08/03/2026
Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kwa Mkoa wa Mtwara mwaka huu yamefanyika katika Wilaya ya Masasi kwenye Viwanja vya Sabasaba Masasi Mjini, yakihusisha mamia ya wanawake pamoja na wadau mbalimbali kutoka taasisi za serikali na zisizo za serikali.
Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Donald Msengi, ambaye aliongoza wananchi katika tukio hilo lililoambatana na shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi.
Shughuli za maadhimisho zilianza kwa maandamano yaliyowashirikisha wanawake kutoka makundi tofauti wakiwemo wafanyabiashara, vikundi vya wanawake wajasiriamali, watumishi wa umma, wanafunzi pamoja na wanachama wa mashirika mbalimbali. Maandamano hayo yalipita katika mitaa mbalimbali ya Mji wa Masasi kabla ya kuhitimishwa katika Viwanja vya Sabasaba.
Katika viwanja hivyo kulifanyika maonyesho maalum ya kazi na bidhaa mbalimbali zinazozalishwa na wanawake wajasiriamali pamoja na taasisi za serikali na zisizo za serikali. Maonyesho hayo yalilenga kuonesha mchango wa wanawake katika maendeleo ya kiuchumi na kuhamasisha jamii kuunga mkono juhudi za wanawake katika shughuli za uzalishaji na biashara.
Aidha, maadhimisho hayo yalipambwa na burudani mbalimbali zikiwemo ngoma za asili, muziki na vikundi vya sanaa vilivyotumbuiza na kutoa ujumbe wa kuhamasisha haki, usawa na uwezeshaji wa wanawake na wasichana katika jamii.
Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara aliwahimiza wanawake kuendelea kushirikiana, kujituma katika shughuli za maendeleo na kutumia fursa zilizopo kujikwamua kiuchumi huku akisisitiza umuhimu wa jamii kuendelea kulinda haki za wanawake na wasichana.
Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani huadhimishwa kila mwaka tarehe 8 Machi, yakilenga kutambua mchango wa wanawake katika maendeleo ya jamii pamoja na kuhamasisha usawa wa kijinsia duniani.