01/05/2026
DC SEMINDU AWAHIMIZA WATUMISHI KUONGEZA BIDII NA UWAJIBIKAJI KUTATUA CHANGAMOTO ZA WANANCHI
Wilaya ya Mbulu imeadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani leo tarehe 01/05/2026 katika viwanja vya Shule ya Sekondari Dongobesh, ambapo watumishi wa umma wamehimizwa kuongeza bidii, uwajibikaji na weledi katika utendaji wao wa kazi ili kuboresha huduma kwa wananchi.
Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mkuu wa Wilaya ya Mbulu, Mhe. Michael Semindu, aliwataka watumishi kufanya kazi kwa kujituma na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma ili kukabiliana na changamoto zinazowakabili wananchi.
“Ndugu wafanyakazi lisala yenu imebainisha changamoto zinazowakabili watumishi, niwaahidi kuzishughulikia niwaombe watumishi muendelee kufanya kazi kwa bidii, kujituma kwa uweledi na kusikiliza serikali yetu kwa usikivu ili kutatua changamoto za wananchi”. Alisema Semindu
Aidha, Semindu alisisitiza umuhimu wa watumishi kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili vinavyoathiri jamii.
“Tunamatukio mengi ya ukatili na vitendo vingine vinavyofanana, niwaase watumishi kwa nguvu yenu na ushawishi wenu kuisaidia jamii kuacha vitendo hivyo kwani ni kinyume na sheria” Alisema Semindu
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, ndugu Abubakar Kuuli, ameishukuru Serikali kwa juhudi zake za kupunguza changamoto ya upungufu wa watumishi katika halmashauri.
“Mwaka 2020/2021 nilikuwa na upungufu wa watumishi 1398 lakini kwa kipindi hiki cha miaka 5 tumepata watumishi 744, upungufu uliobakia ni watumishi 654, kwahiyo nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutuletea watumishi wengi” Alisema Kuuli
Aidha, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Vijijini, Mhe. Emanuel Nuwas, ameahidi kufikisha bungeni changamoto zilizowasilishwa na chama cha wafanyakazi, ikiwemo suala la kikokotoo kwa watumishi, ili zipatiwe ufumbuzi.
Maadhimisho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kujadili masuala ya wafanyakazi, kuimarisha mshikamano, na kuweka mikakati ya kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi katika Wilaya ya Mbulu.