26/07/2025
Mkuu wa wilaya ya Kusini Unguja Othman Masudi amesisitiza kuendelea kudumisha na kuilinda tunu ya muungano ilioachwa na waasisi wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na Abeid Aman Karume pamoja na kuendelea kuimarisha amani na utulivu kuelekea uchaguzi mkuu.
Ameyasema hayo katika mapokezi ya Jukwaa la walimu wazalendo kutoka mikoa 7 ya Tanzania bara waliowasili visiwani Zanzibar kwa ziara ya kikazi ya siku 3 itakayoangazia kubadilishana uzoefu,kutembelea maeneo ya kihistoria pamoja na miradi ya kimkakati inayotekelezwa na serikali chini ya Dr.Hussein Ally Mwinyi.
Aidha ameongeza kuwa Zanzibar katika sekta ya utalii inachangia pato la serikali kwa asilimia 30 kupitia utalii wa ndani hivyo kufanyika kwa ziara hiyo ni ishara ya muamko wa kufanya utalii wa ndani bila ya kutegemea wageni.
Hata hivyo katibu mtendaji wa taasisi ya Vijana nguvukazi kutoka kizimkazi Abuusuphian Yakuti Juma pamoja na mratibu wa jukwaa la walimu wazalendo kutoka Morogoro Mwl Kassimu Mandwanga wamesema ziara hiyo ina lengo la kuendeleza mahusiano mazuri yaliyopo baina ya walimu kutoka mikoa ya Tanzania bara na Zanzibar,kukuza utalii, kudumisha muungano na kuhamasisha dhana ya kushiriki uchaguzi.
Katika ziara hiyo ya Muungano kupitia Jukwaa la walimu wazalendo wanatarajia kutembelea maeneo mbalimbali ya kihistoria katika mikoa ya Mjini Unguja,Kaskazini Unguja na Kusini Unguja,kuzuru kaburi la hayati Ally Hassan Mwinyi,mradi wa bandari,na kutembelea maeneo ya kasa.
Walimu hao ni kutoka mikoa ya Morogoro,Tanga,Pwani,Dar es salaam,Shinyanga,Mbeya na Kigoma ambapo wametembelea Zanzibar kwa mualiko rasmi wa Taasisi ya Vijana nguvu kutoka Kizimkazi mkoa wa Kusini Unguja.