18/12/2025
TRA YAFANYA ZIARA YA KURUDISHA SHUKRANI KWA WALIPAKODI
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Morogoro imefanya ziara ya kutembelea walipakodi mbalimbali mkoani humo kwa lengo la kutoa pongezi na kurudisha shukrani kwa walipaji kodi kwa hiari bila shuruti.
Katika ziara hiyo, maafisa wa TRA wamepata fursa ya kuzungumza moja kwa moja na walipakodi, wakiwapongeza kwa uzalendo wao na mchango mkubwa wanaoutoa katika maendeleo ya taifa kupitia ulipaji sahihi wa kodi. TRA imeeleza kuwa walipakodi hawa ni mfano wa kuigwa, kwani wanatekeleza wajibu wao wa kikatiba bila kusubiri ushawishi au hatua za kisheria.
Aidha, TRA Morogoro imesisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha mahusiano mazuri kati ya mamlaka na walipakodi, pamoja na kujenga utamaduni wa kulipa kodi kwa hiari na uaminifu. Walipakodi waliotembelewa wameeleza kufurahishwa na kitendo hicho, wakieleza kuwa kinawapa motisha ya kuendelea kutimiza wajibu wao kwa uaminifu zaidi. na wamewashauri walipa kodi wengine waweze kutimiza wajibu wao kwa kulipa kodi kwani kodi hizo ndio maendeleo ya nchi yetu.
TRA imewahakikishia walipakodi kuendelea kutoa elimu ya mlipa kodi, huduma bora na ushirikiano wa karibu ili kuhakikisha mazingira rafiki ya ulipaji kodi yanaimarika kwa maendeleo endelevu ya nchi yetu.