21/08/2026
Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imemruhusu mtoto aliyefanyiwa upasuaji wa kwanza wa kutenganishwa na pacha aliyeungana aina ya parasitic conjoined twins, baada ya kuendelea vizuri kwa siku 10 tangu kufanyika kwa upasuaji huo wa kihistoria.
Mtoto huyo alifanyiwa upasuaji huo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, ikiwa ni hatua muhimu katika historia ya huduma za ubingwa na ubingwa bobezi wa matibabu nchini Tanzania.
Kwa mujibu wa taarifa ya Muhimbili iliyotolewa leo, Agosti 21, 2026, mtoto huyo ameendelea vizuri baada ya kutenganishwa na pacha huyo na sasa ameruhusiwa kuendelea na matibabu na uangalizi akiwa nyumbani.
Upasuaji huo wa kutenganisha pacha wa aina ya parasitic conjoined twins umeelezwa kuwa ni miongoni mwa hatua kubwa katika maendeleo ya huduma za kibingwa nchini, huku ukionesha uwezo wa wataalamu wa afya kufanya upasuaji changamani unaohitaji utaalamu wa hali ya juu.
Mafanikio hayo yanaongeza matumaini kwa watoto wenye changamoto zinazohitaji huduma maalumu za upasuaji, pamoja na kuonesha umuhimu wa kuendelea kuimarisha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi katika hospitali za Tanzania.