03/05/2025
Wakati Jeshi la Polisi likiendelea na uchunguzi wa kupotea kwa mwanaharakati na kada wa Chadema, Mdude Nyagali, viongozi na wafuasi wa chama hicho Mkoa wa Mbeya wameanzisha jitihada za kumtafuta katika maeneo ya porini.
Msako huo umeanza baada ya viongozi sita wa Chadema, wakiwa na wafuasi 58, kuandamana leo mchana, Jumamosi, Mei 3, 2025, hadi Ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, wakitaka kupata taarifa kuhusu mambo mawili.
Mambo hayo ni kwanza, hatua zilizofikiwa katika uchunguzi wa tukio la kupotea kwa Mdude Nyagali, na pili, kufuatilia makubaliano yao ya awali ya kushirikiana na Jeshi la Polisi katika juhudi za kumtafuta.
Akizungumza na Knews24 Media LTD, kwa njia ya simu leo Jumamosi, Mei 3, 2025, Katibu wa Chadema Mkoa wa Mbeya, Hamad Mbeyale, amesema kuwa kutokana na ukimya uliokuwepo kuhusu kupotea kwa Mdude Nyagali, leo baadhi ya viongozi na wafuasi 58 wa chama hicho wamelazimika kuandamana hadi Ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya.
"Tumeenda na madai mawili. La kwanza ni kuhusu makubaliano yetu na Jeshi la Polisi tuliyofikia jana, Mei 2, 2025, ya kushirikiana katika kumtafuta k**anda wetu Mdude, hasa walipokuwa eneo la tukio. Hata hivyo, hadi leo asubuhi hakuna dalili yoyote ya ushirikiano wala harakati zozote kutoka kwa Polisi," amesema Mbeyale.
Ameongeza kuwa lengo la maandamano hayo ni kufuatilia hatima ya kupatikana kwa kada huyo, pamoja na kupata uhakika wa usalama wao binafsi katika harakati wanazoendelea nazo.
Amesemawanachama na viongozi wa majimbo wameamua kuingia maporini kwa ajili ya kumsaka Mdude Nyagali, awe hai au amekufa.