia sebuleni, harufu ya ajabu ilimpiga Machibya puani. Haikuwa harufu ya pafyum, wala haikuwa harufu ya chakula. Ilikuwa harufu ya chuma na shombo.
"Mama, kazi yenyewe ni ipi?" Machibya aliuliza akianza kupata wasiwasi.
Mama Hilda hakujibu. Alimwongoza mpaka chumba cha ndani kabisa. Alifungua mlango kwa mikono inayotetemeka. Machibya alipochungulia ndani, alihisi dunia inazunguka.
Kwenye sakafu ya marumaru, kulikuwa na mwili wa mwanamume mmoja ukiwa umelala kwenye dimbwi la damu.
Machibya alirudi nyuma kwa mshtuko, lakini kabla hajageuka kukimbia, alihisi kitu cha baridi na kigumu kikigusa kisogo chake.
"Usipige kelele kijana," sauti ya kiume na nzito ilisikika nyuma yake. "Ukijaribu kutoroka, unakuwa maiti ya pili hapa ndani. Kazi yako ni rahisi; nisaidie kuutoa huu mwili hapa na kuupoteza. Ukimaliza, laki tano yako ipo mezani... Ukikataa, utazikwa kwenye shimo moja na huyu mzee."
Machibya alijikaza kuitazama sura ya yule aliyekufa sakafuni. Macho yake yalimtoka! Alikuwa ni yule Mzee aliyemnyang'anya bajaji miezi mitano iliyopita, Mzee Mwita Chacha!
𝑱𝒆, 𝑴𝒂𝒄𝒉𝒊𝒃𝒚𝒂 𝒂𝒕𝒂𝒌𝒖𝒃𝒂𝒍𝒊 𝒌𝒖𝒖𝒃𝒆𝒃𝒂 𝒎𝒘𝒊𝒍𝒊 𝒘𝒂 𝒂𝒅𝒖𝒊 𝒚𝒂𝒌𝒆? e, Machibya atakubali kuubeba mwili wa adui yake? 𝑵𝒂 𝒉𝒖𝒚𝒐 𝒌𝒘𝒂𝒏𝒂𝒖𝒎𝒆 𝒎𝒘𝒆𝒏𝒚𝒆 𝒃𝒖𝒏𝒅𝒖𝒌𝒊 𝒏𝒊 𝒏𝒂𝒏𝒊?
USIKOSE SEHEMU YA PILI...