04/06/2026
KAYA 173 MBULU DC ZAPIMIWA ARDHI BURE NA KUKABIDHIWA HATI ZA KIMILA KWA UFADHILI WA UCRT
Na Magreth Mbawala
Wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu wamepata ufadhili wa kupimiwa ardhi bure na kukabidhiwa hati za kimila na shirika lisilo la kiserikali la Ujamaa Community Resource Team (UCRT), kupitia mpango wa matumizi bora ya ardhi uliofanyika katika vijiji kumi.
Hafla hiyo ya kukabidhiwa hati za kimila imefanyika leo, Juni 4, 2026, katika Kata ya Endamilay, huku mgeni rasmi akiwa Mkuu wa Wilaya ya Mbulu, Mhe. Michael Semindu.
Mradi wa matumizi bora ya ardhi umefanyika katika vijiji vya Garbab, Yaeda Kati, Endalat, Dirim, Endamilay, Endanachan, Murkuchida, Harar, Mamagi na Gembakw, na kugharimu kiasi cha shilingi milioni 150.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Semindu aliwashukuru sana UCRT kwa kuona umuhimu wa kupanga matumizi ya ardhi na kuwasaidia wananchi wa kaya duni kuweza kumiliki ardhi. Pia aliwaomba waendelee kuwafikiria wananchi hao kwani uhitaji bado ni mkubwa.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Mhe. Yeconia Delless, aliishukuru UCRT kwa kupanga matumizi bora ya ardhi katika vijiji hivyo, akieleza kuwa mpango huo umepunguza migogoro ya ardhi na mipaka baina ya vijiji. Aidha, alisema wananchi sasa wana uwezo wa kukopa katika taasisi za fedha kwa kutumia hati hizo.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Ndugu Abubakar Kuuli, alimshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mazingira yanayowezesha mashirika yasiyo ya kiserikali kushirikiana na serikali katika maendeleo ya wananchi. Pia aliishukuru UCRT na kuiomba iendelee kutoa msaada huo, kwani ni vijiji 25 tu kati ya vijiji 76 vilivyopata mpango wa matumizi bora ya ardhi.
Sambamba na hilo, Mratibu wa Mradi wa Wilaya ya Mbulu, Bw. Dismas Metaya, aliushukuru uongozi wa Wilaya na Halmashauri kwa ushirikiano walioutoa katika kipindi chote cha utekelezaji wa mradi. Pia aliwasihi wananchi kuendelea kutunza mazingira kwa kuepuka ukataji holela wa miti.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na wananchi pamoja na viongozi mbalimbali kutoka vijiji na kata zilizonufaika na mradi huo.